Mbunge Kubenea asema hana bei

KUBENEA: CCM HAWANA JIPYA LA KUNIPELEKA HUKO

Muktasari:

Ameituhumu CCM kuwa inataka kuzima harakati za upinzani kuhoji masuala mbalimbali.

Dar es Salaam. Mbunge wa Ubungo (Chadema), Saed Kubenea amesema hana bei na hawezi kuwa msaliti.

Kubenea ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Pwani, leo Jumatano Desemba 6,2017 akizungumza na waandishi wa habari amesema mwenye ushahidi kwamba amenunuliwa ili kuhama chama hicho auweke hadharani.

"Sina bei na sinunuliki. Taarifa juu yangu ni uzushi mtupu, hakuna ukweli na kama kuna mtu ana ushahidi aweke mezani," amesema Kubenea.

Ameituhumu CCM kwamba inataka kuzima harakati za upinzani kuhoji masuala mbalimbali, ikiwemo ubomoaji wa makazi ya watu na mikataba.

"Siwezi kuwa msaliti kama wabunge wengine na madiwani ambao wanaacha kazi ya ubunge kwa kumuunga mkono Rais John Magufuli," amesema Kubenea.