DAWA LISHE: Fahamu asili ya komamanga na matumizi yake

Muktasari:

Mbali na hilo, komamanga pia lina vitamin  C, B5, A, E  pamoja na madini ya potassium na chuma 

Komamanga   ni tunda lenye asili ya India na  kisayansi linaitwa Punica Granatum, lakini lililetwa Marekani na wawekezaji wa Kihispania na kwa sasa limejulikana dunia nzima.

Wataalamu wanasema, Komamanga  ni zaidi ya tunda kwa sababu limejaa vitamini, madini na virutubisho vingi  vinavyoweza kuufanya mwili kuwa na afya na nguvu.

Mbali na hilo, komamanga pia lina vitamin  C, B5, A, E  pamoja na madini ya potassium na chuma na unapotumia  juisi ya tunda hilo, husaidia kuponya saratani, na husaidia mtiririko wa damu kwenda vizuri katika mishipa ya damu, hivyo kupunguza hatari ya magonjwa ya moyo, shinikizo la damu na kiharusi.

Ulaji wa mara kwa mara wa tunda  hili huzuia meno kuoza na kuhuisha mfumo wa kinga mwilini kwa kuondoa vijidudu, bakteria, maambukizi ya virusi ndani ya mwili, kutibu maradhi ya tumbo ikiwamo kutopata choo.

Husaidia kuondoa  sumu mwilini,  hupambana na tatizo la uzito, husaidia kuua virusi vya aina mbalimbali, lakini kizuri zaidi, komamanga pia ni mahiri  katika kutibu magonjwa ya  kusendeka (magonjwa ya muda  mrefu), kama saratani ya tezi  dume, saratani  mbalimbali, kisukari, baridi yabisi na uvimbe  katika maungo (gout).

Uchunguzi  uliochapishwa katika jarida la Utafiti la Kuzuia Kansa, umeonyesha kwamba kemikali ziitwazo ellegitannins zinazopatikana kwa wingi kwenye komamanga, zinaweza kuzuia kimeng’enyo (enzyme) aina ya aromatase, hali  ambayo huzuia kukua kwa homoni ya estrogen inayopatikana katika kansa ya matiti.

Kiongozi aliyeongoza  katika uchunguzi huo, Shiuan Chen  amesema kemikali hizo hupunguza uzalishwaji wa estrogen na kusaidia kuzuia seli  za kansa ya matiti kuzaliana mwilini pamoja na tezi la ugonjwa huo kukua.

Aromatase ni kimeng’enyo ambacho hugeuza homoni ya androgen  kuwa estrogen na kushambuliwa kimeng’enyo hicho ndio lengo kuu la dawa za kupambana na kansa za matiti zinazosababishwa na homoni ya etrogen.

(Hadija Jumanne)