Changamoto ya kutibu pumu

Muktasari:

  • Pumu kitaalamu inaitwa Asthma ni ugonjwa hatari unaohitaji huduma za dharula, hatua stahiki zisipochukuliwa, mgonjwa anaweza kupoteza maisha.

Mara nyingi watu wengi hupenda kusikiliza na kuzingatia maelekezo mengi ambayo si sahihi wanayoelezwa na watu mitaani. Kwa mfano, mtu anaugua Pumu, badala ya kumpeleka hospitali, anashauriwa na watu ampatie dawa bila kupima au aende kwenye tiba za asili, mwisho wa siku mgonjwa anapoteza maisha au anazidi kuugua bila kupona. Wakati angempeleka kwa wataalamu wa afya, angeweza kupata ufumbuzi wa tatizo hilo.

Pumu kitaalamu inaitwa Asthma ni ugonjwa hatari unaohitaji huduma za dharula, hatua stahiki zisipochukuliwa, mgonjwa anaweza kupoteza maisha.

Ugonjwa huu wenye tabia ya kusababisha mirija ya hewa kusinyaa, kukakamaa au wakati mwingine kuziba kabisa, huifanya hewa ishindwe kuingia na kutoka kwenye mapafu kutokana na njia hiyo kuwa nyembamba.

Ugonjwa wa pumu huathiri sehemu ya kupitisha hewa kwenda kwenye mapafu ya binadamu kupitia mirija myembamba ya inayojulikana kitaalamu bronchioles.

Hali hiyo humfanya muathirika kushindwa kuvuta na kutoa hewa nje, hivyo kupumua kwa shida.

Tatizo hili linaweza kudumu kwa muda mfupi au mrefu kiasi cha kuhitaji tiba ili kumuwezesha mgonjwa kupata nafuu.

Mtu anayeugua pumu, hudumu nayo karibu kipindi chote cha maisha yake.

Aina ya pumu

Pumu imegawanyika katika makundi mawili; ipo ile ya ghafla inayoitwa kitabibu Acute asthma, mgonjwa aliye kwenye kundi hili hali yake huwa ya kawaida kwenye njia ya hewa isiyobadilika kati ya shambulizi moja na jingine.

Kundi lingine ni Pumu sugu (Chronic Asthma). Kundi hili huwa na tabia ya kuwa na njia nyembamba za kupitisha hewa na kadiri mgonjwa anavyoendelea kupata matukio zaidi ya kuumwa, njia za hewa huzidi kuwa nyembamba na kusinyaa zaidi.

Bila kujalisha mgonjwa anaingia katika kundi gani, ugonjwa wa pumu unaweza kugawanywa katika aina kuu nne, ambazo ni:

Pumu inayobadilika (brittle asthma)

Kulingana na tabia ya kujirudia kwa matukio ya ugonjwa huo na madhara yake kwa mgonjwa, aina hii ya pumu inaweza kugawanywa zaidi katika aina nyingine mbili, ambazo ni pamoja na ile inayobadilika ambayo ina tabia ya kujirudia kutokana na matukio na mashambulizi ya kubadilika kila mara japokuwa mgonjwa anaweza kuwa anapata matibabu kadhaa.

Aina ya pili ni pumu inayobadilika ambayo mgonjwa anaweza kupata shambulizi la ghafla hata kama awali iliweza kuthibitiwa kwa matibabu.

Aina ya tatu ni Pumu hatari isiyobadilika. Pamoja na matumizi ya dawa kadhaa, zikiwamo za vitanua njia za hewa (bronchodilators) na vipoza mcharuko mwili (steroids), mgonjwa bado anaweza asipate nafuu ya haraka na anaweza kupoteza maisha.

Ipo pia pumu inayosababishwa na mazoezi (Exercise Induced Asthma)

Hali hii husababishwa na ufanyaji wa kupitiliza wa mazoezi ya viungo.

Kwa kawaida wakati wa kufanya mazoezi mtu hupumua kwa kutumia pua na mdomoni. Wakati mwingine inaweza kutokea hewa aivutayo huingia ndani ikiwa haijapozwa vya kutosha puani na kusababisha ongezeko la mtiririko wa damu katika mishipa inayosambaza damu katika mirija ya kupitisha hewa.

Hali hii husababisha kuvimba kwa kuta za mirija hiyo na muhusika kupata shambulizi la pumu. Aina hii ya pumu yaweza kudhibitiwa na dawa.

Inashauriwa kwa watu wenye matatizo kama haya, kupasha moto misuli kwa mazoezi mepesi kabla ya kuanza mazoezi mazito na ya muda mrefu.

Ipo pia Pumu inayosababishwa na aina ya kazi. Mazingira ya kazi yanaweza kusababisha kutokea kwa pumu hata kwa baadhi ya wafanyakazi wasio na tatizo hilo.

Aina hii huweza kuwatokea watu wanaofanya kazi kwenye viwanda vya kutengeneza matairi, vigae, rangi, kemikali mbalimbali, mbolea, chuma, unga, mbao na nguo.

Pumu husababishwa na nini?

Kuna mambo kadhaa yanayoweza kusababisha shambulizi la pumu.

Mambo hayo ni pamoja na matatizo ya kinasaba.

Haya yanamhusisha mtu kwa karibu asilimia 90 hususani kipindi cha utoto.

Uvutaji wa sigara au tumbaku kipindi cha ujauzito pia unahusishwa na kusababisha pumu kwa mtoto atakayezaliwa.

Maendeleo ya kiuchumi

Ugonjwa wa pumu unaibuka sana kwenye nchi zilizoendelea kiuchumi ikilinganishwa na zenye maendeleo duni.

Magonjwa ya mapafu kama bronchitis, vyanzo vya mzio (allergens) ya vumbi, vinyesi vya wanyama na baadhi ya vyakula ni chanzo kimojawapo.

Uchafuzi wa mazingira kama moshi na baadhi ya harufu kali na kemikali kwenye maeneo ya kazi hasa ya viwanda yapo zaidi kwenye nchi zilizoendelea.

Hata hivyo, baadhi ya wagonjwa wanaotumia dawa za kushusha shinikizo la damu zilizo katika jamii ya beta-blockers ikiwamo propanolol, pia wapo katika hatari ya kupata shambulio la pumu.

Hatari ya ugonjwa wa pumu

Uwezekano wa kupata ugonjwa wa pumu huongezeka iwapo mtu atakuwa na maradhi ya mzio, magonjwa ya ngozi au homa isababishwayo na aina fulani ya vumbi au kama atavuta chavu (pollen) kutoka kwenye maua au miti na kama atajihusisha na uvutaji sigara au kama ana historia ya ugonjwa wa pumu au mzio kwenye familia yao.

Dalili za ugonjwa wa pumu

Dalili za pumu ni pamoja na kuishiwa pumzi, kupumua kwa shida, kutoa sauti kama mtu anayepiga miluzi wakati wa kupumua (wheezing).

Kukohoa sana nyakati za usiku au asubuhi. Pia, kuwa na kikohozi kinachoambatana na kutoa makohozi mazito yasiyo na rangi au yenye rangi ya njano.

Mtu aliyepatwa na shambulizi kubwa la pumu (severe asthmatic attack) anaweza kushindwa kuzungumza na pia, anakuwa na hali kama ya kuchanganyikiwa huku akitweta.

Vipimo na Uchunguzi

Pamoja na daktari kutaka kufahamu historia ya mgonjwa, anaweza pia kuamua kufanya vipimo ili kufahamu chanzo na madhara ya ugonjwa wa pumu kwa muathirika.

Matibabu ya Pumu

Kwa ujumla matibabu ya pumu hujumuisha kuepuka visababishi au vyanzo vya mzio na matumizi ya dawa kwa walio na hali mbaya.

Kwa wagojwa wanaougua kwa sababu ya msongo wa mawazo hupewa ushauri nasaha kwa ajili ya kusaidia kutatua matatizo yanayowakabili.

Inashauriwa pia wenye tatizo hili kuwa na dawa karibu muda wote kwa ajili ya matumizi pindi shambulizi litakapotokea.

Pia, mgonjwa anashauriwa kuyaepuka mazingira ya baridi yanayoweza kuchochea kupata shambulio zaidi la ugonjwa huo.

aidia kutanua mirija ya hewa (bronchodilators).

Dawa za kuondoa mcharuko mwili kama vile cortisone ya drip (hasa wakati wa dharura) au nebulizer, na dawa za kuzuia mzio (antihistamine drugs).

Hata hivyo, kuna matibabu ya ziada kulingana na hali ya mgonjwa pamoja na kundi na aina ya pumu inayomuathiri mgonjwa.

Kwa wagonjwa wenye pumu ya ghafla na wenye hali mbaya (acute asthma) matibabu hujumuisha matumizi ya dawa za kutanua mirija ya hewa (bronchodilators) pamoja na kuongezewa hewa ya oksijeni. Vilevile dawa za kutuliza mcharuko mwili (steroids) pamoja na dawa za kutuliza kukakamaa kwa misuli ya mwili (intravenous muscle relaxants). Aidha kwa vile mara nyingi shambulizi hili laweza kuwa la hatari sana, mgonjwa hulazwa hospitali na huongezewa hewa ya oksijeni, na kwa wagonjwa wasioweza kupumua kabisa, husaidiwa kufanya hivyo kwa kutumia mashine maalum iitwayo (mechanical ventilator).

Kwa wagonjwa wenye pumu sugu, jambo la muhimu ni kuepuka visababishi vya pumu na kuendelea na matumizi ya dawa zinazosaidia katika kutanua mirija ya hewa.

Kwa wagonjwa wanaopata mashambulzi ya mara kwa mara wanaweza kushauriwa na daktari kutumia dawa kadhaa zikiwemo zile zinazopunguza mcharuko mwili (mast cell inhibitors, inhaled steroids au oral steroids).

pamoja na dawa za kutuliza kukakamaa kwa misuli ya mwili (muscle relaxants). Aidha ni vema pia kutibiwa na kuthibiti kutokea kwa magonjwa yote yahusuyo mfumo wa hewa.

Matumizi ya chanjo ya magonjwa kama influenza na pneumococcal pneumonia nayo husaidia sana katika uthibiti wa kutokea kwa pumu. Ni vema pia kuepuka matumizi ya dawa za jamii ya beta-blockers kwa wagonjwa wenye shinikizo la damu na ambao pia wana pumu.