Beatrice: Mrembo aliyeamua kushika jembe kukuza kipato

Muktasari:

Kisa chake ni ishara kuwa unaweza kuwa mwajiriwa, lakini ukaendesha miradi ya kilimo kwa ufanisi

Tofauti na vijana wengi wa rika lake, huwezi kuamini kwa ajira aliyonayo kama Batrice Haule angekuwa na hamu ya kujishughulisha na kilimo.

Umuonapo kazini au barabarani, mwonekano wake ni kama ule wa wanawake wengi wanaoijipenda ambao muda mwingi wanafikiria kuonekana warembo.

Lakini msichana huyu ana sifa ya ziada, siku za mwisho wa wiki au likizo, badala ya kupumzika nyumbani, yeye anatumia nafasi hiyo kusimamia miradi kadhaa ya kilimo anayoiendesha mkoani Ruvuma.

Beatrice mwenye umri wa miaka 28 anaishi Njombe na anafanya kazi katika shirika moja la kimataifa kama ofisa takwimu.

Pamoja na kuwa na ajira ambayo kwa baadhi ya watu ingetosha kumtuliza kimaisha, yeye anaamini katika dhana ya kuwekeza. Kwake maisha kama anavyosema; ‘’…ni kuwekeza, ni kupambana.’’

Ili kutekeleza dhana ya maisha ni kuwekeza akaamua kuwekeza mtaji wa akili na fedha zake kwenye sekta ya kilimo anayosema inalipa kuliko hata ajira rasmi. Anaamini kilimo ni zaidi ya ajira, kwani faida anazozipapata kutoka shambani ni kubwa mno

‘’Kwa zama hizi kama mtu anataka kufanikiwa katika maisha yake ni kilimo pekee. Kilimo ni fursa nzuri ambayo kijana anaweza kuifanya na kumpa mafanikio. ‘’ anasema na kuongeza:

‘’Kama upo kwenye ajira, hakikisha hiyo ajira yako iwe mbegu na anza kwa kuwekeza kwenye miradi ya uzalishaji. Mshahara haununui gari, mshahara haujengi nyumba, mshahara hausomeshi watoto shule nzuri, ila mshahara unaweza kuwa chanzo cha kufanya hayo yote.’’

Tangu mwaka 2015, Beatrice amekuwa akijishughulisha na kilimo cha mazao mbalimbali, na sasa anaendesha miradi yake mitatu ya kilimo na usambazaji wa maziwa aina ya mtindi.

Hii ni kwa sababu alibaini kuwa ajira pekee haitoshi kuendesha maisha yake.

Shauku ya kilimo

Zao la ufuta ndilo liloanza kumpa shauku ya kulima kama anavyosema:

“’Kwa mara ya kwanza nilianza kulima ufuta Chalinze mkoani Pwani, baada ya kuona mafanikio katika zao hilo nikaona kumbe fursa ipo kwenye kilimo,”, anasema.

Kwa kuwa kilimo kwake ni biashara, hakuridhika na zao moja la ufuta baada ya hapo aliongeza miradi mingine miwili ya mazao ya soya na tangawizi mkoani Songea.

INAENDELEA UK 28

INATOKA UK 25

“Mwaka jana nilipata taarifa kuwa kijiji cha Mkongo kuna ardhi nzuri kwa ajili ya kilimo cha soya, sikutaka kupoteza muda nilikwenda kuona hali halisi baada ya kujiridhisha nikaanza na heka 20,”anasema.

Anasema mbali na ardhi nzuri kwa ajili ya kilimo hicho alifanya utafiti kujua soko la soya na wateja wake. Baada ya hapo alilima akiwa na uhakika wa soko kwa asilimia 100.

“Kosa tunalolifanya sisi wakulima ni kulima bila kujua soko likoje; mazao haya ni ya biashara hivyo kabla ya kulima cha kwanza kujua ni soko na ndivyo nilivyofanya mimi” anaeleza.

Anasema sababu ya kulima zao zaidi ya moja na katika maeneo tofauti, ni kufanya kilimo kama sehemu ya biashara hivyo anaangalia mazao yenye faida na ambayo hata soko lake halisumbui.

Kwa zao kama soya ambalo hutumiwa na watu kama lishe na hata chakula cha kuku, wake soko kubwa anakouzia ni katika kampuni ya kutengeneza chakula cha mifugo ya Silverland Intrenation iliyopo iringa.

Mkulima hachoki

Kama ilivyo kawaida, mtafutaji hachoki, Beatrice aliamua tena kuongeza mradi mwingine kwa kulima zao la tangawizi hukohuko mkoani Songea katika kijiji cha cha Mkongotema kwa kulima heka moja pekee.

“Hili zao nilijaribu tu, kuna ndugu yangu mmoja alinieleza katika kijiji hicho tangawizi inakubali sana nikasema ngoja nikajaribu, kwa kweli sikutarajia mana zao limekubali hadi nikajuta kulima heka moja,” anaeleza.

Anavyomudu kilimo na ajira

Pamoja na kuwa mwajiriwa, lakini ajira yake haimzuii kufanya shughuli zake za kilimo, kwa kuwa hupangilia ratiba zake vizuri ili kilimo kisiathiri majukumu mengine ya kazi.

“Huwa naingia kazini asubuhi hadi saa nane mchana, hivyo kwa siku za wiki sipati muda mzuri wa kutembelea miradi yangu hivyo natumia vyema siku za mapumziko kwenda shambani, ‘’ anasema na kuongeza:

“Pia wakati wa likizo ndio muda mzuri kwangu kishirikiana na vijana wangu walioko shambani.’’

Changamoto

Kwa sasa mapenzi yake yameelemea kwenye kilimo, lakini kwa kuwa bado ni mwajiriwa, anajikuta katika mtanziko mkubwa wa kusimama miradi yake kiasi cha kufikiria kuacha kazi.

Kwa kuwa miradi yake ipo katika maeneo tofauti, anasema wakati mwingine anashindwa kuitembelea yote, kitu ambacho ni kosa kwa mkulima makini kama yeye.

“Raha ya miradi yako uwe nayo karibu, lakini inapokuwa mbali sina Amani, hivyo natamani siku moja nihamie katika mashamba yangu” anasema.

Ajivunia kilimo

Kwake kilimo sio tu kwa ajili ya kuvuna mazao mengi na kujipatia kipato. Anasema kupitia kilimo amejifunza mengi.

“Sasa hivi nimekuwa kama bwanashamba, kwani najua aina mbalimbali za dawa za kilimo,’’ anaeleza.

Anasema kipato anachokipata kupitia kilimo, asingeweza kukipata kama angetegemea ajira pekee. Kilimo hicho kwa sasa kimemwezesha kusomesha wadogo zake

“Asikwambie mtu hakuna njia nyingine ya mafanikio kama kilimo, yaani najivunia kutunza familia yangu kupitia kulimo lakini pia hata mahitaji yangu nayamudu sio kama zamani” anasema.

Kufahamiana na watu ni moja ya mafanikia kwa Beatrice, anasema kupitia kilimo amefahamiana na watu mbalimbali ambao hakutarajia kuonana nao ambao wamechangia mafanikio yake hasa kwa kutoa ushauri juu ya kilimo.

“Nimejenga jina kupitia kilimo hivi sasa ukiuliza Beatrice watakuambia yule mkulima, kwa hiyo jina limekua kupitia kilimo na sio cheo changu kazini” anaongeza.

Ndoto zake

Ukiondoa shauku ya kutaka kuwa mkulima mkubwa Afrika na duniani kwa jumla, Beatrice ana ndoto ya kuwasukuma wanawake kuingia kwenye kilimo.

“Nataka wanawake sasa waone kuwa kushika jembe sio ushamba, tusitegemee tu ajira ambazo hata kipato chake ni mara tatu zaidi ya kile kinachopatikana shambani”.

Aidha, anatamani kuwa mjasiriamali mkubwa kwani mbali na kilimo ana mradi wake wa kuuza maziwa mahala anapoishi.

“Katika hili nawaambia Wanawake wenzangu tusimame imara kwani tunaweza na tusikate tamaa mapema, tusichague kazi, hivi sasa kutegemea ajira pekee utachelewa kimaendeleo,’’ anasema.