Kilimo hai kinahitaji mbolea za asili

Mbolea kama hii ya asali ndiyo inayotakiwa kutumika katika kilimo hai.Picha nma Mkulima mbunifu

Muktasari:

  • Kwa walio wengi, suluhisho ni kutumia mazao yanayozalishwa kupitia kilimo hai.
  • Hiki ni kilimo kisichotumia madawa wala kemikali za viwandani. Bidhaa zake zinaelezwa kuwa ni bora maradufu ya bidhaa zinazozalishwa na mbolea za viwandani.

Ni ukweli usiofichika kuwa watu wengi wangependa kutumia bidhaa za mazao yasiyozalishwa na madawa na mbolea za kemikali zinazotengenezwa viwandani.

Kwa walio wengi, suluhisho ni kutumia mazao yanayozalishwa kupitia kilimo hai.

Hiki ni kilimo kisichotumia madawa wala kemikali za viwandani. Bidhaa zake zinaelezwa kuwa ni bora maradufu ya bidhaa zinazozalishwa na mbolea za viwandani.

Lakini kilimo hiki kinafanyikaje? Ili uweze kufanya kilimo hai ni lazima uwe na mbolea za asili. Bila mbolea za asili huwezi kufanya kilimo cha aina yoyote kwa misingi ya kilimo hai.

Mbolea za asili zipo za aina mbalimbali au huweza kutengenezwa kwa njia mbalimbali na kwa kutumia malighafi kama vile samadi, majani ya kurundika na nyinginezo.

Baadhi ya mbolea za asili na njia za kuzalisha mbolea za asili ambazo mkulima wa kilimo hai huweza kutumia katika kilimo kwa ajili ya uzalishaji bora, ni pamoja na mabaki ya mazao, mazao funikizi, matandazo, samadi na mboji.

Mbolea za asili zina faida kuu mbili, moja huongeza na kushamirisha viumbe hai katika udongo na pia ni huru kwa maana kuwa mkulima unaweza kuotesha au kutengeneza mwenyewe nyumbani au shambani kwako.

Aidha, ikiwa utakuwa na mbolea nyingi kupita mahitaji yako, unaweza kuuza na kujipatia fedha.

Hata hivyo, baadhi ya mbolea za asili zinakosa kirutubisho muhimu cha kutosha cha fosiforasi ambayo mmea huhitaji kwa ajili ya kukua.

Lakini upungufu huu unaweza kufanyiwa kazi kwa kuongeza mimea yenye virutubishi vya fosifirasi kwa wingi.

Mabaki ya mimea

Mabua na majani ya baadhi ya mazao ni mazuri sana kwa matandazo. Stover kutoka kwenye mahindi na mtama huanza kuoza taratibu na hivyo hukaa juu ya ardhi kwa muda mrefu kidogo na kufunika udongo.

Aidha, mabua na majani ya mikunde yana wingi wa naitrojeni na huoza kwa haraka hivyo kuwezesha virutubishi kutumika kwa haraka kwa mimea itakayofuata kuoteshwa.

Mazao funikizi

Mazao funikizi yanahitajika kuoteshwa mapema yakiwa yanafaa katika mseto wa kilimo, hivyo kuwezesha kukua na kufunika udongo. Baada ya kuota, yafyeke na kuacha juu ya ardhi kama masalia kabla ya kuotesha zao kuu linalofuata.

Mazao funikizi jamii ya mikunde ni muhimu sana kwani yanakusanya

naitrojeni kutoka hewani na kuifanya kutumika kwa mazao mengine.

Nyasi na magugu

Unaweza kukata na kukusanya nyasi na magugu kutoka pembezoni mwa shamba au kutoka katika eneo lingine na kuyatandaza shambani kama matandazo.

Hata hivyo, kuwa na tahadhari usichukue nyasi au magusu yenye mbegu kwani baadaye huota na kusababisha kuwapo kwa magugu shambani.

Kupogoa majani kutoka kwenye miti na vichaka

Unaweza kupogoa majani ya miti na vichaka ulivyovikata kisha kuweka kama matandazo shambani.

Miti na vichaka jamii ya mikunde ni mizuri zaidi kwa kuwa ina kiwango kikubwa cha naitrojeni na unaweza kuvuna vichaka katika kipindi chochote cha mwaka.

Aidha, baadhi ya mimea huoza haraka wakati mingine ikichukua muda kidogo, hivyo ni muhimu kutumia aina mbalimbali ya mimea ili kupata mchanganyiko mzuri wa kufunika udongo na hatimaye uweze kuozesha mimea kwa haraka wakati utakapohitaji.

Kinyesi cha wanyama (samadi)

Samadi inayotokana na kinyesi cha wanyama ni mbolea nzuri katika kilimo hai. Ni muhimu unapokusanya mbolea hii kuiacha kwa muda wa miezi kadhaa ili iweze kuoza kabla ya kupeleka shambani.

Unapoitumia mbolea hii moja kwa moja baada ya kutoka kwa wanyama, unahatarisha mimea yako kwa kuwa mbolea mbichi ina tabia ya kuunguza mimea.

Unashauriwa kutumia samadi inayotokana na na kuku kama kipaumbele cha kwanza. Unapokosa samadi ya kuku, unaweza kutumia kinyesi cha mbuzi, kondoo na kinyesi cha ng’ombe.

Mboji

Hii inajumuisha mabaki ya vitu mbalimbali. Unaweza kutengeneza mboji kutokana na majani, magugu, samadi, majivu, mabaki kutoka jikoni au malighafi yoyote ya asili yanayopatikana katika eneo lako.

Wakati wa kutengeneza mboji, jaribu kutumia malighafi inayooza haraka na kuzalisha mboji mapema kama vile nyasi na majani.

Unaweza pia ukatengeneza mboji kwa kuweka malighafi kwenye shimo hasa katika maeneo yenye mvua kidogo au za wastani.

Makala haya ni kwa hisani ya mtandao wa mkulimambunifu.www.mkulimambunifu.org