Kama Bongo Movie vile, Bongo Fleva nayo inaanza kurudi ilipotoka

Julie Kulangwa

Muktasari:

  • Miaka miwili au mitatu nyuma ulizuka mtindo wa wasanii kutegemea video kuzibeba nyimbo zao, lakini kwa mifano michache tu ya hivi karibuni utaona utamaduni huo unaanza kufa.

Wimbi la kutegemea video nzuri kuwa zitaubeba wimbo linaanza kupungua kasi. Kama wimbi hilo liliweza kupindua meli basi sasa linaonekana hata mashua itakuwa kazi ngumu kuizamisha.

Miaka miwili au mitatu nyuma ulizuka mtindo wa wasanii kutegemea video kuzibeba nyimbo zao, lakini kwa mifano michache tu ya hivi karibuni utaona utamaduni huo unaanza kufa.

Wiki mbili zilizopita Darassa baada ya kusumbua sana na wimbo wake Muziki, alitoa mwingine Hasara Roho. Niliwahi kuandika hapa kuwa mwanamuziki huyu ana deni kubwa pengine kuliko wasanii wote kwa mashabiki wake.

“Muziki” ulikuwa wimbo wa taifa uliotambaa na kuambukiza nchi jirani. Ukweli ni kwamba kama kuna mtu ametengeneza fedha katika kipindi hiki ambacho wengine tunalia njaa ni Darassa. Nyomi lake katika kila kiwanja au nchi anayotia miguu halikuwa la nchi hii.

Turudi kwenye wimbo mpya wa Hasara Roho. Ukweli haifikii viwango vya Muziki kwa kila kitu na mbaya zaidi sasa hivi sisi mashabiki tunausikiliza huu mpya kwa kuulinganisha na uliotangulia. Labda angeyajua haya angeutanguliza Hasara Roho halafu Muziki utoke sasa. Yote kwa yote muziki ni biashara ya kubahatisha. Alipotoa wimbo huo kuna mtu nilimsikia akisema baada ya kuusikiliza: “Si mkali lakini ngoja niisubiri video.” Video ni nzuri lakini ukweli ni kuwa tumeshazoea kuona vitu vya aina hii.

Wasanii wa WCB, Rich Mavoko, Harmonize na Rayvanny wametoa nyimbo mfululizo na kama kawaida yao ni safi kama jina lao, lakini je, video zimewasadia kwa kiasi gani kuzikuza nyimbo zao?

Bongo Movie imetoka huko sasa wanalazimishwa kurudi katika misingi yake. Walijisahau wakiamini kuwa sura yenye mvuto, picha zilizopigwa vizuri zinaweza kuwafanya washindane na japo Nollywood…imeshindikana.

Sasa wanaambiwa kuwa wakitaka kufanya vizuri sokoni lazima wawe na hadithi nzuri iliyopangiliwa kwa ustadi, picha zilizopigwa vyema na sauti isiyoumiza masikio au kumlazimisha mtazamaji akae karibu na rimoti yake.

Niionavyo Bongo Fleva inaanza kurudi kwenye misingi yake kwamba wimbo mzuri ndio kila kitu. Mashabiki wanaanza kupotezea video au tuseme nazo zimefika mwisho wa ubunifu wake. Hata mwanamuziki ‘underground’ naye anakwenda Afrika Kusini kurekodi video. Imekuwa kawaida sana. Sana.