Madhara wayapatayo wanaotoa mimba

Muktasari:

  • Aliuliza mtu aliyewahi kutoa mimba mara mbili je! akiupata ataweza kujifungua salama?

Karibuni wasomaji wa kona hii ya piramidi ya afya, leo nimeona nitumie nafasi hii kujibu swali nililoulizwa hivi karibuni na msomaji.

Aliuliza mtu aliyewahi kutoa mimba mara mbili je! akiupata ataweza kujifungua salama?

Swali hili limekuwa likiulizwa kwa mara hasa na wanawake waliowahi kutoa mimba kwa makusudi au kwa sababu za kitabibu.

Nitajibu swali kutokana na alivyouliza msomaji, kwakuwa ametumia neno kutoa mimba, ina maana mimba hiyo ilitolewa kwa kudhamiria kinyume na sheria amabyo kwa lugha ya kitaalam tunaita Illigeal abortion.

Kutoa mimba kinyume na sheria maana yake ni uondoaji wa mimba iliyotungwa kabla ya kutimia muda wake wa kujifungua bila sababu ya kitabibu.

Hata hivyo, muuliza swali hakuweka umri wa mimba hizo zilizotolewa wala ni kwa muda gani amekaa bila kupata ujauzito.

Ila ieleweke si lazima utolewaji wa mimba uwe na muingiliano wa uwezo wa mwanamke kupata mimba. Jambo la msingi ni utoaji uwe salama usio na madhara yoyote.

Katika nchi ambazo kutoa mimba si uvunjaji wa sheria, inaonyesha wanawake wengi wanaotolewa hubaki salama bila kudurika na hata baadaye anaweza kubeba mimba tena.

Hii inamaanisha mwanamke aliyetoka kutoa mimba,akijamiiana bila kutumia kinga, anaweza kupata mimba ndani ya wiki mbili zitakazofuata ili mradi tu kiyai cha kiwe kimepevuka.

Mtu anaweza kutoa mimba hata mara tano lakini bado akawa na uwezo wa kubeba tena na akazaa iwapo tu utoaji huo utakuwa ulifanywa kwa kuzingatia utaratibu na haukuleta madhara yoyote.

Hata hivyo, wataalamu wanasema madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na kutoa mimba ni pamoja na maambukizi ya via vya uzazi, majeraha ya mlango wa uzazi na ndani ya mfuko wa uzazi ndiyo yanayoweza kusababisha mtu kushindwa kupata ujauzito baadaye au akapata lakini ikatoka.

Ila ikumbukwe, utoaji wa mimba bila utaalamu mara kwa mara unaweza kusababisha majeraha kwenye mlango wa uzazi na kuufanya uwe dhaifu na kila mimba ikitungwa inakuwa na uwezekano mkubwa wa kutoka.

Maambukizi ya nyumba ya uzazi yanaweza yakatokea wakati au baada ya mimba kutolewa, hivyo uambukizi huo ukasababisha via vya uzazi ikiwamo mirija kuharibika.

Kuhusu kuwahi au kuchelewa kuzaa

Suala hili litategemea pia kama hakuna madhara yaliyojitokeza na mzunguko wa hedhi wa muhusika kurudi katika hali yake ya kawaida.

Inashauriwa kitaalamu, mwanamke aliyetoa mimba au mimba kuharibika na akasafishwa, apumzike kwa miezi Sita hadi 12, ndipo abebe ujauzito mwingine.

Kwa kufanya hivyo, kutamsaidia kuupa mwili nafasi ya kujijenga upya na homoni kurudi katika utaratibu wake wa awali.

Ikumbukwe mimba inapotungwa hutokea mabadiliko mengi ya mwili yanayolenga kuandaa mazingira ya ukuaji wake.

Ni muhimu kuepuka mimba zisizo tarajiwa hasa kwa wasichana walio shuleni, kwani kunakuwa na madhara mengi ya kimwili na kimaisha. Kwani wengi hujikuta wakifukuzwa shule na wengine hudhurika kiafya kwa sababu ya kuzitoa kwa njia isiyosalama.

Ikumbukwe kuwa mtaani watu hufanya pasipo kuwa na ujuzi wala kuzingatia usafi wa vifaa, hivyo hatari ya kupata maambukizi ya maradhi mbalimbali ni kubwa. Kwa watu wazima ni muhimu kutumia njia salama za kupanga uzazi.