Kati ya watoto 1500 wanaozaliwa mmoja ana tatizo la kijinsia

Muktasari:

DONDOO

  • Tatizo la mtu kuwa na jinsi mbili au zisizo za kawaida kwa lugha ya kitabibu hujulikana kwa jina la intersex.
  • Kitabibu maana yake nikuzaliwa na upungufu kwenye maeneo ya viungo vya uzazi na mfumo mzima sehemu za ndani, yaani kwenye kokwa ya kike au yakiume na sehemu za nje yaani kwenye uke, uume na sehemu zingine za siri.

Unapokutana na pasi ya kusafiria ya raia kutoka nchi kama Australia kwa asiyefahamu anaweza kustaajabu kwani zimeachwa sehemu tatu za kujaza jinsi ya msafiri. Na hii ipo wazi, kwasababu mtu anatakiwa ajaze kama yeye jinsi yake ni kike,  kiume au ya kike na kiume.

Hilo siyo jambo la kushangaza, kwani sehemu ya kujaza jinsi kama mtu anazo zote ya kike na kiume iliongezwa baada ya nchi hiyo kubaini matatizo ya kiafya yanayoweza kumpata binadamu.

Kama tulivyoshuhudia mpambano wa kupatikana katiba mpya ambayo ndiyo itakua ikiongoza maisha ya Watanzania, vivyo hivyo hata mwili wa mwanadamu huwa na katiba yake na inapovurugwa au kubadilishwa kiholela, huwa na matokeo mabaya.

Katiba ya mwili wa binadamu imo ndani ya vinasaba, kitabibu ni Genes.

Chembe hizo ndizo hubeba taarifa za kiurithi za binadamu zenye maelekezo ya shughuli zote pamoja na maumbile yake yatakavyokuwa.

Wataalamu wanasema kuvurugika kwa taarifa hizo, husababisha matatizo ya kimwili ambayo binadamu anapozaliwa hujikuta akiwa na maumbile tofauti na ilivyo kawaida kama mtu kuzaliwa akiwa na jinsi mbili.

Inaelezwa kuwa uwapo wa jinsi mbili mwilini na huku zikikaribiana kiutendaji kwa muathirika, ni mojaya matokeo ya kuvurugika kwa chembe za urithi.

Unawezaje kumtambua mtu mwenye jinsi mbili

Machoni unaweza ukamtambua mtu kwa mwonekano wa kiume, lakini akawa mwilini mwake ana chembe za urithi za kiume. Vivyo kwa kwa upande wa mwanamke.

Katika jamii matatizo kama hayo hupokelewa tofauti kutokana na watu kutokuwa na uelewa wa tatizo.

Hali hiyo huwafanya waathirika kutokuwa wawazi na uhofia hata kwenda katika vituo vya afya kwa ajili ya kupata ushauri nasaha wa kitabia au hata kupata matibabu mengine.

Taarifa za jumla za tatizo hilo

Tatizo la mtu kuwa na jinsi mbili au zisizo za kawaida kwa lugha ya kitabibu hujulikana kwa jina la intersex.

Kitabibu maana yake nikuzaliwa na upungufu kwenye maeneo ya viungo vya uzazi na mfumo mzima sehemu za ndani, yaani kwenye kokwa ya kike au yakiume na sehemu za nje yaani kwenye uke, uume na sehemu zingine za siri.

Takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaonyesha kwa kila watoto 1,500 hadi 2,000 wanaozaliwa, mmoja huwa na tatizo hilo lakimaumbile ambalo huonekana kwa macho.

Moja ya changamoto kubwa ambayo waaathirika hawa hukumbana nayo ni uhusiano wa kimapenzi, kijamii na binafsi.

Watu hawa hukumbana na hali ya kuwa na aibu na wengine hutengwa na kunyanyapaliwa.

Jambo kama hili huwafanya waathirike kisaikologia na kujitenga na jamii.

Nini kinatokea mwilini na kusababisha tatizo hili?

Kwa kawaida, mwanadamu huwa na mgawanyiko wa chembe hai za urithi nusu toka kwa mzazi wa kike na nusu kutoka kwa mzazi wakiume, pale yai la kike na kiume yakikutana hupatikana mtoto aliye na chembe za urithi toka kwa wazazi wake.

Taarifa hizi hubebwa na chembe zilizo kama utepe na umbile kama la herefu X na huwa na kifundo katikati.

Chembe hizi kitabibu huitwa chromosome ndizo zinabeba taarifa za urithi kwa kila kitu mwilini kuanzia urefu wa mtoto anayezaliwa hadi rangi ya macho anayotakiwa kuwa nayo.

Chembe hizi huwa na protini maalum na molekyuli moja ya DNA (vinasaba) ambavyo vimo ndani ya seli ambayo hubeba taarifa nyeti.

Hiyo sasa ndiyo huwa kama katiba yenye maelekezo yote yanayotakiwa kufanywa na mwili.

Kuanzia wanadamu, wanyama na mimea, chembe za urithi za chromosomes zipo katika mtindo wa jozi.

Zipo jozi 22 ambazo huitwa autosom na nyingine ni jozi ya ziada ambayo inahusika na mustakabali wa jinsi ya mwanadamu itakavyokuwa, ambayo kitabibu huitwa sex chromosome.

Hii ndiyo inafanya jumla yake kuwa  jozi 23 au kwa maana nyingine, ni seli huwa na chromosomes 46 jumla.

Sex chromosomes ndizo  zinazohusika kutoa mustakabali wa jinsi ya mtu katika maumbile ya nje na ya ndani, chembe za aina hii huwa na chembe ya chromosome X na Y.

Inapotokea muunganiko wa jozi ya XX huyo ni mwanamke na jozi XY ni mwanamume, sehemu ya nje ya jinsi huwa na sehemu za siri za nje na sehemu za ndani huwa ni korodani na kokwa ya kike kitaalam ovary.

Sehemu za ndani ndiyo tezi zinazozalisha vichochezi vya kike kwa mwanamke na kwa mwanaume ni mbegu za kiume na kichochezi cha kiume.

Vichochezi hivi ndivyo hutoa tabia za kijinsia za kike na kiume na humsababisha mtu aonekane mke au mme.

Mbegu ya kiume na yai lakike baada ya mizunguko ya seli huwa na malighafi za urithi nusu ambazo ndiyo chromosomes, yaani hujigawa kutoka chembe 46 nakuwa nusu yake ambayo ni 23.

Mimba inapotungishwa ndipo nusu ya chembe za chromosome 23 huunganika na kutengenezwa kiumbe ambacho huwa na chembe 23 toka kwa baba na 23 toka kwa mama.

Lakini panapotekea upungufu kwenye chembe za urithi kitaalamu huitwa gene mutation.

Katika chembe hizo za urithi ndipo mabadiliko ya kimaumbile yanapotokea ya nje na ya ndani.

Wapo watu wenye muonekana wa mwanamke, ambao huwa na korodani na uume, lakini na wana chromosomes XY ndani ya mwili ambayo humthibitsha kuwa ni jinsi ya kiume.

kazi ya korodani kutengeneza homoni itwayo testosterone.

Homoni hii ndiyo inakazi ya kumfanya mtu awe na tabia za kiume pamoja na maumbile yake.

Homoni hii huwa na kazi yakumfanya mwanaume kipindi anabalehe kuwa na sauti nzito, misuli mikakamavu na mikubwa, utawanyikaji wa nywele kama vile ndevu.

Lakini miili ya wanawake huwa inashindwa kuipokea homoni hiyo ili iweze kufanya kazi yake, tatizo hilo kitabibu huitwa Androgen Insensitivity syndrome.

Watu wenye tatizo hilo hungeliweza kuwajua kwakuwa wanapozaliwa huwa na sehemu zakike katika seheme zao za siri.

Na hata wazazi na wahudumu wa afya hupewa taarifa kuwa umejifungua mtoto wa kike na cheti cha kuzaliwa pia hujazwa mtoto wa jinsi yake ni ya kike.

Lakini kadiri mtoto huyo anavyozidi kukua, dalili za uwapo wa jinsi mbili huonekana.

Miaka ya nyuma wataalamu wa upasuaji walikua wakifanya marekebisho na kuangalia jinsi ipi iko imara walikuwa wakiiacha na kuiondoa ile dhaifu.

Lakini kumbe ilikua ni makosa kwani wale waliopasuliwa walipofikia umri wa utu uzima, walijikuta wameondolewa jinsi ya kiume, lakini ana muonekano wa kike ukubwani.

Na walipopimwa walikutwa na chembe zao za urithi ni XY yaani mwanaume. Mwingine katiba ya mwili wake ni ya kike, yaani ana chembe XX, hivyo anakuwa na maumbile ya kiume na jinsi yake ni yakiume.

Ushahidi wa kiuchunguzi wa kutumia uchambuzi wa kina wa chembe hai ndiyo unatoa uthibitisho kuwa mwanadamu huyo ni mwenye katiba ya chembe za urithi za kike au za kiume.

Kwa wenzetu walioendelea wamekuwa na watu wenye tatizo hili, hivyo wakaamua kuwajali kwakuwapa uhuru wakuamua baada ya kupatiwa ushauri.

Taarifa iliyotolewa Juni 14 na Shirika la Habari la CNN, ilisema kuna ushuhuda wa baadhi ya waaathirika wa tatizo hilo walioanzisha umoja wao na walitoa ushahidi wa wazi kuwa unapomtazama usoni, hufanana kwa kila kitu na mwanaume. Shuhuda mmoja alisema alianzisha uhusiano na mwanaumke, lakini ilikua ikimnyima raha kwakuwa alikua na muonekana wa kiume ila ana jinsi ya kike.

Vivyo hivyo kwa mwanadada……ambaye alikua na uhusiano ambao haulufikia katika mapenzi.

Anasema kila alipofikiria jambo hilo, ilimuwia ugumu kwa sababu ya maumbile yake.

Uanishwaji wa tatizo la muingiliano wa jinsi

Kuna aina 4 za muingiliano wa jinsi yaani 46xy, 46xx, muingiliano jinsi wenye kokwa moja au zote mbili na muingiliano jinsi wakutatanisha.

Sehemu ya pili ya makala haya itaeleza aina hizo zilivyo na kama tatizo hili linatatulika.