Kilimo cha uyoga kinavyoweza kukuingizia kipato kizuri

Muktasari:

Hivi sasa uyoga sio tena zao adimu, zao ambalo zamani wengi tulizoea kuona likijiotea tu. Hivi sasa uyoga unalimwa tena kwa njia za kisasa kiasi cha kuwa chanzo kizuri cha mapato kama ilivyo kwa mkulima Ruth Samwel.

Umewahi kula keki ya uyoga? Je, unafahamu kama uyoga unaweza kukupa supu maridhawa ukafurahia chakula chako mezani?

Hivi sasa uyoga sio tena zao adimu, zao ambalo zamani wengi tulizoea kuona likijiotea tu. Hivi sasa uyoga unalimwa tena kwa njia za kisasa kiasi cha kuwa chanzo kizuri cha mapato kama ilivyo kwa mkulima Ruth Samwel.

Anasema alianza kulima zao hilo lenye virutubisho lukuki kwa afya ya binadamu tangu Mei mwaka huu.

Tofauti na aina nyingine za mazao, kilimo cha uyoga hufanyika ndani. Kwa Ruth yeye anatumia kibanda cha udongo kilichoezekwa na makuti kwani anasema uyoga haupatani na joto na hustawi sehemu yenye giza.

Kwa kupitia mifuko ya plastiki ambayo ndio mashamba yatumikayo kuotesha uyoga, huweka vimeng’enya ambavyo ni mahususi kwa ajili ya uyoga wake.

“Nikishaandaa vimeng’enya naviweka kwa muda wa wiki moja kwa kuvifunika vizuri ili visipate mwanga, baada ya hapo najaza kwenye mifuko yangu na hatua inayofuata ni kuchemsha kwa kutumia mvuke ili kuua bakteria”

Anasema vimeng’enya hivyo vyenye mchanganyiko wa majani makavu ya mgomba, taka zitokanazo na mbao, pumba za mahindi, pamoja na sukari, huchanganya na mbolea ya itokanayo na kinyesi cha kuku kwa ajili ya ukuaji mzuri wa uyoga.

“Inategemea na wingi wa mashamba yangu. Kwa mfano, yaliyopo sasa ni mashamba 500 hivyo natumia mbolea kilo tano. Kama mifuko ni 1,000 mbolea inabidi iwe kilo 10” anaeleza. Kwake kila mfuko mmoja wenye vimeng’enya ni sawa na shamba moja kama anavyoita yeye mwenyewe.

Anasema kilimo cha uyoga pamoja na kuwa ni cha kisasa, lakini kinaweza kutumiwa na mtu yeyote kutokana na njia zinazotumika kutotumia gharama kubwa.

INAENDELEA NUK 28

INATOKA UK 27

“Kilimo hiki nimejifunza ndani ya miezi mitatu tu, na kilichonisukuma kuingia kwenye kilimo hiki ni baada ya kuona wengi wanakidharau kwa kigezo kwamba watu hawapendi uyoga” anasema.

Baada ya kuona faida katika kilimo hicho, Ruth hakutaka kuingia katika kilimo kingine , alijikita moja kwa moja kama sehemu ya ajira kwake.

“Niliona kuwa wakulima nchini wanapenda kufanya vitu vya kufanana, mfano hivi sasa wakulima wengi wamejikita kwenye kilimo cha matunda kwa hiyo mimi nimetumia fursa hii kuwa tofauti,” anasema.

Ruth anayeendesha mradi wake Tuangoma wilayani Temeke, nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam, anasema uyoga aina ya aina ya ‘Mamama’ (Oyster mushroom) huchukua miezi miwili kuwa tayari kwa ajili ya kuwauzia wateja wake ambao ni wa jumla na rejareja.

“Nauza kilo moja kwa Sh10,000 na wateja wangu wa jumla hununua kuanzia kilo 10, huku wengine wakinunua bei ya rejareja kuanzia robo hadi kilo moja” anasema.

Anasema kupitia kilimo hicho sio tu amefanikiwa kufahamiana na wafanyabiasha mbalimbali na kumjengea mwanzo mzuri kibiashara, lakini uyoga unampatia kipato cha kuendesha familia yake.

“Kwangu mimi haya ni mafanikio pamoja na kwamba kilimo hiki sajakianza muda mrefu, lakini napata moyo wa kuendelea nacho kutokana na faida nipatazo,” anaongeza.

Faida ya uyoga kwa binadamu

Kila chakula kina umuhimu katika mwili wa binadamu, ndiyo maana wataalamu hushauri ulaji wa vyakula vyenye virutubisho ili kujikinga na maradhi.

Tofauti na vyakula vingine, uyoga una vitamin D nyingi ambayo hakuna matunda wala mbogamboga ambazo zinazoweza kufikia kiwango cha hicho.

Dk Sajjad Fazel ni mtaalamu wa dawa na tiba kutoka hospitali ya Sanitas jijini Dar es Salaam, anashauri jamii kujenga mazoea ya kula uyoga kutokana na faida zake kiafya.

Mbali na vurutubisho vipatikanavyo kwenye uyoga, anasema uyoga una madini mengi ya chuma, potashi na shaba.

Anasema mazoea ya kula uyoga mara kwa mara, huimarisha kinga ya mwili ambayo itasaidia mlaji kumkinga na magonjwa mbalimbali na kupitia vitamini D, mlaji ataimarisha ngozi yake na kuboresha mifupa.

Wito kwa Serikali

Anatoa rai kwa Serikali, pamoja na wataalamu wa afya kutoa elimu juu ya umuhimu wa kula uyoga kwani wengi hawana mwamko juu ya matumizi ya uyoga kiafya.

“Kama elimu itatolewa vizuri walaji wataongezeka, wengine bado wanadhani uyoga ni mimea inayojiotea, kwa hiyo wanatakiwa wajue umuhimu wa uyoga na faida zake kiafya na kiuchumi,’’ anasema.

Aidha, anaiomba Serikali kuunga mkono jitihada za wajasiriamali na wakulima wanaobuni mbinu mbalimbali za kilimo.

Anasema kama kilimo hiki kitapewa kipaumbele kina uwezo wa kumbadilisha mtu kutoka kipato cha kawaida hadi kipato cha juu.

‘’ Ikiwezekana Serikali ianzishe mashamba kwa ajili ya vijana ili kuepuka wimbi la vijana wasio na ajira,” anashauri.