Kutoa mimba kadhaa hakuondoi uwezo wako kuzaa

Muktasari:

Swali likuwa hivi (jina nimehifadhi) : Hivi mtu aliyewahi kutoa mimba mara mbili na mpaka dakika hii bado hajapata ujauzito, je hapo baadaye akipata ujauzito ataweza kuzaa vizuri bila kupata shida yoyote? Na je atawahi au atachelewa kuzaa?

Karibuni wasomaji wa kona hii ya piramidi ya afya, leo nimeona nitumie nafasi hii kujibu moja ya swali ambalo linafanana na mengine yanayoulizwa.

Swali likuwa hivi (jina nimehifadhi) : Hivi mtu aliyewahi kutoa mimba mara mbili na mpaka dakika hii bado hajapata ujauzito, je hapo baadaye akipata ujauzito ataweza kuzaa vizuri bila kupata shida yoyote? Na je atawahi au atachelewa kuzaa?

Ni swali ambalo nimekuwa nikiulizwa mara kwa mara hasa na wanawake wengi ambao waliwahi kutoa mimba kwa makusudi au kwa sababu za kitabibu kama vile kuumwa au mimba kuharibika yenyewe.

Nitajibu swali kutokana na alivyouliza msomaji, kwakuwa umetumia neno kutoa mimba ina maana ilitolewa kwa kudhamiria yaani kinyume na sheria ambayo kwa lugha ya kitabibu tunaita illigeal abortion.

Kutoa mimba kinyume na sheria ni uondoaji wa kiumbe kilichotungwa kabla ya muda wa kuzaliwa haujafika pasipo sababu ya kitabibu.

Katika swali lako hukuweka umri wa mimba zilizotolewa wala muda gani uliokaa bila kushika ujauzito mwingine ila nitajibu. Ieleweke kuwa si lazima utolewaji wa mimba kuwa na muingiliano wa uwezo wa mwanamke kupata mimba, jambo la msingi ni utoaji uwe ni salama na usio na madhara yoyote.

Katika nchi ambazo kutoa mimba si uvunjaji wa sheria, wanawake wengi hutolewa mimba na kuwa salama bila kujitokeza kwa madhara yoyote na baadaye huweza kupata ujauzito mwingine wakiwa tayari kufanya kwa hilo.

Endapo mwanamke aliyetoa atajamiiana bila kinga yoyote anaweza kupata mimba nyingine ndani ya wiki mbili zitakazofuata baada ya yai lake la uzazi kupevuka.

Mtu anaweza kutoa mimba hata mara tano na akawa na uwezo wa kuzaa wakati wowote kama tu utoaji ulifanywa kwa kuzingatia utaratibu unaotakiwa na hakuna madhara yoyote yaliyojitokeza.

Madhara yanayoweza kujitokeza kwa kutoa mimba nipamoja na maambukizi ya via vya uzazi, majeraha ya mlango wa uzazi na ndani ya mfuko wa uzazi ndiyo yanayoweza kusababisha mtu kushindwa kupata ujauzito hapo baadaye au akipata inatoka.

Utoaji wa mimba kila mara bila ushauri wa daktari unaweza kusababisha majeraha katika mlango wa uzazi na kuufanya kuwa dhaifu na wakati wakubaeba mimba zinaweza kutoka.

Maambukizi ya nyumba ya uzazi yanaweza yakatokea wakati au baada ya mimba kutolewa hivyo kutokea kwa maambukizi kwenye via vya uzazi ikiwamo mirija kuharibika.

Kuwahi au kuchelewa kuzaa hili litategemea kama hakuna madhara yoyote yalijitokeza na mizinguko ya hedhi kurudi kama kawaida.

Inashauriwa kitaalam, mwanamke aliyetoa mimba au mimba yake kuharibika na kusafishwa apumzike kwa kipindi kati ya miezi 6 mpaka 12 au mwaka mzima kabla ya kushika ujauzito mwingine.

Kufanya hivi ni kuupa mwili nafasi ya kujijenga upya na homoni kurudi katika utaratibu wake wa awali. Kumbuka, mimba inapotungwa kunatokea mabadiliko mengi mwilini ili kuandaa mazingira ya ukuaji wa mimba iliyotungwa.

Ni muhimu kuepukana na mimba zisizotarajiwa hasa kwa wasichana wanaosoma hii ni kutokana kutokana na changamoto zinazoweza kujitokeza ikiwamo kuachishwa masomo au kwenda zahanati za uchochoroni kutoa mimba hiyo.

Ikumbukwe kuwa mtaani watu hufanya pasipo kuwa na ujuzi wala kuzingatia usafi wa vifaa jambo ambalo linaongeza hatari ya kupata maambukizi ya maradhi mengine. Kwa watu wazima ni muhimu kutumia njia salama za kupanga uzazi.