Macron atua Mali, aapa kuwamaliza magaidi

Bamako, Mali. Rais Emmanuel Macron amefanya ziara ya kwanza katika bara la Afrika kwa kuitembelea Mali ambako amesema Ufaransa haitarudi nyuma katika vita dhidi ya magaidi na wapiganaji wengine wa kijihadi katika nchi hiyo na eneo la Sahel.

Macron alitoa kauli hiyo jana baada ya kuwatembelea wanajeshi wa Ufaransa katika kambi yao ya Gao, kaskazini mwa nchi hiyo, ambako wanaisaidia Mali kurejesha hali ya utulivu na amani. Ufaransa imewatuma wanajeshi wake 1,600 kaskazini mwa Mali kupambana na magaidi.

Huku akiwa na mwenyeji wake Rais Ibrahim Boubacar Keita, Macron alisema mbali ya Ufaransa, Ujerumani pia itaendelea kuhakikisha kuwa magaidi hao wanashindwa. “Ujerumani wapo nasi katika operesheni hizi,” alisema.

Aidha, amesema kuwa ushirikiano wa Ufaransa na Ujerumani ni muhimu sana barani Ulaya katika masuala ya usalama lakini pia kulisaidia bara la Afrika.