Hasira huchangia kupungua kwa kinga ya mwili ya binadamu

Muktasari:

NUKUU

“Vyakula vyenye manufaa kwa binadamu ni mboga za majani na matunda yenye rangi tofauti kwa sababu zile rangi ni virutubisho tosha, lakini hata maji ya kunywa ni chakula japo kuwa watu wengi hawajui kama maji ni chakula.
Maji ni chakula kwa sababu ili virutubisho vyote viweze kuingia kwenye mwili wa binadamu, lazima kuwe na maji ya kutosha.
Maji ya kunywa ambayo ni safi na salama ndiyo kitu cha kwanza katika kukabiliana na chembechembe hai zinazokuwa kwenye mpangilio.”

Kinga  ya mwili huongezeka au kupungua kila siku kutegemeana na mtu amekula nini, amekunywa nini au hali ya ubongo wake ikoje kwa sababu kama mtu atakuwa na hasira siku nzima, anakuwa na uwezekano mkubwa wa kupungua kinga yake ya mwili.

Watalaamu wa masuala ya lishe wanasema hakuna dawa au chakula cha kula siku moja cha kuponya tatizo la kushuka kwa kinga ya mwili, badala yake jamii inatakiwa kula mlo wenye mpangilio unaokubalika.

Wanabainisha kuwa njia nzuri ya kukabiliana na tatizo hilo ni kula matunda, mboga za majani, vyakula vya nafaka na maji ya kunywa ya kutosha.

Mkurugenzi wa Idara ya Kinga kutoka Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (ORCI), Dk Crispin Kahesa anasema kila chakula kina umuhimu na mchango wake katika kujenga na kuupa mwili nguvu.

Anasema  baadhi ya vyakula vinasaidia kupunguza kemikali zinazosababisha saratani.

“Saratani ni ukuaji wa chembechembe hai zinazokuwa bila mpangilio, hata hivyo mwili wetu  unaanza kujengwa na chembechembe hai moja na baadaye zinaunganika na kuwa nyingi na hatimaye kuwa chembechembe hai zinazotengeneza tishu zenye baadhi ya  viungo (organs),” anasema Dk Kahesa.

Anavitaja baadhi ya vyakula  vyenye uwezo wa kupambana na saratani  kuwa ni vyote vyenye vitamini na vina mchango mkubwa katika kuzuia saratani.

Anasema kuna baadhi ya vyakula vinajenga kinga ya mwili na kuna vingine vinachochea saratani kutokea kutokana na mazingira.

Wakati Dk Kahesa akisema hayo, Muuguzi kutoka Shirika la Watawa la Mabinti wa Maria Immakulata (DMI),  Farida Mathola anavitaja baadhi ya vyakula na matunda yanayopambana na kuzuia saratani kuwa ni maboga, karoti, viazi vitamu, pilipili nyekundu na zile za njano.

Vingine ni  Bilinganya, Binzari, Broccoli, Nyanya, majani ya ngano huku kitunguu saumu kikionyesha  uwezo wa kuondoa hatari ya kupatwa na saratani ya tumbo, koo na matiti kwa mtu anayetumia mara kwa mara.

Farida anasema  mboga za majani zenye rangi ya kijani zinauwezo mkubwa wa kupambana na Saratani huku Spinachi ikiwa inaongoza kwa sababu ina uwezo mkubwa wa kutoa kinga mwilini au kuondoa hatari ya kupatwa na saratani ya ini, kizazi, utumbo mpana na kibofu cha mkojo.

“Kutokana na hali hiyo, jamii inaweza kuziweka mboga hizi katika orodha ya vyakula vya kila siku, hasa ukizingatia umuhimu wake wa kupambana dhidi ya magonjwa ya kansa na kuwapo kwa kiwango kingi cha Vitamin E, ambayo nayo ni muhimu kwa kinga ya mwili,” anasema Farida.

Anafafanua kwa upande wa matunda , Stafeli, Barungi , Tufani, machungwa na Nanasi ni miongoni mwa yanayotajwa kuwa na uwezo mkubwa wa kupambana na saratani huku nanasi likiwa na kimeng’enyo cha aina ya ‘bromelain’, ambacho ni muhimu  kwa kinga dhidi ya saratani ya matiti na mapafu na pia, lina vitamin C inayoongeza kinga mwilini.

Pia, Tufani (Apple) lina kirutubisho muhimu kiitwacho ‘quercetin’ kilichoonyesha kuwa na uwezo mkubwa wa kupunguza hatari ya mtu kupatwa na saratani ya mapafu na ina . Pia, uwezo wa kupunguza kasi ya kukua kwa seli za kansa ya kibofu. Muuguzi huyo anaelezea  kwa ufupi baadhi ya faida zilizopo kwenye vyakula na matunda yanayozuia Saratani kwa binadamu.

Kuwa moja ni pamoja na majani ya ngano, sharubati (juisi) ya majani ya ngano nayo husaidia kuimarisha protini kwenye seli nyekundu za damu na kuimarisha kinga ya mwili na mfumo wa kusaga chakula na kuondoa lehemu.

Pia, majani hayo huimarisha mfumo wa sukari mwilini na kutibu wenye matatizo ya kisukari. Huimarisha na kutibu matatizo ya ini, figo na kuondoa sumu mwilini.

Barungi lina wingi wa asidi ya citric, potassium na calcium na mtu anapokula tunda hilo usiku wakati wa kwenda kulala humfanya apate usingizi mzuri.

Lakini unywaji wa juisi ya tunda hilo asubuhi kabla ya kula chakula kingine, huondoa tatizo la kukosa haja kubwa na kuongeza hamu ya kula pamoja na kusaidia uyeyushaji wa chakula mwilini, lakini pia hupunguza homa itokanayo na mafua makali.

Barungi hutibu pia magonjwa ya kiharusi, hupunguza rehemu, unene, kukarabati mishipa ya damu na kuipa damu uwezo wa kutembea mwilini.

Binzari au manjano (Turmeric)

Licha ya watu wengi kutumia binzari kama kiungo, lakini kina faida nyingi mwilini ikiwamo ya kuzuia hatari ya kupata saratani.

Ulaji wa binzari mara kwa  mara huimarisha afya ya macho, viungo vya mwili na utendaji kazi wa ini. Lakini pia huimarisha chembe hai za mwili na mfumo wa uzalishaji mbegu za uzazi.

Tikitimaji chungu

Kwa mujibu wa uchunguzi uliochapishwa kwenye Jarida  la Utafiti wa Kansa, majimaji yanayotolewa katika tikitimaji chungu yanayojulikana kama ‘karela’ kwa kihindi, hupunguza kasi ya kukua kwa seli za sarataniya matiti.

 Utafiti huo ulioongozwa na mtafiti  Ratna Ray, unaeleza  tikitimaji chungu lina uwezo wa kuzuia saratani ya matiti, lakini bado haijathibitika kama majani yake yanauwezo wa kutibu ugonjwa huo.

Kitunguu Saumu

Licha ya kutibu magonjwa zaidi ya 30, kitunguu swaumu kimetajwa kwenye vitabu mbalimbali vya dini kikielezewa kuwa na faida katika kutibu maradhi mbalimbali yasababishwayo na bakteria, matatizo kwenye mapafu, mfumo wa umeng’enyaji chakula na matatizo ya kuishiwa nguvu.

Ulaji wa mara kwa mara wa kiungo hicho huondoa sumu mwilini, husafisha tumbo, huyeyusha mafuta mwilini, husafisha njia ya mkojo na hutibu UTI na kuondoa amoeba, minyoo na bakteri wengine.

Lakini pia kiungo hicho kina uwezo wa kuongeza nguvu za kiume na hutibu matatizo ya kukosa nguvu za kiume.

Brokoli (Broccoli)

Miongoni mwa faida iliyopo katika mboga hiyo ni kuzuia mwili kupatwa na saratani. Kwa sababu ina glucoraphanin ambayo hubadilishwa mwilini na kuwa sulforaphane inayozuia saratani.

Pia, broccoli husaidia mfumo mzima wa neva na ubongo kufanya kazi inavyotakiwa, huipatia misuli nguvu, lakini pia  huimarisha msukumo wa damu na hupunguza sumu mwilini kwa kusafisha uchafu

Bilinganya

Ni aina ya mboga inayopatikana katika kundi la mbogamboga, lakini pia inaweza kutengenezwa juisi ambayo husaidia kutoa taka mwili kwa njia ya haja ndogo.

Virutubisho vilivyopo katika mboga hiyo husaidia kupunguza hatari ya ugonjwa wa moyo na kiharusi na ngozi ya bilinganya inaambatana na miseto iitwayo terpenes inayosaidia kupunguza lehemu mwilini.

Stafeli

Asilimia 12 ya tunda hilo lina sukari ya asili na ni salama kwa mlaji na ni chanzo kikuu cha vitamini C, madini ya chuma na Niacin  Riboflavin huku likiwa na kirutubisho aina ya Annona Muricata chenye uwezo wa  kukabiliana na maradhi ya saratani. Tunda hilo huzuia matatizo ya mfumo wa fahamu, shinikizo la damu, msongo wa mawazo, hudhibiti ukuaji wa bakteria, virusi, vijidudu nyemelezi, hutibu majipu na uvimbe, huongeza stamina ya mwili na kurahisisha kupona haraka, hufukuza chawa na kuzuia magonjwa yasaratani.

Utafiti  uliowahi kufanyika, unaonyesha juisi ya stafeli hutibu saratani kwa haraka kwa sababu inanguvu mara 10,000 zaidi ya tiba ya mionzi katika kuzia seli za saratani.

Nyanya:

Moja kati ya faida ya nyanya katika mwili wa binadamu ni kulinda uharibifu wa DNA kutokana na wingi wa antioxidants, vitamin  C na A ambazo kwa pamoja hufanya kazi ya kulinda DNA isishambuliwe, lakini nyanya hiyo husaidia kukinga mwili dhidi ya ugonjwa wa kisukari.

Nyanya huzuia saratani ya tumbo, mapafu, koo na saratani ya kizazi, lakini ulaji wa nyanya kwa wingi huzuia saratani  ya tezi dume na hupunguza kiwango cha sukari mwenye damu, husaidia kusafisha ngozi, husaidia macho kuona vizuri hasa nyakati za usiku. 

Nini kifanyike

Luitfrid Nnally ni mtaalamu wa Masuala ya Lishe kutoka Taasisi ya Chakula na Lishe Nchini ( TFNC), anasema ili kukabiliana na tatizo la saratani, ni lazima kuwapo na maandalizi bora ya chakula kabla ya kupikwa ili virutubisho vilivyopo visiweze kupotea.

Dk Kahesa ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya Saratani anasisitiza ili jamii iweze kukabiliana na saratani na magonja menginie, inatakiwa kula vyakula hai na halisi badala ya vilivyosindikwa. “Kuna baadhi ya watu wanaondoa virutubisho bila kujua, mfano unatenegeza juisi ya embe halafu unaongeza radha, unakuwa umeweka kemikali na unaua baadhi ya virutubisho hai vilivvyokuwapo kwenye tunda lako,” anasema Dk Kahesa.

Idadi ya wagonjwa wa saratani wanaogunduliwa nchini

Mtaalamu wa Kliniki ya Saratani  kutoka ORCI, Khamza Maunda anasema wagonjwa 50,000 hugundulika kuwa na saratani kila mwaka huku taasisi hiyo ikiwa na uwezo wa kuhudumia wagonjwa 5,000 sawa na asilimia 10 ya idadi ya kitaifa.

Mkurugenzi wa Idara ya Magonjwa yasiyo ya kuambukiza nchini, Profesa Ayoub Magimba anasema katika miongo miwili iliyopita, magonjwa yasiyo ya kuambukiza ikiwamo saratani yamekuwa kwa kasi na kutishia  afya za Watanzania.

Profesa Magimba anasema juhudi za haraka zinapaswa kuchukuliwa  na Serikali ili kukabiliana na  hali hiyo kwa sababu  watu wengi wapo hatarini kupata magonjwa hayo kwa kukosa uelewa wa namna ya kukabiliana na magonjwa  hayo.