Mkenya apiga tatu La Liga

Muktasari:

  • Wakati Mkenya huyo akiweka historia, mabingwa wa Hispania wameendelea kuzama baada ya kufungwa bao 1-0 na Villareal, bao lililofungwa katika dakika ya nane na kuwafanya vigogo hao kuachwa kwa tofauti ya poiunti 19 na mahasimu wao wakubwa, Barcelona.

        Mshambuliaji wa kimataifa wa Kenya, Michael Olunga amekuwa Mkenya wa kwanza kufunga mabao matatu kwenye mechi moja ya Ligi Kuu ya Hispania alipoiongoza timu yake ya Girona kuichakaza La Palmas kwa mabao 6-0.

Wakati Mkenya huyo akiweka historia, mabingwa wa Hispania wameendelea kuzama baada ya kufungwa bao 1-0 na Villareal, bao lililofungwa katika dakika ya nane na kuwafanya vigogo hao kuachwa kwa tofauti ya poiunti 19 na mahasimu wao wakubwa, Barcelona.

Olunga alifunga mabao hayo ndani ya dakika 22 katika mechi iliyofanyika Uwanja wa Montilivi.

Mshambuliaji huyo ambaye anaichezea Girona kwa mkopo akitokea klabu ya Guizhou Zhicheng ya China, alifunga mabao hayo katika dakika za 57, 70 na 79 na kuw apia mchezaji wa kwanza wa Girona kufunga mabao matatu katika mechi moja ya Ligi Kuu ya Hispania, maarufu kama La Liga.

Ushindi huo pia ni mkubwa kwa Girona kwenye La Liga, ikiwa katika msimu wake wa kwanza katika daraja hilo na ushindi mkubwa iliowahi kuupata katika mashindano yote ndani ya miaka minne.

Bao lililofungwa kwa njia ya penati na Cristhian Stuani katikati ya kipindi cha kwanza ndio lilikuwa bao pekee katika kipindi hicho, lakini Girona ilicharuka katika kipindi cha pili na kufunga mabao hayo matano yanayoifanya La Palmas kupoteza mechi ya 14 kati ya 19 za ligi.

Mabao mengine yalifungwa na Borja Garcia na Cristian Portu.

Kilio kingine kilikuwa kwenye Uwanja wa Santiago Bernabeu ambako wageni, Villarreal walimuongezea presha kocha wa Real Madrid, Zinedine Zidane baada ya kushinda kwa bao 1-0.

Real ilifuzu kucheza robo fainali ya Kombe la Mfalme katikati ya wiki na itakutana na Leganes, lakini iliingia uwanjani juzi ikiwa nyuma ya Barcelona kwa tofauti ya pointi 16.

Na pengo hilom liliendelea kuwa kubwa baada ya Pablo Fornals kumalizia shambulizi la kushtukiza katika dakika ya 87 lililoanzishwa na Yellow Submarine.

Katika mechi nyingine, Atletico Madrid italazimika kumshukuru kipa Jan Oblak baada ya kuifikia Barcelona kwa pointi kutokana na ushindi wao wa bao 1-0 dhidi ya Eibar.

Bao pekee la wageni lilifungwa na Antoine Griezman katika dakika ya 27.

Katika mechi zilizochezwa usiku Jumamosi, Valencia ilishinda kwa mabao 2-1 dhidi ya Deportivo La Coruna na sasa inaizidi Real Madrid kwa tofauti ya pointi nane.