Jini mkata kamba :Sababu tano kwa nini ndoa, uhusiano wa watu maarufu haudumu

Muktasari:

  • Watu maarufu ‘wanapambana’ na uhusiano wao kama wengine. Kwanza wao kuanzisha penzi na kubaki ndani ni ngumu zaidi. Siyo kwa sababu maisha yao yanamulikwa na kamera wakati wote, ni kwa sababu maisha yao yanaweza kuwafanya waishi tofauti ndani ya uhusiano.

Mara ngapi umeumia uliposikia wapendanao unaowakubali wametengana. Kuanzia Angelina Jolie na Brad Pitt, Heidi Klum na Seal, Vanessa Mdee na Jux, Lady Jady na Gadner G Habash. Inatokea mara kwa mara.

Watu maarufu ‘wanapambana’ na uhusiano wao kama wengine. Kwanza wao kuanzisha penzi na kubaki ndani ni ngumu zaidi. Siyo kwa sababu maisha yao yanamulikwa na kamera wakati wote, ni kwa sababu maisha yao yanaweza kuwafanya waishi tofauti ndani ya uhusiano. Mwanamuziki wa Marekani John Mayer anasema umaarufu unachangia uhusiano kutodumu. Mtaalamu wa Saikolojia nchini Uingereza, Donna Rockwell anasema umaarufu huwa unawasahaulisha. Wanazoea kuona kila mtu anawatazama wao, wanawake kwa wanaume wakijigonga kuwa karibu nao kiasi cha kusahau kuwa wanawajibu wa kutoa pia hasa wanapokuwa katika uhusiano.

Anasema ubongo hujenga mazoea ya kutaka kusikia kelele za watu wakimshangilia na huwa vigumu kuifunga sehemu hiyo. Msanii anapoasikia kelele za mashabiki au kufuatwa na mashabiki ubongo hutoa homoni ambazo humfanya ajisike akiwa ‘juu ya dunia’ lakini hajisikii hivyo akiwa na mpenzi wake.

“Mwanamuziki au mcheza filamu huyu anapoondoka ukumbini anaagwa na kundi la watu kila mmoja akijaribu kumshika mkono na wengine wakimwinda kupata japo usiku mmoja wa faragha naye, anarudi nyumbani na kukutana na mpenzi wake akimuuliza maswali magumu kutokana na ujumbe uliokutwa kwenye simu yake, ana ghadhibika haraka. Angetamani kunyenyekewa na si kuulizwa kwa ukali,”

Kupenda vichwa vya habari

Donna anasema iwapo itatokea mmoja katika uhusiano anapenda kuanika habari zake magazeti ya udaku huchangia uhusiano kufa kwa sababu hufukua mambo mapya kila siku ambayo yanaweza kumchosha mwenzi wake.

Anasema kuna uhusiano mkubwa wa uhusiano kuvunjika na mambo yanayoandikwa katika majarida ya udaku. Mfano hai ni uhusiano wa Kim Kardashian na Kris Humphries ambao ndoa yao ilidumu kwa siku 72 tu. Kwa Tanzania unaweza kuufananisha na uhusiano wa Wema Sepetu na Diamond Platnumz.

Kupishana sana umri

Ingawa anasisitiza kuwa umri siyo kigezo kikubwa lakini una nafasi katika kuufanya uhusiano udumu au ufe haraka.

Kuwa na ratiba tofauti

Mwanasaikolojia wa Marekani, Julia Flood anasema wasanii wengi wana ratiba ngumu ambazo huwaweka mbali na wapenzi wao na hii huchochea kutokuwa waaminifu. Anasema ubaya wake huchochewa na mazingira kwani watu hawa hufanya kazi na watu wengine wanaovutia kwa kila namna kwa hiyo anapokuwa mbali na mpenzi wake ni rahisi kushawishika.

Mahali walipokutana

Julia anasema mahali penzi linapoanzishwa panaweza kutoa jibu iwapo litadumu au la.

Anasema penzi linaloanzishwa kwa kukutana sehemu ya kurekodi filamu au video ya muziki na sehemu yoyote ya kazi huwa halidumu.

“Penzi la hivi huwa limeanzishwa kwa kuvutiwa na mwonekano wa nje, kadri wanavyokaa huanza kuujua mwonekano wa ndani na hivyo kupoteza hamu iwapo tabia haziendani,” anasema Julia.

Wivu, wivu wivu...

Kwa kawaida watu maarufu huzungukwa au kufanya kazi na watu wa jinsia tofauti.

Inawezekana mwenza akawa na wivu kwa kuunganisha matukio ambayo yanaweza kuwafanya wawe katika ugomvi mara kwa mara.\

Uhusiano ulitikiswa na jini mkata kamba

Kwa kipindi cha miezi miwili mastaa wa filamu na muziki nchini wameingia katika mtikisiko baada ya uhusiano wao kudaiwa kuingiliwa na ‘jini mkata kamba’. Alianza Diamond na Zari baada ya kudaiwa kuwa amezaa na mwanamitindo Hamisa Mobetto. Ingawa baada ya kukiri watu waliamini hiyo ingekuwa dawa ya kurudisha mapenzi kwa mzazi mwenzake anayeishi nchini Afrika Kusini.Inavyoonekana kidonda cha usaliti moyoni mwa Zari kimekuwa kigumu kupona na jini mkata kamba amesimama kidete.

Hata hivyo inaonekana penzi hilo litaendelea kudumu hasa baada ya Zari kudai kuwa hajamwacha na hana mpango wa kuanchana na baba watoto wake wawili, Latiffah na Nillan.

Wolper na Brown

Moja kati ya couple nchini zilizoonekana zinaendelea kuwa Power Couple ni pamoja na ile kati ya mwigizaji Jackline Wolper na mpenzi wake aliyemtambulisha kwa jina moja la Brown. Hata hivyo wapenzi hao waliokuwa wakipendezana kwa mwonekano inasemekana wamepitiwa na jini mkata kamba.

Shamsa na Chid

Penzi la mwigizaji Shamsa Ford na mumewe Chid Mapenzi linadaiwa kunyemelewa na jinni mkata kamba kutokana na mwenendo wa maandiko ambayo amekuwa akibandika katika ukurasa wake wa Instagram. Mapema wiki hii aliandika: “Jamani sitokuja kumuacha mume wangu kwa ajili ya mwanamke hata siku moja labda afanye makubwa yasiyoeleweka kwenye jamii. ‘Amecheat’ Bili clinton sembuse Rashid wangu?” alihoji mwigizaji huyo maarufu aliyecheza filamu ya Chausiku.

Aunty Ezekiel na Mose Iyobo

Mwigizaji Aunty Ezekiel mwanzoni mwa wiki aliandika waraka mzito katika ukurasa wake wa Instagram akimkemea jini mkata kamba anayelinyemelea penzi lake kwa Mose Iyobo.

Alindika:… kwa uhandsom gani aliona huyu saa hizi mkajifanya kutwa kumtongoza kama sio tu ilimradi ‘umeshare’ na fulani sasa mimi sio mzungu ndugu yangu ntakukanyaga hutaamini kaulize yule …. wa china akupe habari yangu.”