Sumu yakwamisha Afrika kupenya Ulaya

     Mkurugenzi wa usalama wa chakula wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Raymond Wigenge     

Muktasari:

Hayo yalibainishwa jana na mkurugenzi wa usalama wa chakula wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Raymond Wigenge kwenye kongamano la udhibiti wa sumu kuvu kwa kushirikina na wadau kutoka umoja wa Afrika kupitia programu ya udhibiti wa sumu kuvu (PACA).

       Dar es Salaam. Inakadiriwa mwaka 2014 nchi za Afrika zilipata hasara ya Dola 670 milioni za Marekani kwa kushindwa kuuza vyakula katika Jumuiya ya Ulaya (EU), kutokana na sumu kuvu.

Hayo yalibainishwa jana na mkurugenzi wa usalama wa chakula wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Raymond Wigenge kwenye kongamano la udhibiti wa sumu kuvu kwa kushirikina na wadau kutoka umoja wa Afrika kupitia programu ya udhibiti wa sumu kuvu (PACA).

Wigenge alisema uwapo wa sumu kuvu katika vyakula unaosababishwa na baadhi ya fangasi wanaoingia ikiwamo mahindi, imekuwa changamoto kubwa hivyo huathiri ukuaji wa biashara ya vyakula.

Alisema inakadiriwa watu milioni 208 katika bara la Afrika wanategemea mahindi kama chakula kikuu, hivyo kupata mbinu mwafaka za udhibiti wa sumu kuvu kutapunguza tatizo hilo.

Wigenge alisema nchi 16 kati ya 22 zinategemea mahindi duniani zimeathirika.

Pia, alisema inakadiriwa asilimia 30 ya wagojwa wa kansa ya ini barani Afrika, wanapata tatizo hilo kupitia ulaji wa vyakula vyenye sumu kuvu hivyo jitihada zaidi zinahitajika kuhakiisha hali hiyo inadhibitiwa.

Alisema tatizo hilo linaweza kusababisha baadhi ya watoto kupata ugonjwa wa udumavu, hivyo hatua za udhibiti zinatakiwa kuanzia kwa wakulima.

Naye mshauri wa sumu kuvu kutoka Umoja wa Afrika wa Udhibiti wa Sumu Kuvu (Paca), Profesa Martin Kimanya alisema tatizo ni kubwa kwa sababu linahusu maisha ya binadamu kila siku.

Profesa Kimanya alisema mahindi yanapobanguliwa shambani kunakuwa na fangasi ambao wanaingia kwenye mbegu, hivyo kusababisha madhara kwa watumiaji.

Alisema asilimia 30 ya watumiaji wa mahindi kwa nchi za Kenya na Tanzania, wanakabiliwa na hatari ya kupata athari zitokanazo na sumu hiyo.

Pia, alisema lazima Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wahakikishe tatizo hilo linadhibitiwa. “Vyama vya wakulima, watafiti, wataalamu wa kilimo na wa lishe tushirikiane kuondoa tatizo hili mapema,” alisema.