Ishi kidigitali lakini mambo ya ndani yabaki katika ulimwengu wa analogia

Muktasari:

  • Ilikuwa ni fasheni kuwaona watu katika vyombo vya usafiri, majumba ya starehe na bustani wakiwa wameinamia vifaa vyao hivyo wakisoma vitabu. Mauzo ya vitabu mtandaoni yalikua kwa kasi kama moto nyikani.

Wakati digitali inaanza kushika kasi miaka ya 2005- 2006 hata usomaji vitabu ulibadilika kwani wengi walidownload katika mitandao. Ndio wakati matumizi ya tablets na kindle yaliposhika kasi .

Ilikuwa ni fasheni kuwaona watu katika vyombo vya usafiri, majumba ya starehe na bustani wakiwa wameinamia vifaa vyao hivyo wakisoma vitabu. Mauzo ya vitabu mtandaoni yalikua kwa kasi kama moto nyikani.

Miaka 10 baadaye mauzo ya vitabu mtandaoni yameshuka. Mauzo ya vitabu vilivyochapishwa yamekuwa yakiongezeka kwa asilimia saba tangu wakati huo. Utafiti uliofanywa mwaka jana umeonyesha asilimia 64 ya vijana wa kati ya miaka 16-35 wanapendelea kusoma vitabu vilivyochapishwa.

Kwa nini mfano huu wa vitabu katika mada hii? Ni kwa sababu utafiti uliwahusisha vijana ambao inaaminika digitali imewakumba na kuwazoa wazima wazima. Maana yake ni nini sasa? Kumbe analogia ina utamu wa aina yake ambao hauwezi kubatilishwa na digitali.

Basi hata katika maisha kuna mambo inabidi yanabaki katika analogia. Sasa hivi kila kitu kinaanzia kwenye mitandao ya kijamii na kwa sababu kuna deni kwa watazamaji inabidi kila kitu kianikwe huko ili kuuaminisha umma kuwa mambo yapo vizuri.

Ubaya katika hilo ni kwamba watu wanayafukua hata ambayo hayakustahili lakini wanafanya hivyo kwa kuwa mwenyewe umeamua kuishi hivyo. Kubaki analogia kuna saidia pia kuepusha maumivu na udhalilishaji.

Wema Sepetu miaka yote huwa anaitwa mgumba kwa kuwa hajazaa mpaka sasa lakini siyo Jokate Mwegelo, Flaviana Matata au Jackline Wolper ambao wamemzidi umri. Anasemwa hivi kwa kuwa mwenyewe ameamua kuipeleka ishu hiyo katika ulimwengu wa kidigitali.

Uzuri wa analogia unakufanya uwe na umiliki na siyo vya umma. Ni sawa na unapokuwa na kitabu chako katika kabati ni tofauti na kile kilichopo katika tablet. Mgeni akifika nyumbani kwako anakiona kikipendezesha nyumba na kumuonyesha kuwa ameingia katika nyumba ya msomi.

Siyo kwamba watu hawafanyi mambo mabaya katika maisha yao lakini wameamua maisha yao kuyaacha katika analogia na hiyo inawasaidia kuficha aibu zao. Kila mtu kuna wakati huteleza na ndio ubinadamu lakini ni chaguo binafsi kuyaacha analogia au digitali. Ni muhimu maisha binafsi yabaki katika analogia.