Dalili hizi zinaweza kuashiria una tatizo la kiafya

Muktasari:

  •  Lakini ni vyema kuwa makini na uchovu na maumivu ya mwili yanayodumu kwa muda mrefu mwilini. Watu wengi wanatabia ya kupuuzia baadhi ya dalili zinazojitokeza kwenye afya zao bila kujua chanzo cha dalili hizo. 

        Kutokana na shughuli za kila siku na sababu zitokanazo na hali ya hewa, ni kawaida mtu kujikuta akipatwa na uchovu na maumivu ya aidha baadhi ya viungo au mwili mzima. Lakini hali hiyo mara nyingi huwa ni ya muda mfupi tu na baadaye hutoweka. Lakini ni vyema kuwa makini na uchovu na maumivu ya mwili yanayodumu kwa muda mrefu mwilini. Watu wengi wanatabia ya kupuuzia baadhi ya dalili zinazojitokeza kwenye afya zao bila kujua chanzo cha dalili hizo. Naoma ifahamike kuwa tabia hii ni hatari sana kwa sababu matatizo yote yote makubwa ya kiafya huwa yanaanza na dalili ndogo ndogo ambazo wengi wamekuwa wakizidharau. Leo kupitia safu hii nitaeleza baadhi ya dalili mbalimbali zinazojitokeza kwenye afya zetu japo zinaonekana ni ndogo lakini hupaswi kuzifumbia macho kwa sababu zinaashiria tatizo fulani kwenye mwenendo wa afya kwa ujumla.

Dalili ya kwanza ni udhaifu wa kwenye miguu na mikono kunakoambatana na ganzi.

Ikiwa sehemu za mikono na miguu zinadhohofika, zinakosa nguvu na kupata ganzi na hasa zikitokea hadi usoni, inaweza kuwa ni dalili ya kiharusi na hasa kama hali hii inatokea upande mmoja tu wa mwili.

Sambamba na dalili hizo, kiharusi pia huambatana na dalili ya kuishiwa nguvu unapotembea unapata kizungunzungu, na kushindwa kutembea vizuri.

Nikukumbushe tu msomaji kiharusi ni ugonjwa unaosababishwa na matatizo ya usambazwaji wa damu kwenye ubongo kutokana na kuziba au kupasuka kwa mirija inayosambaza damu kwenye ubongo na kusababisha chembechembe za damu kufa.

Kiharusi ni moja ya maradhi yanayoongoza kusababisha vifo vya ghafla kwa miaka ya hivi karibuni.

Hivyo pata msaada wa kitabibu haraka ikitokea unapatwa na dalili hizo pamoja na zingine kama kutoona vizuri, maumivu makali ya kichwa, kuhisi kuchanganyikiwa au kupata shida unapozungumza. Dalili nyingine ni maumivu ya kifua. Maumivu yoyote ya kifua na hasa yanayoambatana na joto kali na kutokwa na jasho, upumuaji wa shida, na hata kichefuchefu yanapaswa kutafutiwa ufumbuzi wa kitabibu haraka.

Maumivu ya kifua yadumuyo kwa muda mrefu yanaweza kuwa ishara ya maradhi ya moyo au shambulio la moyo na hasa yakitokea wakati wa kufanya mazoezi au hata shughuli yoyote inayofanya mwili utumike.

Lakini pia maumivu ya mara kwa mara ya kifua yanaweza kuashiria tatizo lingine tofauti na moyo, kama kuganda kwa damu kwenye mapafu au mzunguko wa damu kutokuwa sawa kwenye mapafu.

Ukibaini dalili hizo nenda kamuone haraka kwa ushauri wa kitabibu kama hali hiyo inajirudia mara kwa mara.

Lakini dalili nyingine ni mkojo unaoambatana na damu. Yapo matatizo mengi ambayo yamezoeleka yanayoweza kusababisha kutoa mkojo uliochanganyika na damu, kama maambukizi ya kwenye njia ya mkojo na ya baadhi ya maradhi ya zinaa kama yatakuwa yamedumu kwa muda mrefu bila tiba. Kama unatoa mkojo uliochanganyika na damu ikiambatana na maumivu ya mgongo au ya chini ya kitovu ni ishara unashambuliwa na baadhi ya maradhi ya figo na hasa uwapo wa mawe madogo kwenye figo ambayo kitaalamu yanaitwa kidney stones.

Tatizo hili hutokea wakati mawe hayo yanajitengeneza na kujikusanya kwenye figo baada ya mkojo kuchujwa. Yale mabaki ya mkojo hutengeneza mawe hayo yatokanayo na ile chumvi chumvi. Hulazimika kutoka kupitia njia ile inayotumika na mkojo kutoka kwenye figo ndani hadi kwenye njia ya mkojo ya nje iliyoambatana na via vya uzazi. Hivyo kupitia mchakato huu, wakati mwingine huchubua njia ya mkojo na kusababisha majeraha madogo kwenye njia ya mkojo. Ni vyema kumuona daktari ili kuangalia uwapo wa aina hii ya mawe kwenye figo.

Lakini tatizo lingine kubwa, mkojo uliochnganyika na damu mara nyingi huashiria saratani ya kibofu na hasa ikitokea hauambatani na maumivu yoyote hivyo ni vyema kuwahi kupata vipimo ili kuliwahi tatizo hili katika hatua zake za awali.