Messi aitaka Super Eagles Kombe la Dunia

Muktasari:

  • Winga huyo wa Argentina, alifunga mabao muhimu dhidi ya Ecuador katika mechi za kufuzu na kuipa tiketi ya Russia na kusema hamu yake wapangwe na Nigeria watakapokuwa Russia.

Staa wa Barcelona, Lionel Messi amesema hamu yake kubwa ni kupangwa Kundi moja na timu ya Taifa ya Nigeria, Super Eagles kwenye Fainali za Kombe la Dunia za 2018 nchini Russia

Winga huyo wa Argentina, alifunga mabao muhimu dhidi ya Ecuador katika mechi za kufuzu na kuipa tiketi ya Russia na kusema hamu yake wapangwe na Nigeria watakapokuwa Russia.

Messi alikaririwa na gazeti la National Helm la Argentina akisema, mechi dhidi ya Nigeria ni kati ya mechi bora kwake.

Amewahi kucheza dhidi ya Nigeria mwaka 2005 katika mashindano ya ubingwa wa dunia kwa vijana na mwaka 2008 kwenye Michezo ya Olimpiki ya Beijing na mara zote wameshinda.

Ukubwani sasa, ameshafunga mara tatu katika mechi walizocheza na Nigeria ikiwemo Kombe la Dunia Brazil na bao lingine walipocheza mechi ya kirafiki nchini Malaysia mwaka 2012.

“Alisema baada ya mchezo wake aliopiga hat-trick kwa Argentina dhidi ya Ecuador, na alipoulizwa kuhusu mechi anayopikumbuka ya Kombe la Dunia, alisema ni dhidi ya Serbia ambayo Argentina ilishinda mabao 6-0, na mechi ya Olimpiki ya Beijing walioshinda bao 1-0 dhidi ya Nigeria, na mechi dhidi ya Ecuador,” mwandishi wa Sky Sports’ Guillem Balague alisema.

Waliokata tiketi

Mataifa yaliyofuzu Kombe la Dunia kutoka Asia ni

Iran, Korea Kusini, Japan na Saudi Arabia wakati Afrika ni Misri na Nigeria.

Amerika Kaskazini Ukanda wa Concacaf ni Mexico, Costa Rica na Panama wakati Amerika Kusini ni Brazil, Uruguay, Argentina na Colombia.

Mataifa ya Ulaya yaliyokwisha kufuzu ni wenyeji Russia, Ufaransa, Ureno, Ujerumani, Serbia, Poland, England, Hispania, Ubelgiji na Iceland.