Ofisa ustawi kizimbani kwa rushwa

Muktasari:

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Juni 19 mwaka huu na mtuhumiwa ameachiwa  baada ya kutimiza masharti ya dhamana.

Dar es Salaam. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) imempandisha kizimbani Ofisa Ustawi wa Jamii wa  vituo vya mahakama za Mwanzo,  Deogratius Shirima (35)  kwa makosa mawili likiwemo kuomba na kupokea rushwa ya Sh200,000 kutoka kwa Hamadi Mussa.

Akisoma hati ya mashtaka katika Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni, Wakili wa Takukuru Faraja Sambala  amedai kuwa katika shtaka la kwanza, mtuhumiwa ambaye mwajiriwa katika Wizara ya Mambo ya Ndani, Mei 11 mwaka 2017 ndani ya Manispaa ya Kinondoni alimashawishi Mussa ili  kujipatia fedha hizo,

Sambala alidai kuwa mtuhumiwa huyo ambaye alikuwa ofisa wa ustawi wa jamii wa vituo vya mahakama za Mwanzo, Wilaya na Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Dar es Salaam akiwa katika eneo lake la kazi alimshawishi Mussa mwenye kesi ya jinai yenye namba 275/ 2017 huku akijua kuwa kufanya hivyo ni kinyume cha sheria ya nchi.

Shtaka la pili mtuhumiwa anakabiliwa na kosa la kupokea kiasi hicho cha fedha ambapo inadaiwa tukio hili lilitokea Mei 16 mwaka huu maeneo ya Manzese Tiptop.

Baada ya maelezo hayo mtuhumiwa alikana kutenda makosa hayo  ambapo wakili alidai upelelezi bado unaendelea hivyo kuomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.

Hakimu Mkazi, Caroline Kiliwa alisema shtaka hilo linadhaminika kwa mujibu wa sheria, alimtaka mtuhumiwa awe na wadhamini wawili ambao ni ndugu wa karibu walioajiriwa serikalini au taasisi inayotambulika kisheria ambao wataweka saini ya maandishi ya Sh500,000  kwa kila mmoja.