Mbinu mbadala zinazoweza kupaisha kazi za mjasiriamali

Hakuna faida ya kuwa miongoni mwa wajasirimali wanaotengeneza bidhaa nzuri na zinazoweza kufanya vizuri katika ushindani wa soko la ndani na hata nje ya mipaka ya Tanzania, lakini bidhaa hizo hazifahamiki.

Inawezekana umekuwa mbunifu na mara kadhaa umekuwa ukitamani bidhaa yako iweze kufika mbali zaidi ya masoko ulionayo.

Unaweza kuwa na jina kubwa kuliko bidhaa lakini bidhaa yako haijulikani.

Hatua ya bidhaa kufikia watumiaji wengi ndiyo mafanikio ya kazi ya mjasirimali yeyote aliyejiajiri mwenyewe.

Kumbuka, katika ushindani wa soko, hakuna miujiza rafiki.Sasa umekata tamaa au unatumia njia gani kusukuma bidhaa yako iweze kuwafikia walengwa, uongeze kipato na kubadilisha maisha yako kiuchumi.

Kama unamiliki simu ya kisasa, inaweza kukufanya bilionea kupitia jukwaa la watumiaji wa mitandao.

Katika Makala haya, nitazungumzia jinsi gani mjasiriamali anavyoweza kupanua biashara yake kwa kufikia wateja wengi zaidi kupitia matumizi ya kurasa za mitandao ya kijamii.

Panga ratiba ya kazi zako vizuri

Katika saa 24 za siku moja, hakikisha unaweka ratiba itakayokuongoza kuweka na kupokea mrejesho wa matangazo ya bidhaa zako mitandaoni.

Utafiti unaonyesha kurasa zenye idadi kubwa ya watu ni Twitter, Facebook, Instagram. Unaweza kujisajili pia katika kurasa za LinkedIn na zaidi usikose kujiunga na majukwaa ya mawasiliano ya WhatsApp na Snapchat.

Unatakiwa kufungua akaunti hizo kwa sababu ni majukwaa yanayowakutanisha watu mbalimbali ndani ya Tanzania, Afrika na Duniani, watumiaji wa bidhaa na wazalishaji.

Weka ratiba ya kutembelea majukwaa hayo kwa dakika kadhaa asubuhi na jioni ili kupata taarifa mpya, kutuma na kujibu ujumbe. Usipofanya hivyo, dunia itakuacha hatua nyingi nyuma katika ushindani wa bidhaa zako.

Kalenda na muda wa kuingia ni siraha itakayokusaidia kuongeza idadi ya marafiki kwa sababu kuna utafiti mwingi unaonyesha muda wa idadi kubwa ya watu wanaoingia na kutoka katika mitandao ya kijamii.

Hakikisha unaweka ratiba vizuri na kujua nini unachotakiwa kusambaza na kwa muda gani.

Kwa mfano, unaweza kufikiria nini unatakiwa kusambaza ndani ya mwezi mmoja ujao.

Unaweza kutumia softwea za kalenda kama eClincher au Hootsuite kwa ajili ya kuhifadhi taarifa zote muhimu kabla ya kuzisambaza mtandaoni.

Tafuta tovuti zinazokuhusu

Usipoteze muda mwingi kuandaa taarifa nyingi kuhusu bidhaa yako kwa ajili ya kutupia mitandaoni kwa wateja wapya unaowahitaji.

Jambo la muhimu ni kutafuta tovuti 10 au 15 zinazoaminika na zinazohusika na utengenezaji wa bidhaa zako.

Kwa mfano, unafanya biashara ya kuuza Korosho. Muhimu ni kuangalia tovuti zenye taarifa mbalimbali kuhusu biashara yako, mbinu za kibiashara ikiwamo namna ya kuyafikia masoko.

Tovuti hizo zitakusaidia kupata taarifa mpya, kuandika na kutupia katika kurasa zako mitandaoni ili kuongeza ushawishi kwa watumiaji.

Zingatia taarifa mpya zenye mashiko kuhusu bidhaa yako katika kila utakachohitaji kutupia kwenye ukurasa wako.

Tengeza ujumbe wa kusambaza

Baada ya kupata tovuti na vyanzo vya taarifa mpya, tengeza ujumbe wa bidhaa kabla ya kuitupia mtandaoni.

Kwa mfano, kama ni mjasirimali wa kuuza mafuta ya nazi, unataka watu wafahamu nini kuhusu ubora wa bidhaa hiyo.

Siyo kila kitu unatakiwa kutupia mtandaoni kuhusu bidhaa yako, hakikisha ujumbe au picha utakayotuma inavutia na inaibua hisia kuhusu ubora wa bidhaa yako.

Bidhaa yako inaweza kuwa bora lakini ujumbe ulioutuma haushawishi watumiaji wapya.

Maoni au mapendekezo, changamoto zitakazoibuliwa na wachangiaji, yatakusaidia kupata mrejesho na jinsi ya kufanyia kazi taarifa ulioituma mtandaoni.

Rudia kusambaza ujumbe tofauti wa bidhaa yako mara kadhaa katika kurasa zako mtandaoni na hakikisha unasambaza wastani wa asilimia 80 ya taarifa zinazohusu ubora na upatikanaji wa bidhaa zako.

Unaweza kusambaza picha, ujumbe mfupi wa kuvutia, vipande vya video ili watu waizoee bidhaa yako machoni.

Watalaamu wa Saikolojia wanasema kitu kinachojirudia kusikika maskioni au kuonekana machoni ndiyo hudumu kwenye akili ya mwanadamu.

Ndiyo maana utajiuliza kwanini matangazo ya simu za mkononi yanarushwa kila baada ya dakika redioni au katika televisheni, sababu kubwa ni hiyo.

Jiondoe kwa kundi lisilokunufaisha

Kumbuka kuna watu muhimu waliokosa mbadala wa kupata bidhaa nzuri kama unazotengeneza. Hivyo, ukifanikiwa kuwafikia maana yake utakuwa umeua soko la washindani wako na utakuwa umeingia kwenye mtandao mkubwa.

Kwa mantiki hiyo, hakikisha unakuwa na marafiki wanaoendana na mahitaji ya bidhaa zako wanaoweza kuguswa kwa karibu zaidi na kazi zako uzifanyazo.

Fanya utafiti wa mtandao kila mwezi

Mabadiliko hufanyika haraka kwa washindani wako wapya wanaoingia mitandaoni. Kila baada ya mwezi, unahitaji ripoti itakayokuonyesha ni posti gani zilifanya vizuri, nani aliyevutiwa zaidi na bidhaa zako, watakupataje, washindani wako ni akina nani na wanakuzidi nini. Usipoandaa ripoti, hautakuza soko la bidhaa yako kwa haraka.

Unaweza kushangazwa na taarifa unazozipata kama mrejesho, itakusaidia jinsi ya kuwa bora na kuongeza ubunifu katika mabadiliko ya soko la aina ya bidhaa yako.

Fuatilia wateja wako

Tafuta tovuti inayotoa takwimu za kimtandao kila wakati. Mtandao wa Swayy, ndiyo unaaminika zaidi katika utoaji wa taarifa za kimitandao ambazo zinaweza kusaidia ufuatiliaji wa karibu taarifa zinazosambazwa mitandaoni.

Wafuatilia hao na waratibu wa mitandao ya kijamii (Swayy), kazi kubwa wanayofanya ni kukusanya taarifa za watumiaji wakubwa wa mitandao ya kijamii. Kwa takwimu zilizopo sasa, wanabainisha zaidi ya taarifa 4.75 bilioni zilizoko katika mfumo tofauti zinasambazwa katika mtandao wa Facebook kila siku huku milioni 500 zikisambazwa na twitter kila siku.

Kila mtumiaji anayetumia kibiashara hakosi kufuatilia taarifa zinazohusiana na maslahi yake. Kwa mfano, mameneja, maofisa masoko, maofisa uhusiano, washauri wa kuuza majina ya bidhaa, kampuni au mtu binafsi wanatumia zaidi fursa na wamesambaa kila ukurasa mtandaoni. Hivyo, anza sasa usingoje kesho.

Mwandishi anapatikana kwa simu 0716186074