AJIRA NA KAZI: Mambo ya kuzingatia kwa waajiriwa mwaka 2017

Muktasari:

Unaweza kuwa katika kundi la watu wenye utamaduni wa kushiriki mwaka mpya, kwa tafsiri ya kusamehe yaliyopita, kujitathmini na kuweka malengo mapya.

Inawezekana kila mwaka umekuwa miongoni mwa mamilioni ya Watanzania wanaonza mwaka mpya kwa mikogo na mbwembwe nyingi

Unaweza kuwa katika kundi la watu wenye utamaduni wa kushiriki mwaka mpya, kwa tafsiri ya kusamehe yaliyopita, kujitathmini na kuweka malengo mapya.

Kuna kundi linalosherehekea baada ya kuongeza idadi ya miaka, wapo wanaoshereheka kwa kushinda vikwazo vya mwaka uliopita.

Katika makala haya naangazia mambo sita ambayo mwajiriwa anapaswa kuyazingatia tunapoanza mwaka mpya wa 2017.Inawezekana mwaka 2016 ulibakia nyuma kwa sababu ya wengine au kwa makosa yako mwenyewe, lakini ukijaribu mambo haya, mwaka huu unaweza kuwa wa mafanikio kwako.

Ongeza thamani

Kuna mambo matatu yanayoweza kuongeza thamani ya mwajiriwa kazini bila kujali uzoefu.Kwanza ni muhimu kuongeza mbunifu. Inawezekana umekuwa ukifanya hivyo au hukuwahi kujihusisha lakini ni jambo la msingi.

Ubunifu unahusisha zaidi kufikiria mambo mapya au mawazo yanayohusiana na ofisi yako ili kuongeza thamani yako kazini.

Pili, ni muhimu kuongeza kiwango cha elimu yako. Hii inatofautiana na suala la ubunifu kwani unaweza kuwa mbunifu licha ya elimu ndogo uliyonayo na ukawa bora kuliko wenzako wanaokuzidi elimu

Unaweza kujisomea mambo yanayohusu taaluma yako kwa njia ya mtandao au kuhudhuria madarasa ya baada ya muda wa kazi. Kimsingi, tengeneza muda na ratiba isiyoweza kuathiri ajira yako.

Tatu, unatakiwa kuendelea kuonyesha uwezo zaidi wa kile unachokijua mbele ya wafanyakazi wenzako ili wakutambue.Tumia njia chanya kuwasilisha ili kuepuka kuwakwaza.

Kumbuka ajira yako inawindwa na watu wengine wenye uwezo na hata uzoefu kuliko hata ulionao. Mchango wako ofisini ni sawa na mchezaji wa soka, ambaye kiwango chako ndiyo kinakutengenezea thamani katika soko la usajili.

Linda hadhi yako

Je wewe ni muongo, mbabaishaji au haupo makini? Umewahi kujiuliza ofisi na wafanyakazi wenzako wanakutambua kwa utambulisho wa mtu makini, mwelevu, mchapakazi, mbishi, mjuaji, mchekeshaji tu au mzigo tu.

Ziko sababu za kimazingira zinazoweza kusababisha ukaonekana una au hauna mchango. Lakini kwa sehemu kubwa hupaswi kumnyooshea kidole mfanyakazi mwenzako.

Kumbuka uwezo wako ni jambo moja na hadhi yako ni jambo lingine. Lakini baada ya kuona hivyo umefanya nini? Umewahi kujitathmini kati yako na ofisi unayofanya kazi ni upande gani ulionufaika zaidi ya mwenzake?

Je, umeinyonya ofisi yako au imekunyonya? Je, umekuwa na matokeo gani kwako binafsi.Unadhani kwa miaka uliopo ofisini, elimu na uzoefu vina uhusiano na nafasi au kipato ulichonacho. Ni mambo gani yamekwamisha. Umemshirikisha nani na kwa namna gani.Ulipata mrejesho?

Pengine una tatizo la aina ya mavazi au mazungumzo yako. Unadhani umeathiriwa na ulevi au sifa mbaya kama udokozi, uzinzi, uchafu na tabia nyinginezo zinazokera?

Kama ulifanya hivyo mwaka 2016, hakikisha unabadilika haraka, vinginevyo, utaendelea kukosa raha. Jitathmini kwa kuuliza marafiki zako, waulize wewe ni mfanyakazi wa aina gani? Waulize viongozi unatakiwa kufanya nini ili kujenga taswira mpya.

Vumilia

Umekuwa mtu wa kulalamika kila jambo. Wakati mwingine unahisi unatengwa au kutopewa nafasi.Umejaribu pengine njia kadhaa kupata faraja lakini hujafanikiwa.

Jiulize matatizo yanayokusonga ni jambo la kujitakia au unatengenezewa mazingira hayo. Jitathmini ili kujua endapo umetengenezewa na ni kwa nini. Kumbuka unaishi katikati ya binadamu bila kujali anayekuongoza, lakini jaribu kutambua zaidi bosi wako anataka nini na kwa wakati gani.

Epuka kumkwaza kwa jambo lisilokuwa na ulazima. Mambo mengine kaa kimya na usionyesha chuki ukitofautiana japo ni vyema kutumia busara kuwashirikisha wafanyakazi wenzako kwa mrengo chanya.

Ongeza kujiamini kwako

Tafsiri ya kujiamini ndiyo inayozaa kuaminika.Kuaminika ndiyo kunazalisha mafanikio yako. Na hali ya kujiamini haijitokezi kwa bahati mbaya ila ni muhimu kwanza kuwa mjuzi wa mambo. Ili kuishi katika dunia mpya ya taaluma, ni lazima kujenga uwezo wa kujiamini katika kile unachokiamini.Hali hiyo itakujengea heshima ofisini kwako.

Mwaka 2017, jaribu kuhakikisha unatenga muda wako kwa ajili ya kuongeza maarifa kupitia usomaji wa vitabu na makala mbalimbali zinazohusu ajira yako. Kujiamini pekee haitoshi lakini kujiridhisha na unachoambiwa na kutetea unachokiona kwa macho yako.

Rekebisha makosa yako

Kuna makosa ya kutengenezewa na kuna makosa ya kutengeneza mfanyakazi mwenyewe. Kufanya makosa yanayokuwa kinyume na kanuni za ofisi yako kunaweza kuathiri ajira yako moja kwa moja. Ni kigezo cha kwanza kutofanikiwa.

Lakini kuna makosa mengine yanayohusiana kwa karibu na taaluma ikiwemo mwenendo wa tabia yako, uhusiano wako na wafanyakazi wenzako.

Pengine hata unavyovaa mavazi yako na unavyoishi kwa matendo yako na jamii nje ya ofisi. Ujumbe unaoweka mitandaoni vina uhusiano mkubwa na ajira yako.

Makosa hayaepukiki lakini ni muhimu kuwa makini ili kujilinda zaidi na kibarua chako, utambulisho wako. Jitathmini 2016 umefanya makosa ya aina gani, umeyashughulikia au bado na kwa nini imekuwa vigumu.

Angalia uhusiano wako na wengine

Nguzo ya mfanyakazi yeyote kufanikiwa ni uhusiano mzuri na wengine.Uhusiano kazini utakusaidia kupata ushirikiano wa mambo kadhaa usiyoyafahamu na mengine yaliyofichika.

Siyo rahisi kuwa na uhusiano na kila mtu, lakini jaribu kuwa makini na vikwazo na uwatambue wanaoweza kuwa watetezi wako pale inapotokea changamoto ya kikazi.

Angalia watu walioshikilia maslahi yako na upime changamoto za vikwazo vinavyoweza kukutenganisha nao. Kuwa mtulivu lakini isiwe kwa kiwango cha kupitiliza na ukabadilika asili yako ya awali.

Tumia busara kuwasiliana na wenzako.Usijifanye wa tofauti au kundi la watu muhimu zaidi ofisini kwa sababu ya utofauti wa kipato, elimu au ajira yako.

Nje ya ofisi yako angalia tena uhusiano wako. Unatambuliwa na nani na kwa mtazamo upi.Fursa unazipata au zimejificha nyuma yako kwa sababu ya kujitenga kwako? Tumia maarifa yako kwa mwaka 2017 kujenga taswira yako mpya.