Mbinu bora za utoaji wa chakula kwa kuku

Mfugaji akilisha kuku wake chakula. Wafundishe kuku wako kula chakula chote kiishe asubuhi ili jioni wapate hamu tena ya kula chakula chote. Picha na mtandao wa livestocking. net

Muktasari:

Nawakaribisha watu wote wenye nia na biashara hii waendelee kunufaika na makala hizi za mara kwa mara kujifunza mbinu na kanuni mbali mbali kuboresha kazi ya ufugaji.

Napenda kuwapongeza wote wanaofuatilia kwa karibu makala haya ya ufugaji wa kuku kwa muda mrefu. Bado naguswa kuendelea na harakati hizi za kutoa elimu juu ya ufugaji wa kuku kwa wafugaji na kuongeza ufanisi zaidi kwenye biashara hii.

Nawakaribisha watu wote wenye nia na biashara hii waendelee kunufaika na makala hizi za mara kwa mara kujifunza mbinu na kanuni mbali mbali kuboresha kazi ya ufugaji.

Ukizingatia makala hizi na kuzifanyia kazi, ni dhahiri kwamba unaweza kubadilisha hali yako ya uzalishaji shambani kutoka kuzalisha kwa faida ndogo na kuingia kwenye uzalishaji wenye faida kubwa.

Kosa dogo katika biashara huleta upungufu mkubwa kwenye uzalishaji na faida kwa ujumla.

Kila siku biashara hubadilika kulingana na mazingira, teknolojia, upeo wa watu na mahitaji ya jamii.

Kuna wakati unahitaji kupata mawazo mengine mapya na kupanua fikra zaidi ili kuendana na hali ya ushindani katika soko la biashara.

Kampuni kubwa na mashirika mbali mbali wanajua kuwa kila baada ya muda watumishi wao wanahitaji kupewa elimu kwenye kazi zao, ili kuongezewa upeo na namna ya kufikiri na kutoa huduma bora kila wakati.

Hivyo hivyo katika ufugaji kwani ni sekta kubwa inayoweza kuajiri watu na kuwalipa vizuri sawa na biashara nyingine kubwa za mashirika au kampuni.

Hakuna shirika au kampuni inayoweza kusimama bila kuanguka kama elimu haitolewi kwa wafanyakazi wake.

Ndiyo maana utaona semina zikitolewa mara kwa mara kwenye mashirika na kampuni bila kujali gharama kubwa ya kuendesha semina au mafunzo ya mara kwa mara.

Pengine wanafanya hivyo kwa sababu wanajua faida ya kutoa elimu kuimarisha usimamizi na utoaji huduma bora katika mambo yao wanayofanya.

Ukienda kupata ushauri wa kuanzisha biashara fulani kwa mtu swali la kwanza atakuuliza ‘una uzoefu gani au una mtaalamu wa kukuongoza?’

Elimu ni mwongozo kwa mtu ili asikosee jambo kwenye kazi yake na kupata hasara. Makala haya ni mwongozo mzuri kwa mfugaji, ni semina au mafunzo ya kuongeza upeo wa kufikiri kuendana na mazingira ya uzalishaji kwa faida. Maendeleo katika jambo lolote yanakuja baada ya kupangwa na kutafutwa kwa kufuata maelekezo ya watu wenye ujuzi, kusoma maandiko au kuhudhuria semina zinazofundisha mambo hayo. Ukurasa huu kwa wafugaji ni sehemu ya kupata elimu kwa urahisi.

Ulishaji kuku

Katika makala yaliyopita tuliona ni namna gani ulishaji kwa kuweka vyombo vichache bandani, unavyosababisha kuku kukua kwa matabaka.

Tuliona kuku au vifaranga wenye nguvu hutangulia kula chakula chote chenye virutubisho na kuacha vifaranga wanyonge wakila mabaki.

Ili kuepuka tatizo hilo tuliona kuwa ni vema mfugaji aweke vifaa vya kutosha ili kuku wote wapate chakula kwa pamoja tangu siku ya kwanza vifaranga wanapoingia bandani.

Hii itawasaidia kukua kwa pamoja bila kutokea wa kumpiga mwenzake wakati wa kulisha.

Moja kati ya matokeo mazuri ambayo tuliona endapo mfugaji atafuata kanuni hizi za ulishaji bora, ni pamoja na kuku kufikia umri wa kutaga mayai au kuuzwa wakiwa wote wanalingana.

Faida ya kulingana kwa kuku wanapofikia umri wa kuzalisha ni kubwa kwani hata uzalishaji wao utakuwa mzuri.

Kama ni kuku wa mayai watataga mayai mengi; kama ni kuku wa kuuzwa kwa ajili ya nyama mteja hatochagua kuku kwa sababu wote wanalingana hivyo mfugaji anaweza kuuza mara moja na kuingiza wengine.

Sehemu hii katika ulishaji ni muhimu na inatakiwa kuangaliwa na wafugaji wote kwenye mifugo yote.

Mbali na ulishaji na idadi ya vyombo vya kulishia, leo tuangalie namna ya utoaji wa chakula kwa kuku.

Kuku ni mifugo wenye kuzoea haraka mazingira. Mfugaji wa kuku anatakiwa kuwa na muda maalumu wa kulisha kuku wake; sio kila wakati unafaa kulisha kuku.

Lisha chakula mapema asubuhi kuku wanapoamka na jioni wakati jua limepoa. Weka utaratibu unaojulikana ili kuku waelewe saa ya kula na saa isiyo ya kula.

Usilishe chakula wakati wa mchana jua likiwa kali au usiku kuku wakiwa wamelala.

Kuku ni sawa na ndege wengine tabia zao hupangiliwa kwa muda hivyo ni vizuri kutoa huduma kulingana na wakati.

Kama kuku wamefikia umri wa kupimiwa chakula, hakikisha unawapa chakula nusu asubuhi mapema na nusu iliyobaki jioni na ratiba hiyo waizoee.

Kuku wasiolishwa kwa utaratibu hukosa hamu ya kula na kujikuta kila siku chakula kinabaki kwenye vyombo vya kulishia na uzalishaji au ukuaji kushuka. Wafundishe kuku wako kula chakula chote kiishe asubuhi ili jioni wapate hamu tena ya kula chakula chote.

Hii itasaidia kuongeza uzalishaji na ukuaji wakiwa wote wamelingana tangu wakiwa wadogo. Wakati wa kulisha hakisha unatumia ndoo na bakuli la kuchotea na kuweka kwenye vyombo vya kulishia.

Weka chakula kidogokidogo kwanza kwenye vyombo vyote ili vipate chakula na kuku wasambae kwenye vyombo vyote kisha rudia kujazia kwenye vyombo kadiri inavyotakiwa.

Usiweke chakula kikaishia njiani na vyombo vingine vikabaki tupu; utasababisha fujo na kugombania nafasi bila sababu.

Mara baada ya kuweka chakula kwenye vyombo vya kulishia, toa vyombo vya maji na vioshe kwa maji safi na kurudishia maji haraka. Kuku hawatakiwi kukosa maji kwa muda mrefu.

Epuka kulisha chakula kisichofaa. Hata kama utafuata kanuni za utoaji chakula kwa wakati, itakuwa kazi bure kwa sababu kuku watakosa lishe ndani ya chakula na kubaki hawana uwezo wa kuzalisha ipasavyo.

Lisha mchanganyiko wenye makundi yote ya chakula uliochanganywa kwa uwiano sahihi kwa kila kundi la virutubisho.