Fursa za masoko kwa wakulima wa papai

Mkurugenzi wa  kampuni JOG Agri-consult and Solution ya jijini Dar es Salaam, Grace Mzoo akiwa katika shamba la mipapai. Na Mpigapicha wetu

Muktasari:

  • Achilia mbali virutubisho vingi vinavyopatikana katika mapapai katika kuboresha afya ya binadamu, wengi wanataka kuwa wakulima wa zao hili kwa sababu ni moja ya mazao yasiyochukua muda mrefu kuvuna.
  • Ni zao unaloweza kuvuna kuanzia miezi sita kwa uchache tangu kupandwa na hata sokoni bei yake inatia matumaini.

Kilimo cha matunda kimekuwa kikiwavutia Watanzania wengi. Mojawapo ya mazao yanayopendwa kwa sasa ni kilimo cha mipapai.

Achilia mbali virutubisho vingi vinavyopatikana katika mapapai katika kuboresha afya ya binadamu, wengi wanataka kuwa wakulima wa zao hili kwa sababu ni moja ya mazao yasiyochukua muda mrefu kuvuna.

Ni zao unaloweza kuvuna kuanzia miezi sita kwa uchache tangu kupandwa na hata sokoni bei yake inatia matumaini.

Hata hivyo, uzoefu unaonyesha wanaovutika na kilimo hiki wanakosa taarifa sahihi hasa kuhusu maarifa ya kilimo chenyewe, menejimenti ya kilimo na masoko.

Kwa sababu hii, baadhi ya wadau wa kilimo ambao ni wataalamu wa mazao ya mbogamboga na matunda, wamebuni mkakati wa kuwasaidia wakulima wa papai wakiamini zao hilo pekee linaweza kuwatoa wengi kutoka katika umasikini.

Wataalamu wa kampuni ya JOG Agri-consult and Solution ya jijini Dar es Salaam, wanasema kwa sasa wana masoko mkononi. Kinachohitajika ni wakulima kujitokeza kwa minajili ya kupewa maarifa na hatimaye kunufaika na kilimo cha mipapai.

Mwandishi wetu amefanya mahojiano na Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Grace Mzoo anayesema kilimo cha papai ni utajiri tosha ikiwa wakulima watakuwa tayari kufuata kanuni za kisayansi zinazoendesha kilimo cha kisasa.

Swali: Unawezaje kuwahakikishia Watanzania kuwa zao hili linalipa kwa maana ya kuwaingizia kipato kizuri?

Jibu: Nathibitisha kuwa kilimo cha papai ni utajiri mkubwa, kwani mahitaji yake kwa masoko ya ndani ni makubwa kwa matumizi ya kula na kusindika. Acha nionyeshe namna unavyoweza kupata fedha nyingi kupitia kilimo hiki.

Katika eneo la ekari moja ukizingatia vipimo sahihi unaweza kupanda miche 800 hadi 1000,ambayo ina uwezo wa kuzalisha matunda 100,000. Ukiamua kuuza kwa bei ya chini ya Sh 500, utakuwa na kiasi cha milioni 50 kwa mwaka mmoja. Kumbuka zao hili linakaa kwa muda wa miaka mitatu shambani.

Watanzania tujaribu kutafakari namna gani tunaweza kuuondoa umaskini kwa kuheshimu kilimo kama sehemu ya utajiri.

Tuache kupoteza muda kwa mambo yasiyokuwa ya msingi, bali tujikite kwenye kilimo maana kuna fedha nyingi kulinganisha na biashara nyingine hapa duniani.

Swali: Zao hili siyo geni, wakulima wamekuwa wakilima kwa muda mrefu, pengine wanakosea wapi kiasi cha kutofanya vizuri?

Jibu: Wakulima wengi hawafanyi kilimo biashara, wanalima kwa mazoea, kwa maana hawatumii mbinu bora za kisasa kuzalisha mipapai.

Mbinu hizi ni kama upimaji wa udongo, uandaaji mzuri wa shamba, matumizi ya mbegu bora, matumizi mazuri ya mbolea yanayozingatia aina ya mbolea na wakati mzuri wa kutumia. Pia, matumizi ya madawa ya kuua wadudu na kudhibiti magonjwa.

Swali: Kuna madai kuwa zao hili halina soko, hivyo wengi wanalikimbia?

Jibu: Ni kweli zao hili halipo kwa wingi sokoni kutokana na Watanzania kutoelewa umuhimu wake mwilini na virutubisho vinavyotokana na papai. Pia, kuna hofu ya wakulima kuogopa kuzalisha kwa kuogopa masoko.

Swali: Umesema mna mkakati wa kuwasaidia wakulima wa zao hili, ni upi huo?

Jibu: Tunatangaza kuwa masoko ya zao hili tunayo mikononi mwetu. Soko lililopatikana ni la nje na zinahitajika tani nyingi,hivyo kama kampuni tunawakaribisha watu wa kuanza nao.

Kwa Tanzania tunahitaji wakulima 300 ambao tutaanza nao awamu ya kwanza. Papai zinazohitajika ni zile ambazo tutakushauri kuzilima maana tumepewa masharti ya hizo aina za papai. Pia, kilimo tutakachokifanya ni kilimo hai kwa maana ya kuwa hatutatumia kemikali za viwandani.

Kwa kupitia mpango huu wa kilimo biashara, zipo fursa za mazao mengi ukitoa papai, ila tumeanza na papai kwa maana soko lake limeshapatikana,hivyo kadri tupatapo masoko tutakuwa tayari kuwapa fursa Watanzania wenzetu.

Swali: ukoje utaratibu ikiwa mkulima atahitaji kufanya kazi na nyinyi?

Jibu: Mkulima anapotaka kufanya kazi na sisi ni lazima akubali taratibu zetu zikiwamo kujisajili kwenye orodha, akubali kukaguliwa miradi yake na kusimamiwa na timu ya wataalamu wetu na akubali kusaini mkataba wetu wa masoko.

Mhariri: Wataalamu hawa wanapatikana kwa simu 0715500136 /0768279408.