Dar es Salaam sasa ni Darinstagram

Muktasari:

Dunia ya Tanzania ya sasa. Kila kitu kiko Instagram. Ndo sehemu pekee inayohifadhi wapumbavu. Malaya. Matapeli na kila aina ya binadamu wenye ushetani ndani yake.

        Huku kwetu Uswahilini kila ukigonga mlango wa chumba cha mabinti. Utasikia subiri kwanza. Sijui huwa wanafanya nini wakiwa peke yako? Any way tuishie tu ‘kuimejini’ kila mtu kwa hisia zako.

Dunia ya Tanzania ya sasa. Kila kitu kiko Instagram. Ndo sehemu pekee inayohifadhi wapumbavu. Malaya. Matapeli na kila aina ya binadamu wenye ushetani ndani yake.

Ukiondoka Instagran huku mitaani nako kuna mambo yake. Tazama hili. Na hii ni kwa wadada. Ambao wamekuwa sehemu ya mtafaruku wa mishipa ya shingo na nyuso za wanaume huko mitaani.

Hii tabia inakera na inafurahisha kwa watu wenye mapepo ya ngono zembe. Kuvaa hayo madera yenu mitaani. Na kisha kuyashikilia na kuyanyanyua juu mpaka ngozi nyeupe inaonekana.

Mnawapa tabu na wakati mgumu sana baba na kaka zenu mitaani.Yaani ukimkuta mwanamke wa Temeke amevaa dera. Anachofanya ndo kile kile anachofanya wa Ilala. Kinondoni. Rufiji na kama siyo Kakola Geita huko.

Halafu kuna ile staili ya kulibana kwenye nguo ya ndani. Ni nini hasa mnatafuta? Hii tabia ipo kwenye maeneo ya wazi kama sokoni. Kwenye vituo vya mabasi. Madukani na mitaani. Unakuta mwanamama na msambwanda wake kavaa dera na kulibana ndani kwa ndani kwenye nguo ya ndani.

Hata kama mwanaume haoni anaishia kuhisi tu na kujikuta anapata mihemko. Wadada wenyewe wanatazama tu. Hawajui au makusudi kwamba hawaoni kama kikwazo kwa kaka na baba za jamani? Mkoje lakini na madera yenu hayo?

Hii tabu yote mnayopata kwa nini msiyakate ili yasiwape tabu namna hiyo. Kama kweli mnayabana na kuyashikilia kwa sababu ya kuburuza chini? Bora anayenyanyua kwa mbele basi. Kuliko yule anayechomekea ndani ya nguo ya ndani aisee. Mshindwe na mlegee. Sijui mkoje.

Lakini hiyo ndo raha yake kwa wakware na wapuuzi wa tabia za kipuuzi. Utasikia “Raha ya dera shurti linyanyuliwe kidogo mbele. Tukate ili liwe gauni? Hiyo ndo raha ya dera... likitosha sio dera tena kanzu hiyo.”

Hayo ndo majibu yao hawa wanaizaya waliokosa haya huku mitaani aiseee. Ningekuwa rais wa nchi hii ningeruhusu dera kuwa vazi rasmi la ofisini. Aidha kudumisha mila desturi na utaifa.

Pia kulinda wapuuzi wanaozurula tu mitaani badala ya kutulia maofisini. Maana uvaaji wa madera kwa dada na mama zetu siku hizi ni sehemu ya kivutio cha utalii wa ndani kwa kweli.

Tuachane na hayo. Tuangalie tatizo lingine ambalo ndo kubwa zaidi.

Mastaa wetu hasa wa kike wamekuwa na kautaratibu flani hivi, ambako neno sahihi kukatamka ni kautaratibu kakipuuzi, kipumbavu, hovyo kabisa.

Wakiwa kwenye uhusiano au kwenye ndoa kabisa, wana kawaida ya ‘shoo ofu’ mitandaoni. Kana kwamba wao ndo wa kwanza kuolewa au kumiliki mpenzi.

Watapamba kila picha nzuri mbele ya macho yao na mashabiki wao. Watawashirikisha mashabiki wao mpaka mambo ya faragha. Kifupi mitandaoni hasa Instagram watataka kutawala wao.

Hii imekuwa ikiwatesa wengi wao pindi wanapoachana. Na kwa vile wengi wao ni magubegube wakomavu. La sivyo vifo vya kujitakia kukwepa aibu vingepatikana sana.

Kwa sababu mwanzo wa penzi lao walishirikiana na mashabiki wao. Basi mashabiki watataka kushirikishwa mpaka mwisho wao.

Kuna wale ambao wanaishia vibaya kwa kuibiana mabwana. Yaani staa huyu anamchukua bwana wa staa yule. Mitandaoni inakuwa ni matusi yasiyoelezeka.

Team ya huyu inamtukana nyakunyaku na team ya nyakunyaku inamkingia kifua kwa kujibu mapigo ya mitusi.

Katika hili mfano ulio hai ni wa Hamisa na Zari. Kwa sababu ya maisha yao kuyaanika sana mitandaoni yamezalisha haya yaliyotokea na kuendelea.

Tukio la hawa wawili limetengeneza matusi mapya. Yaani kuna watu wanatukana tusi ambalo halijawahi kutamkwa popote Duniani. Kisa Hamisa na Zari kuchukuliana bwana.

Ingawa wenyewe wamekuwa wakichukulia poa kwa sababu ya matukio haya kuwasaidia kwa namna moja ama nyingine lakini ni mbaya sana.

Lazima mastaa wetu wajipime na maisha ya mitandaoni. Haya wanayoyafanya na mashabiki wao yamepita kwenye ustaarabu siyo tu wa Kiafrika bali wa kibinaadamu dunia nzima.

Mambo ya ajabu kabisa. Na kupitia hawa Mastaa wetu wawili ndipo utagundua kuwa Mange anachofanya kutukana watu mitandaoni ni asili yake.

Kumbe huku Bongo kuna kina Mange wengi kuliko idadi ya kura alizopata Lowassa 2015. Kifupi kila mtu anajua kutukana. Na kila mtu anajua kulipiza tusi kwa tusi. Inasikitisha sana.

Lakini yote haya ni sababu ya mizuka ya maisha ya mitandaoni. Zari anapenda maisha ya ‘shoo ofu’ na Hamisa naye anapenda hiyo kitu.

Na zaidi bwana wao ndo anapenda zaidi pamoja na familia yake yote mpaka majirani.Sasa nani wa kumshikia paka kengere? Hakuna.

Wanaishia kuacha dunia iende kama inavyokwenda. Hayo ndo madhara ya kuacha wazi mambo mitandaoni.

Achana na hao. Kama ulifuatilia siku chache zilizopita kabla ya mume wa Irene Uwoya Hamad Ndikumana hajafariki. Walikuwa wakilumbana kwa vijembe vingi mitandaoni. Ndikumana anasema hili Irene anajibu hili. Kila shabiki akajua kinachoendelea.

Hakuna wanandoa wasiogombana. Lakini kwa nini ugomvi wa wanandoa wenye mtoto mkubwa kabisa wafanyie mitandaoni? Kwa faida ya nani? Ili iweje?

Matokeo yake maneno ya mwisho katika ugomvi wao ambayo yalikuwa makali sana. Bado yapo mitandaoni.

Na mtoto atakuja kuyaona muda siyo mrefu hata Magufuli akiwa hajamaliza muhula wake wa kwanza. Mtoto anaachwa kwenye hali gani? Maneno ya baba yake ya mwisho kabla ya kufariki yatamuacha kwenye hali gani mtoto?

Wao walilumbana na kuapiana viapo kana kwamba hawana damu inayowaunganisha nyuma yao.

Mastaa wetu tukio la Uwoya kufiwa na mumewe huku wakiwa katikati ya malumbano makali mitandaoni. Liwe funzo kwenu. Akiba ya maneno kitu cha msingi.

Maneno ya Ndikumana yanaelea tu mitandaoni yakimsubiri mtoto aje kuyaona. Ajue kile alichokuwa nacho babaake moyoni juu ya mama yake. Inasikitisha sana.

Wekeni akiba ya maneno acheni kujitoa ufahamu mitandaoni. Imekuwa kama wendawazimu sasa kila staa kugeuza kurasa za Instagram kama guest house yake. Hotel yake. Chumba chake na bafu lake.