Azam wapigwa butwaa Yanga kumsajili Gadiel

Muktasari:

Gazeti hili kupitia vyanzo vya uhakika vilivyo ndani ya Yanga, lilithibitishiwa kuwa beki huyo amemwaga wino Jangwani jambo lililowaibua Azam na kuamua kukomaa na beki huyo wa kushoto.

Taarifa za beki Gadiel Michael kusaini mkataba wa miaka miwili Yanga zimewashtua Azam ambao wametoa angalizo kuwa bado ana mkataba wa miezi sita na timu yao.

Gazeti hili kupitia vyanzo vya uhakika vilivyo ndani ya Yanga, lilithibitishiwa kuwa beki huyo amemwaga wino Jangwani jambo lililowaibua Azam na kuamua kukomaa na beki huyo wa kushoto.

"Tunaziona tu taarifa kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii kuwa Gadiel amesaini mkataba wa kuichezea Yanga. Tunashangaa kwa kuwa bado tuna mkataba naye.

Mkataba wa Gadiel na Azam unamalizika mwezi Desemba hivyo kama kweli wamemsainisha mkataba  basi watakuwa wamefanya makosa kwa sababu sheria haziruhusu kumsainisha mchezaji ambaye ana mkataba na timu nyingine," alisema Meneja wa Azam, Phillip Alando.