Asilimia 70 ya watu maskini hufariki dunia kwa saratani

Muktasari:

Saratani ni moja ya janga hatari katika afya zetu kwani wengi wa wagonjwa hushindwa kupona na huugua kwa muda mrefu na kupata mateso makubwa kabla ya kufariki dunia.

Kadiri dunia inavyopiga hatua za kiuchumi katika maeneo ya nchi zinazoendelea ndivyo pia magonjwa yasiyoambukiza yanavyozidi kujitokeza na kuipa hofu jamii.

Saratani ni moja ya janga hatari katika afya zetu kwani wengi wa wagonjwa hushindwa kupona na huugua kwa muda mrefu na kupata mateso makubwa kabla ya kufariki dunia.

Saratani kwa lugha ya kitabibu hujulikana kama malignancy, cancer, neoplasm au tumour kwa lugha ya Kiingereza ni new growth. Pia kwa Kiswahili hujulikana uvimbe unaosambaa.

2008 peke yake watu milioni 7.6 walikufa kwa saratani duniani kote, hii ilikua ni sawa na asilimia 13 ya vifo vyote ndani ya mwaka huo.

Hata hivyo, utafiti umebaini asilimia 70 ya saratani zinatokea katika maeneo mengi wanayoishi watu wa hali ya chini katika nchi mbalimbali.

Pia, inaelezwa saratani inashika nafasi ya pili kwa kusababisha vifo vingi kwa nchi zilizoendelea huko magharibi baada ya ugonjwa wa moyo.

Imefika mahali baadhi ya nchi duniani zimeamua kupitisha sheria inayoruhusu kumpa huduma ya kifo cha huruma, kifo kisicho na maumivu mtu anayeugua ugonjwa huyo.

Pamoja na kupingwa kwa huduma hizi kutokana na kutoendana na maadili ya tiba, lakini nchi hizo ziliamua kufanya hivyo baada yakuona mateso makali nay a muda mrefu wanayoyapata wagonjwa hawa.

Saratani inaanzaje

Ni hali inayojitokeza baada ya chembe hai za mwilini yaani seli kukua kiholela baada ya kutokea mparanganyika ndani ya chembe hai.

Saratani ni ugonjwa unaotokea baada ya chembe hai zisizo za kawaida kuzaliana na kuongezeka idadi pasipo kudhibitiwa, hivyo kuweza kuvamia sehemu nyingine za mwili na kuleta madhara.

Chembe hai za saratani huweza kusambaa maeneo mengine ya mwili kupitia mfumo wa damu na mfumo unaochuja vimelea vya maradhi unaoitwa lymph na tishu zilizo jirani ilipo saratani.

Ipo tofauti kubwa katika kupata saratani kwa upande wa umri, jinsia na mazingira tunayoishi.

Tofauti ya kiuchumi na kimaendeleo katika baadhi ya maeneo, huweza kuonekana katika kujitokeza kwa saratani mbalimbali.

Mojawapo ni ile ya uvimbe mgumu kama ya mapafu na matiti zinazojitokeza zaidi katika nchi zilizoendelea.

Hatari ya mtu kupata saratani ya mapafu ni mara nne zaidi kwa mtu anayeishi nchini Uingereza ukilinganisha na mtu aliyeishi India.

Tofauti nyingine ya kimaeneo ni ya saratani ya shingo ya uzazi.

Kwa nchi za Carribien, saratani hii inashika namba mbili kwa kusababisha vifo vya wanawake.

Kwa nchi zilizo kusini mwa Jangwa la Sahara, saratani ya mlango au shingo ya uzazi, Tanzania ndiyo inaongoza kwakuwa na idadi kubwa ya wagonjwa.

Saratani si ugonjwa mmoja, bali ni maradhi zaidi ya moja kwani athari zake huibuka na dalili tofauti kadiri zinavyovamia mfumo mmoja kwenda mwingine.

Zipo takribani aina 100 za saratani, huweza kupewa jina kutokana na mahali iliposhambulia mwilini na aina ya chembe hai zilizoathirika.

Mfano saratani zinazoanzia kwa jina la chembe hai za ngozi ziitwazo melanocytes, huitwa melanoma wakati zile za utumbo mpana (colon) huitwa saratani coloni

Aina za saratani huweza kuainishwa katika makundi mbalimbali kutegemeana na mahali na aina ya tishi iliyoathiri.

Zifuatazo ni saratani na aina yake.

Carcinoma - saratani hii huanzia katika ngozi au tishu zinazofunika viungo vya ndani.

Sarcoma, hii ni saratani inayoanzia kwenye mifupa migumu, mifupa plastiki, misuli, sehemu zenye mafuta mengi na kwenye mishipa ya damu.

Leukemia, saratani hii huanzia katika tishu zinazotengeneza chembe hai, mfano (bone marrow) ute wa njano uliopo katikati ya mifupa, husababisha kutengeneza chembe hai zenye saratani na huingia moja kwa moja katika mfumo wa damu.

Lymphoma na myeloma saratani hizi huanzia katika chembe hai za mfumo wa kinga.

Mfumo wa fahamu ubongo na uti wa mgongo; saratani zilizoanzia katika chembe hai za ubongo ziitwazo neuroni.

Saratani inavyotokea katika mwili

Saratani zote huanzia ndani ya chembe hai. Hizo ndiyo muhimili mkuu wa kazi za kimwili. Ili kuweza kujua saratani inavyotokea, ni vema kujua nini kinatokea kwa chembe hai ya kawaida yenye afya na kubadilika na kuwa chembe hai iliyoathirika yenye saratani.

Mwili umeundwa kwa chembe hai tofauti ambazo huhitajika ili kuuweka mwili kwenye afya njema.

Chembe hai za mwili hujidhibiti katika ukuaji kimaumbile na kujiongeza idadi au kujigawanya.

Wakati seli zinapozeeka au kupata madhara, hufariki au kuuwawa na askari mwili, hivyo nafasi yake huchukuliwa na chembe hai mpya.

Seli hizi hupitia katika mizunguko mikuu miwili, yaani Meosis na Mitosisi. Mzunguko wa mitosis, seli moja hujigawa na kuwa seli mbili.

Pale inapotokea mparaganyiko wa vitu vya ndani ya seli vilivyobeba taarifa za kiurithi na maelekezo ya kimwili za vinasaba (DNA), huweza kuvurugwa na kukosa ufanisi.

Hali hii huleta matatizo katika mzunguko na kusababisha mtiririko usio wa kawaida. Pia, huleta matokeo mabaya ya ukuaji na ugawanyikaji wa seli kiholela usio wakawaida.

Basi hali hii ikitokea, seli hushindwa kufa pale inapohitajika ife na pia seli mpya huzalishwa pasipo mwili kuzihitaji.

Seli hizi za ziada zenye saratani kwa pamoja, hujirundika katika tishu na kuvimba, ndio huitwa Saratani.

Bado hakuna uthibitisha wa moja kwa moja kujua sababu hasa ya kisayansi kutokea kwa saratani, lakini kuna vitu au tabia hatarishi na vihatarishi vinavyoambatana na saratani mbalimbali kama dawa aina ya Cytotoxic huambatana na kujitokeza kwa saratani ya damu maarufu leukemia.

Maambukizi ya kichocho huambatana na saratani ya kibofu cha mkojo, kirusi cha papiloma namba 16 na 18, saratani ya shingo ya uzazi na siku za karibuni inahusishwa pia na saratani ya koo na bomba la chakula.

Jenetiki au chembe za kiurithi, inahusishwa na kujitokeza na saratani ya matiti na kokwa za mayai ya uzazi hasa kwa wanawake na utumbo mpana.

Mienendo na mitindo yakimaisha ni moja ya tabia na vitu hatarishi katika nchi za magharibi ambako watu hupata saratani kama ya matiti na utumbo mpana, lakini chanzo chake bado hakijajulikana.

Pia utumiaji wa tumbaku umeonekana kuwa sababu kubwa inayochochea karibu saratani zote ingawa zaidi ni kwa ya mapafu, kibofu, kichwa na shingo.

Unywaji wa pombe kupita kiasi husababisha saratani ya koo, sumu ya aflatoxin na saratani ya ini.

Mazingira yakufanyia kazi ikiwamo maeneo yenye mabati aina ya asbestos, husababisha saratani ya mesotholioma, kemikali ya aniline dyes yenyewe inasababisha saratani ya kibofu na mionzi ya jua husababisha saratani ya ngozi.

Vyakula vya wanyama na vyakusindika kama vya makopo vyenye kemikali za kuzuia kuharibika, vyakula vilivyo ambatana na uchafu, virusi vya HIV, kuwa na uzito au mwili wenye mafuta mengi, kutofanya mazoezi, matumizi ya dawa za kulevya, mazingira ya mwili kutokua safi, ngono zembe, majeraha sugu au ya mara kwa mara mwilini pia husababisha saratani.

Kuwa na historia yakifamilia ya kuugua saratani kwa zaidi ya mwaka mmoja na pia baadhi ya vichochezi vya mwili mfano oestrogeni vimeonekana kuambatana na saratani ya matiti.

Pamoja na kutaja sababu na mambo hatarishi, haimanishi kua kila mtu anayefanya hayo atapata saratani, kupata au kutopata hutegemeana na ubora na uwezo wa mwili wa mtu mwenyewe kupambana na maradhi.