Walimu hamjashushwa vyeo, Serikali yawaambia waliohamishiwa msingi

Muktasari:

Taarifa ya mkuu wa kitengo cha mawasiliano Ofisi ya Rais (Utumishi), Florence Lawrence iliyotolewa jana imesema Serikali kuwapangia baadhi ya walimu wa sekondari kufundisha shule za msingi ni moja ya hatua za kuongeza ufanisi na kuleta mgawanyo sawa wa walimu katika shule hizo.

Serikali imesema mwalimu wa sekondari kufundisha shule ya msingi si kushushwa cheo na wala si jambo la ajabu.

Taarifa ya mkuu wa kitengo cha mawasiliano Ofisi ya Rais (Utumishi), Florence Lawrence iliyotolewa jana imesema Serikali kuwapangia baadhi ya walimu wa sekondari kufundisha shule za msingi ni moja ya hatua za kuongeza ufanisi na kuleta mgawanyo sawa wa walimu katika shule hizo.

Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dk Laurean Ndumbaro alikaririwa katika taarifa hiyo akisema hatua hiyo haimaanishi kuwa walimu wanaotoka katika shule ya sekondari kwenda kufundisha msingi wameshushwa cheo.

Dk Ndumbaro alitoa ufafanuzi huo katika kikao kazi na watumishi wa Halmashauri ya Mji wa Makambako.

Alisema lengo la Serikali ni kuondoa upungufu wa walimu katika shule za msingi na kuimarisha utoaji wa elimu.

Katibu mkuu huyo alisema sifa za kufundisha na kiwango cha elimu zinaendana na mabadiliko yanayotokea duniani, hivyo mwalimu mwenye elimu ya kiwango cha shahada ya kwanza kufundisha shule ya msingi isionekane ni jambo la ajabu.

Dk Ndumbaro aliwaeleza watumishi wa umma kuwa maendeleo katika sekta yoyote ikiwamo ya elimu yanakuja na mabadiliko hivyo wayapokee na kufanya kazi ili kufikia lengo.