Maadili yamechangia muziki wa sasa kuwa na ‘utamu wa banzoka’

Mara nyingi nimeulizwa ni kwanini nyimbo nyingi za zamani bado zinadumu, wakati za siku hizi zinakuwa na umaarufu wa muda na kupotea? Nimeshaulizwa swali hili na wapenzi wa muziki, watangazaji wa vipindi vya muziki, waandishi na hata wanamuziki vijana wa kizazi hiki wamekuwa wananiuliza swali hili tena na tena.

Labda leo nitoe tena mawazo yangu juu ya swali hilo. Kuna mambo mengi ambayo ni tofauti katika jamii ya watunzi wa sasa na wa zamani, hapa nitaongelea hali ya watunzi wakati nikiwa katika bendi mbalimbali kati ya mwaka 1975 mpaka 1990.

Tofauti ya kwanza kubwa ilikuwa ni malezi ya awali ya watunzi. Kuna msemo maarufu unaosema ‘msanii ni kioo cha jamii’. Hivyo basi ukitaka kujua jamii ikoje angalia kazi za wasanii. Tungo za miaka hiyo zinaonyesha kuwa jamii ilikuwa na staha katika mambo mengi. Jamii ilikuwa bado ya watu waliokuwa watoto au wajukuu wa wazee waliokuwa wanazingatia malezi ya kiasili yaliyosisitiza kujiheshimu na kuheshimu watu wengine.

Hivyo tungo zilikuwa ni zile zilizokuwa zikijikita bado katika misingi hiyo. Jambo jingine muhimu, kulikuwa na taratibu rasmi na zisizo rasmi za kurekebisha wale waliopotoka na kukiuka misingi hii.

Kama nilivyosema nitaongelea miaka niliyokuwa katika muziki na kwa kuwa nilipata bahati ya kuwa katika bendi ambazo nyimbo zake bado zinapendwa na hata kupigwa na bendi za sasa miaka karibu arobaini na zaidi toka tulipotunga nyimbo hizo.

Jambo la kwanza ni tofauti kubwa ya sababu za kuamua kutunga, ni kawaida kabisa kusikia msanii siku hizi akisema anataka kutunga ili’ atoke’ au anatunga kwa kuwa ‘muziki ni biashara’. Katika utunzi wa namna hii kunakuwepo la lengo linaloongoza aina ya utunzi. Hivyo mtunzi anaweza kutunga wimbo wa mapenzi lakini nia yake si kuonyesha hisia ya mapenzi bali kutengeneza wimbo ili uuze au apate umaarufu. Msanii anaweza kutunga wimbo wa msiba lakini hisia yake haikuwa msiba bali ni kutafuta kutoka au kutimiza amri ya kutunga wimbo wa msiba.

Hisia za ukweli ni muhimu katika tungo. Watunzi niliokuwa nikiishi na kufanya nao kazi wakati huo walikuwa wakitunga wimbo kutokana na mwongozo wa hisia zao tu. Tungo zilitokana na tukio la kweli au la kubuni lakini kilichowaongoza kutunga hakikuwa faida au umaarufu bali kutoa hisia zao kuhusu kile walichokuwa wakikielezea. Msanii ambaye anatengeneza kazi yake kwa huambukiza kwa kila anayesikia au kuangalia kazi ile.

Wimbo ambao mtunzi kaimba kusikitika humsikitisha kila anayeusikiliza na ule anaouimba kufurahi humfurahisha kila anayeusikia.

Kwa kuwa muziki wakati huo ulikuwa ni mkusanyiko wa watu wengi kila tungo ilipitia katika chujio kubwa. Mtunzi ukifikisha tungo yako kwenye kundi lako, bendi, taarab au kwaya, watu wa kwanza kuanza kuukosoa au kukusifu walikuwa wenzio katika kundi, kisha hawa hukusaidia kuuboresha na kila mtu kushiriki katika kuufanikisha, mpiga solo alitunga mapigo yako yake, mpiga bezi, wapulizaji na kadhalika, na kila mmoja alikuwa ana uwezo wa kutoa ushauri kuhusu sehemu yoyote ya wimbo. Hatimaye kama kundi hufikia mahali na kuridhika kuwa kazi yao sasa inaweza kutolewa kwa umma. Katika bendi zote nilizopitia, siku ya kuupiga wimbo kwa mara ya kwanza ilikuwa muhimu, kwani wanamuziki wote kwa ujumla mlikuwa na kazi mbili, kwanza kupiga kwa ufasaha tungo yenu mpya na pili kuangalia washabiki wenu wanauchukuliaje wimbo wenu mpya. Kama wimbo haukupokelewa vizuri na mashabiki wenu, ulikuwa unarudi tena jikoni, kuliwekwa hata vikao vya kujiuliza kwa nini watu hawakuuchangamkia wimbo. Na kama ingeonekana kuwa umefurahiwa na wapenzi wenu, basi ungeendelea kupigwa kwenye kumbi hata mwezi mmoja zaidi kwa kile tulichokiita ‘wimbo uive’.

Baada ya hatua hii ndipo mipango ya kurekodi wimbo huanza kufanyika na kwa miaka hiyo kulikuwa na chujio jingine, tungo zilipelekwa mapema Radio Tanzania ambako ndiko kulikuwa na studio za kurekodi, na huko kulikuwapo na kamati iliyokuwa ikiangalia kama tungo zimefuata maadili yaliyokuwepo wakati huo.

Tungo zilizopita chujio hilo ndizo zilizorekodiwa. Na hakika ndizo nyimbo ambazo zingine zina miaka zaidi ya hamsini lakini zinafurahiwa na wapenzi wa muziki wa rika zote hadi leo.

Kwa utaratibu wa sasa, ni kawaida msanii kutunga wimbo wake chumbani kwake peke yake, kisha akaingia studio, wakawa watu wawili yeye na mtayarishaji wake na kutengeneza wimbo ambao ukitoka hapo unapelekwa redioni tayari kwa kurushwa kwa umma.