Fuata kanuni hizi ufanikiwe katika mradi wako wa kilimo-1

Muktasari:

  • Watu hupanda mimea na kuitunza hadi mavuno hasa kwa uzalishaji wa chakula cha binadamu na lishe ya wanyama, lakini pia kwa shabaha ya kupata malighafi mbalimbali zinazotumiwa kwa kutengeneza nguo za watu.
  • Kilimo biashara kwa sasa kimekuwa kikifanywa na Watanzania wengi. Wengi wakiwa ni watu wenye kipato na waajiriwa katika maeneo mbalimbali. Wapo wanaojiandaa kuanza, wengine wameshaanza, wengine wakiwa na uzoefu wa hali ya juu. Lakini wapo pia wanaolima kwa mazoea na wengine wakitaka kukiacha kutokana na kushindwa kupata faida ya kilimo chao.

Kilimo ni uzalishaji wa mazao kwenye mashamba. Kilimo kina maana pana inayojumuisha mifumo ya uzalishaji mimea, ufugaji wa wanyama na uvuvi wa samaki. Mara nyingi kilimo cha mimea kinakwenda sambamba na ufugaji wa wanyama.

Watu hupanda mimea na kuitunza hadi mavuno hasa kwa uzalishaji wa chakula cha binadamu na lishe ya wanyama, lakini pia kwa shabaha ya kupata malighafi mbalimbali zinazotumiwa kwa kutengeneza nguo za watu.

Kilimo biashara kwa sasa kimekuwa kikifanywa na Watanzania wengi. Wengi wakiwa ni watu wenye kipato na waajiriwa katika maeneo mbalimbali. Wapo wanaojiandaa kuanza, wengine wameshaanza, wengine wakiwa na uzoefu wa hali ya juu. Lakini wapo pia wanaolima kwa mazoea na wengine wakitaka kukiacha kutokana na kushindwa kupata faida ya kilimo chao.

Makala ya leo yanaangazia kanuni kadhaa muhimu ambazo ni mwongozo kwa mkulima anayetaka kulima kwa mafanikio.

Fanya kilimo cha umwagiliaji

Kwa sasa kuna tatizo kubwa la ukame, yaani unapanda mazao yako lakini mwishowe yanakauka au yanakosa afya nzuri, hali inayosababisha mavuno kidogo. Kulima kwa kutegemea mvua ni mchezo wa kubahatisha, hivyo wakulima wanapaswa kuhakikisha wana maji, tena masafi yasiyokuwa na chumvi nyingi kwa sababu chumvi inapozidi huathiri ukuaji wa mimea.

Lakini pia mmea huhitaji maji kutokana na ukuaji wake. Unapopandwa unahitaji maji mengi, unapoanza kukua huhitaji maji pia, unapotoa matunda ambayo huelekea kukomaa maji hupunguzwa; hili nalo mkulima anapaswa kujua.

Kwa ufupi kujua kiwango cha umwagiliaji katika zao lako shambani itategemeana na aina ya udongo, aina ya zao, ukuaji wa zao na urefu wa mizizi na hali ya hewa ya eneo. Kwa haya washirikishe wataalamu kabla ya kukurupuka kama wengine.

Wengi humwagulia maji asubuhi na jioni kimazoea bila kujali aina ya udongo mwishowe maji yanazidi na kukumbana na magonjwa ya fangasi. Hivyo kuna haja ya kujifunza na kufahamu ratiba sahihi yaumwagiliaji.

Pima udongo wa shamba lako

Wakulima wengi huingia katika kilimo bila kupima udongo. Hali hii huleta madhara makubwa hasa katika kupunguza uzalishaji. Mmea unahitaji virutubisho 16 ili uweze kukua. Katika virutubisho hivyo kuna ambavyo huhitajika kiasi kikubwa ambavyo ni naitrojeni, fosiforasi na potasiamu. Kutokana na umuhimu wa virutubisho hivi mkulima anahitajika aweke mbolea mara kwa mara ili aweze kuvirudisha kwa kuwa hupotea kwa kuchukuliwa na mmea kila anapolima.

Kwa mfano, ili uweze kuota na kuwa na mizizi yenye nguvu na shina lenye nguvu, fosiforasi huhitajika. Hapa ndipo tunapomshauri mkulima aweke mbolea ya DAP. Mmea ukiwa unakua unahitaji naitrojen wa wingi ili jani lisiwe la njano na kusababisha mmea kushindwa kutengeneza chakula chake.

Mmea huhitaji pia potasiam na kalshamu hasa katika kuukinga mmea na magonjwa lakini pia kusaidia tunda kutengenezwa na kuliepusha na kuoza kitako. Hivyo huwa tunashauri kuweka mbolea ya NPK kipindi cha ukuaji. Pia unaweza kuweka mbolea za asili mara kwa mara.

Pima udongo wako na uache kubahatisha katika kilimo. Huwezi kujua uchachu wa udongo (ph) kama hujapima udongo. Ukipima udongo utajua aina ya mazao ya kulima, kiwango cha mbolea na ratiba ya umwagiliaji.

Panda kwa vipimo sahihi

Mkulima anapoambiwa ekari moja ya mahindi inaweza kuingia miche 55,000 haamini hata kidogo. Mkulima utakuta ana ekari 10, lakini kiuhalisia utakuta amelima kama ekari nne au tano.

Hii ni kutokana na sababu muhimu ya kutozingatia nafasi za upandaji. Kila zao hapa duniani lina nafasi yake maalumu ambayo shambani inapaswa kuzingatiwa kwa malengo maalumu.

Kupunguza nafasi hizo elekezi au kuzidisha kunasababisha madhara makubwa hasa katika uzalishaji wa mazao, kudhibiti magonjwa hatari na ugumu katika kuhudumia shamba. Kumbuka miche ikiwa michache, mazao hupungua wakati wa mavuno.

Simamia kwa karibu mradi wako

Kuna mkulima mmoja mkubwa na aliyefanikiwa katika kilimo. Yeye huzingatia usimamizi wake shambani. Aliwahi kusema: ‘‘Pale pesa yako ilipo nawe uwepo la sivyo utaibiwa au itapotea.’’

Anachokisema hapa ni kuwa kama mkulima makini lazima uwepo siku zote muhimu za mradi wako kama vile wakati wa upandaji, uwekaji dawa, uvunaji,uuzaji na nyinginezo.

Wengi hapa tumekwama kwa sababu tunafanya kilimo kwa njia ya simu. Tunajisahau kuwa kijana wa kazi hajui maumivu ya pesa ya bosi wake. Kwa mfano, usipokuwepo anaweza asimwagilie maji, au anaweza kupanda kwa utaratibu usiokubalika.

Tafuta soko kabla hujalima

Ili mkulima afaidike na kilimo anapaswa kukumbana na bei nzuri sana sokoni ambayo itamsaidia kurudisha gharama zake za kilimo. Ikiwa bei itakuwa chini anapaswa kuhifadhi mazao yake mpaka bei itakapopanda. Hata hivyo, changamoto wanayokumbana nayo wakulima wengi ni kuharibika kwa mazao yao kwa muda mfupi.

Unashauriwa kufanya utafiti wa soko na muda mwafaka wa kulima ili usikumbane na kadhia niliyotaja hapo juu.

Jifunze kutambua pembejeo bora

Kushindwa kuchagua mbegu bora tayari ni dalili ya hasara katika kilimo, kushindwa kutambua dawa nzuri ya wadudu au ya ukungu hilo nalo ni kosa litakalosababisha kupata hasara kubwa katika kilimo. Hapa wakulima mnahitajika kudadisi ili kupata ukweli. Unapoona wadudu mfano inzi weupe unapaswa kujua dawa gani sahihi kwa kumuua mdudu huyo. Kukosea kujua dawa kwanza utapata gharama ya kununua dawa ambayo sio sahihi..