Kuna huu upande wa pili sasa…

Muktasari:

  • Kumekuwa na hoja za mambo yanayoendelea katika medani za soka, lakini tutaionyesha nini Fifa usafi wetu katika utawala bora wa soka Tanzania.

Wakati viongozi wa juu wa Shirikisho la Soka la Kimataifa, Fifa na lile la Afrika, CAF wakiwasili nchini, kuna mengi yanaweza kuangazwa ambayo ninaweza kusema ni ya upande wa pili.

Kumekuwa na hoja za mambo yanayoendelea katika medani za soka, lakini tutaionyesha nini Fifa usafi wetu katika utawala bora wa soka Tanzania.

Kimsingi, tunasifia lakini kiukweli, hakuna ligi imara za mpira wa miguu kwa vijana na wanawake huku pia mfumo wa utawala bora unaozingatia weledi na uwazi ukiwa ni ndoto za alinacha.

Tangu Tanzania ilipoanza kupokea mamilioni ya fedha za kuendeshea na kusimamia miradi ya soka hadi leo hii, tuna jambo gani kubwa ambalo tunaweza kujivunia kama nchi tumefanikiwa zaidi kwenye mchezo wa soka kulinganisha na nchi nyingine kupitia fedha hizo?

Kama nchi, ni wazi tumeshindwa kuzalisha makocha bora ambao wangekuwa hata wanagombewa nje ya Tanzania. Mfano mzuru tunaiona nchi ndogo tu ya Burundi, makocha wametawanyika Afrika kwani hata kocha wa Gendarmerie ya Djibouti ni Mrundi, Issa Mvuyekure.

Mbali na kutawanyika nje ya Tanzania kufundisha, kwa ambao wangekuwepo, wangekuwa chachu ya kuibua, kukuza na kuendeleza vipaji vya soka hasa kwa vijana wadogo.

Badala yake sasa, klabu zetu zimeendelea kupigana vikumbo kuajiri makocha wa kigeni kutokana na uwezo duni wa kundi kubwa la makocha wazawa.

Tumeshindwa kuandaa mipango imara ya kuhakikisha tunazalisha kundi kubwa la wachezaji bora ambao watakuwa msaada kwa timu yetu ya taifa na na hii inalazimisha viongozi wa klabu kuelekeza nguvu kwa wachezaji wa kigeni ambao wanaongeza gharama za klabu na wanachota mamilioni ya fedha ambazo zingelipwa kwa wachezaji wazawa.

Tunaweza kuandaa shughuli nyingi za kitalii na kiutamaduni kama sehemu ya burudani kwa msafara mzima wa Infantino na watu wake lakini ni lazima tukumbuke Fifa ipo kwa ajili ya kusimamia na kuendeleza mchezo wa mpira wa miguu.

Kwa kuwa wamekuwa wakitoa fedha kusaidia maendeleo hayo, furaha kubwa kwa jopo hilo linalokuja itakuwa ni pale watakapojiridhisha pasipo na shaka kwamba fedha wanazotoa zinatumika vizuri lakini pia maagizo ambayo wamekuwa wakiyatoa kwa ajili ya uendeshaji wa soka, yanafuatwa kikamilifu.

Soka ya wanawake, soka ya vijana wa rika mbalimbali na uimarishaji wa miundombinu ya soka kama viwanja, vifaa vya michezo, wataalamu kama madaktari wa michezo, wanasaikolojia na wakufunzi mbalimbali.

Pia utekelezaji wa maagizo ya Fifa kwa kuzingatia agizo la mkutano wa Bagamoyo.