Jamii ilimuacha Lulu afike alipofika

Elizabeth Michael

Huwezi kuwa Lulu bila kuwa Elizabeth Michael. Ana akili sana yule mtoto. Ngumu sana kumuelewa kama hujakaa naye wala kufanya naye kazi.
Ni fundi kweli kweli wa kupuuzia wapuuzi. Ukileta dharau kwake kuna bohari kuu ya dharau.
Ukileta mbwembwe kana mbwembwe mpaka mbwembwe zenyewe zinakaogopa.
Kiumbe bora uzao wa Eva anacheza kwenye kuta ndefu za gereza muda huu. Dunia ya Tanzania inakosa moja ya pambo bora kabisa mitaani mpaka miaka miwili itimie.
Makosa ya wazazi? Makosa ya jamii? Makosa ya tasnia ya filamu? Au ni makosa ya Lulu kukosa hofu?
Huu siyo muda sahihi wa kuzungumzia chanzo kilichopelekea mtoto yule mwenye urembo usiotiliwa shaka kwenda jela.
Kitu pekee ni kwa wapenzi wake kumuombea kwa Mungu. Kwenda kumuona gerezani mara kwa mara.
Kutunza kile alichofanya kabla ya matatizo haya. Ili akitoka gerezani asianze upya maisha.
Kila mtu anasema anavyojua yeye. Kila mtu kawa mshauri juu ya maisha ya Lulu.
Wapo waliofurahia eti adhabu ya kifungo inapunguza maumivu ya Mama Kanumba. Hakuna jambo lolote linaloweza kuondoka maumivu ya kuondokewa na mtoto wako wa pekee.
Maumivu yataondoka pale utakapokufa na wewe mzazi. Jaji hakutoa hukumu kwa ajili ya kumfariji mama Kanumba. Adhabu imetolewa kulingana na mazingira ya kesi yenyewe.
Wapo wanaosema adhabu aliyopata itamnyoosha maana amezidi sana mashauzi. Ndipo mtu unagundua kuwa mitandaoni hasa Instagram watu wengi wana matope vichwani na siyo ubongo. Instagram ‘majitu’ yasiyojielewa ni mengi sana. Kuna makopo mengi sana yanayojiita binadamu.
Wapo wanaosema hasa kuwa ni makosa ya mama yake yaliyopelekea Lulu kuanza upuuzi angali mtoto.
Malezi ya mtoto wa kike kwa mzazi mmoja wa kike yana tabu sana. Na hatuwezi kujua kwa nini waliachana na mumewe.
Itoshe tu kusema kuna maisha hayazuiliki kwa familia yenye makuzi ya upande mmoja wa mzazi.
Lakini pia wale waliomtumia kingono kwani hawakuwa kama wazazi wake? Kwa hiyo mtoto wa mtu ukimkuta barabarani amezidiwa utamuacha kwa sababu siyo mwanao?
Lulu alikuwa na kazi ndogo sana ya kumuaga mama na akaruhusiwa. Ambayo ni kwenda ‘Location’. Na kweli anayempigia simu ni Steven Kanumba mama ataacha kumruhusu mtoto atoke ikiwa akienda anarudi na chochote? Location hata wiki wanakaa mama hawezi kuwa na hofu. yuko na Kanumba wanacheza filamu.
Unamlaumu Mama Lulu kwa kuruhusu mwanaye kwenda kwa Kanumba. Wakati kuna wanaume waliwaruhusu wake zao kisa wamepigiwa simu na Kanumba kwenda kufanya naye filamu?
Alichoponzwa Lulu ni imani kubwa ya mama yake kwa watu waliomzunguka Lulu.
Sawa ni makosa ya wazazi ikiwa ni pamoja na wazazi wake waliomlea kisanaa. Walimuacha mtoto atende makubwa kuliko umri wake. Walimuacha mtoto atendewe mazito kuliko umri wake.
Na badala ya kumsaidia wakaamua kujisaidia wao wenyewe kwa tamaa za ngono.
Katoto kazuri kale aiseee. Mungu akalinde na mateso ya gereza.
Na kuna wanawake wakubwa kabisa kwenye sanaa ya filamu waliogeuka kuwa makuwadi kwa Lulu. Hawakuwa na hofu ya Mungu zaidi ya kuwaza kipato cha ukuwadi.
Leo hii ukimtazama Lulu ni sehemu ya wasichana wenye miili midogo. Pata picha miaka mitano iliyopita alikuwaje? Aliwezaje kuingia kwenye kumbi za starehe na kina Kanumba katika umri ule. Hili nalo la kumlaumu mama yake ambaye muda huo alikuwa anaamini mwanaye yuko Location na Kanumba kumbe wapo klabu wanakula vyombo.
Sasa hapo ni kosa la mama au la Kanumba kujitoa ufahamu? Na wale walinzi wa mageti ya kumbi za starehe kukosa haya na kuruhusu kitoto chenye akili za kitoto kuingia klabu usiku wa manane kikiwa na jibaba lenye mwili mkubwa kama makabati ya maktaba?
Jamii kwa ujumla wake iliacha huyu mtoto afikie hapo alipofikia. Uzuri wake ni kwamba amepata matatizo akiwa bado na umri mdogo sana. Ana muda mrefu wa kurekebisha alipokosea.
Kuwepo kwake gerezani kuna kitu kikubwa sanaa inakikosa  kuliko kile Lulu anachokosa kwa kutokuwepo kwake mtaani.
Kupitia matatizo ya Lulu liwe somo kwa wazazi kuwa makini na kina Lulu wao majumbani wasiaamini sana watu aina ya Kanumba.
Kuna kina Kanumba kwenye utangazaji. Uandishi. Makondakta. Mabodaboda. Mabajaji na wauza chips mitaani. Wapo.
Somo zuri kwa tukio la Lulu ni kwamba siyo tu anatumika kingono bila wazazi kujua. Bali hata jamii inayowazunguka wanaacha mtoto wa mtu atafunwe na mabazazi yaliyokosa soni. Utu. Hofu ya Mungu na roho mbaya iliyopitiliza.
Mchunge mwanao mwenyewe usisubiri jirani akuchungie.
Kinachotokea kwa Lulu. Binti mdogo kama yeye ni makubwa mno. Hayabebeki.
Kuna watu wanafurahia matatizo ya Lulu huku akiwa guest na mpenzi wake ambaye siyo mume/mke wala mchumba. Hajui kuwa naye lolote linaweza kumtokea huko chumba namba saba.
Lulu ni dhahabu. Dhahabu lazima ipite kwenye tanuru la moto mkali ili iwe dhahabu.
Atarudi mtaani atakuwa mpya. Atapiga pesa. Maisha yatandelea. Asante Mungu kwa kumfanya Lulu awe sehemu ya somo zito kwa wazazi na watu wengi sana mitaani.