Makundi ya Morocco, Nigeria na Tunisia siyo ya kitoto!

Muktasari:

  • Unaambiwa Rais wa CAF aliyepita, Issa Hayatou, tangu aingie madarakani Lionel Messi akiwa na mwaka mmoja, hajawahi kufanya. Hayatou alimwagwa kwenye uchaguzi wa CAF uliofanyika Addis Ababa Machi 16, mwaka huu.

Kuna kitu hakijawahi kufanyika Afrika lakini juzi Rais wa Shirikisho la Soka Afrika, CAF, Ahmad Ahmad alifanya, alizipa nchi zilizofuzu Fainali za Kombe la Dunia, kila mmoja Dola 500,000 za maandalizi.

Unaambiwa Rais wa CAF aliyepita, Issa Hayatou, tangu aingie madarakani Lionel Messi akiwa na mwaka mmoja, hajawahi kufanya. Hayatou alimwagwa kwenye uchaguzi wa CAF uliofanyika Addis Ababa Machi 16, mwaka huu.

Achana na Hayatou, Ahmad Ahmad anataka kuiweka Afrika karibu kwa kila mmoja, ametoa nafasi kwa timu kujiandaa, anaziandalia mechi za majaribio lakini pia amesogeza mechi za kuwania kucheza Afcon 2019 zilizokuwa zichezwe Machi mwakani akazipeleka Oktoba mwakani.

Mataifa matano ya Afrika yatakayokwenda Moscow, Russia kwenye Fainali za Kombe la Dunia ni Nigeria, Morocco, Tunisia, Misri na Senegal.

Ijumaa jioni, wenyeji wa fainali hizo waliandaa hafla kubwa ya kupanga ratiba na makundi ya fainali hizo zikiwemo nchi hizo za Afrika.

Ukiangalia droo hiyo, mataifa ya Morocco na Nigeria yatakuwa na kibarua pevu katika makundi yao.

Nigeria imepangwa na mabingwa wa zamani Argentina. Super

Eagles inaweza kugeuziwa kibao licha ya kuifunga mabao 4 – 2 katika mchezo ya kirafiki hivi karibuni. Mbali na Argentina,

Nigeria itakutana na Croatia na Iceland katika Kundi D.

Kundi B, Morocco watakuwa na shughuli pevu watakapokutana na kasi ya Cristiano Ronaldo na mastaa wengine wa Ureno. Timu hiyo pia ni bingwa wa Ulaya.

Shughuli nyingine watakayokutana nayo Morocco ni kwa wakali wa Hispania na timu isiyotabirika ya Iran.

Wawakilishi wengine wa Afrika, Tunisia watakutana na mziki wa Ubelgiji utakaokuwa ukiongozwa na Romelu Lukaku katika Kundi G. Nchi nyingine katika kundi hilo ni England na wageni wa fainali hizo, Panama.

Misri walioko Kundi A itawalazimika kuweka pembeni masuala yao ya kidiplomasia na kuingiliana na Saudi Arabia.

Pia watakumbana na joto la wenyeji, Russia. Timu nyingine watakayokumbana na nayo ni wataalamu wa rafu, Uruguay.

Senegal walioingia robo fainali za Kombe la Dunia mwaka 2002 Korea Kusini na Japan wanaonekana kutokuwa na kazi ngumu, lakini shughuli watakutana nayo kwa Poland, Colombia na Japan na jina la Sadio Mane tayari limeanza kuonekana kama litakuwa tishia katika Kundi hilo kutoka Senegal.

Rekodi za Wawakilishi wa Afrika

1. MISRI – ‘Pharaohs’ ilicheza Fainali za Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza nchini Italia 1990

2. MOROCCO – ‘Simba wa Atlas’ walifuzu wakiwa na rekodi nzuri Afrika.

3. NIGERIA – ‘Super Eagles’ wamekosa Fainali moja tangu walipocheza Fainali za Kombe la Dunia Marekani 1994

4. SENEGAL – Waliingia kwa mara ya kwanza Korea/Japan 2002, Simba wa Teranga wakaingia robo fainali.

5. TUNISIA – walicheza Fainali za Argentina 1978, ‘Tai wa Carthage’ ilikuwa timu ya kwanza kushinda mechi ya Kombe la Dunia.

FAINALI ZA 2014 VS 2018

Mwaka 2014 timu za Afrika zilizofuzu ni Ghana, Cameroon, Ivory Coast, Nigeria na Algeria. Moja ya Afrika Kaskazini na nne kutoka sub Sahara.

Miaka minne baadaye, ni Nigeria pekee ikarudi kwenye fainali. wakati huo sasa ikawa na timu nyingine ya Afrika Magharibi, Senegal.

Timu nyingine ni kutoka Afrika Kaskazini – Misri (mabingwa mara nyingi wa Afcon), Morocco na Tunisia.

Timu kutoka mataifa mengine

UKANDA WA UEFA – ULAYA

UBELGIJI – Walifuzu wakitokea Kundi H na hawakupoteza mechi hata moja.

CROATIA – Wazoefu, walikuwa watatu Fainali za Ufaransa 1998

DENMARK – Walifuzu kiulaini kwa kuifunga Jamhuri ya Ireland.

ENGLAND – ‘The Three Lions’ wameingia mara ya 14 kati ya 16 walizoshiriki.

UFARANSA – ‘Les Bleus’ wanacheza mara ya sita mfululizo.

UJERUMANI – Waliingia wakijiamini kwa ushindi wa asilimia 100.

ICELAND – Taifa lenye idadi ndogo ya watu kuwahi kufuzu.

POLAND – ‘The Poles’ walikuwa wa tatu Fainali za Ujerumani mwaka 1974 na Hispania 1982

URENO – ‘Seleção das Quinas’ Fainali za tano mfululizo.

RUSSIA – Kama Soviet Union, walikuwa wanne Fainali za England 1966

SERBIA – ‘The Serbs’ilifuzu kutokea Ukanda wa UEFA Kundi D ikipoteza mechi moja.

HISPANIA – Mabingwa 2010, ilianza kucheza Fainali za Italia 1934.

SWEDEN – Walimaliza wa pili Fainali za Kombe la Dunia 1958.

USWISI – Mara tatu wamemaliza nafasi ya tatu Kombe la Dunia.

CONMEBOL – AMERIKA KUSINI

ARGENTINA – Mabingwa mara mbili. Walikuwa kwenye uzindizi wa Kombe la Dunia mara ya kwanza nchini Uruguay 1930

BRAZIL – ‘Seleção’ ilikuwa ya kwanza kufuzu fainali za mwakani ukiacha wenyeji Russia.

COLOMBIA – ‘Los Cafeteros’ ilikuwa chini ya kocha, Jose Pekerman raia wa Argentina Fainali za Ujerumani mwaka 2006.

PERU – Imerudi Fainali za 2018 baada ya miaka 36.

URUGUAY – ‘La Celeste’ walitwaa ubingwa 1930 na Fainali za Brazil 1950

CONCACAF – AMERICA KASKAZINI

COSTA RICA – ‘Los Ticos’ ilionyesha soka yake Brazil 2014, na kuingia robo fainali.

MEXICO – ‘The Mexicans’ ilipoteza mechi moja ikiwani kufuzu Russia 2018

PANAMA – Imetokea Amerika ya Kati, imefuzu kwa mara ya kwanza Russia.

UKANDA WA AFC – ASIA

AUSTRALIA – ‘Socceroos’ Inaingia mara ya tano Kombe la Dunia.

IRAN – ‘Team Melli’ timu ya kwanza Asia kwenda Russia 2018

JAPAN – Mara ya 16 kuingia fainali.

JAMHURI YA KOREA – ‘The Taeguk Warriors’ Haikuwahi kucheza Kombe la Dunia tangu 1986

SAUDI ARABIA – Ilianza kucheza Fainali za Kombe la Dunia 1994 nchini Marekani.