Mmea wa mchicha nafaka ni zaidi ya mboga

Muktasari:

Unaweza kulima mchicha huu kwa lengo la kuzalisha mbegu zinazotumika kama malighafi za bidhaa mbalimbali

Kama unafikiri majani ya mchicha ndicho chakula pekee, unakosea.

Mbegu zake zinaelezwa kuwa na virutubisho mbalimbali kwa ujenzi wa mwili wa binadamu.

Mtu anayetumia chakula kitokanacho na mbegu hizi, huwezi kumsikia akilalamika magonjwa ya aina mbalimbali wala maumivu; na yote ni kutokana na nguvu inayopatikana katika chakula hicho.

Taarifa njema kwa wajasiriamali

Mbegu hizi ni taarifa njema kwa wakulima nchini, kwa kuwa sasa wanaweza kulima mchicha siyo kwa minajili ya kuuza majani kama mboga, lakini pia kuuza mbegu.

Tangu mwaka 1995, mjasiriamali wa mkoani Dar es Salaam, Consolata Haule, amekuwa akijishughulisha na matumizi ya mbegu za mchicha nafaka kutengeneza bidhaa kama vile kashata, bisi, keki maandazi na bidhaa nyinginezo.

Amefungua kampuni maalumu iitwayo Jacoli inayojishughulisha na utengenezaji wa bidhaa zitokanazo na mbegu za mchicha.

Kwa mujibu wa Consolata ambaye zamani alikuwa ofisa lishe serikalini, kabla ya kustaafu, mbegu za mchicha zina uwezo wa kuwasaidia wagonjwa wa saratani zote, kisukari, shinikizo la damu, ukimwi, wazee, watoto, wajawazito na wanaonyonyesha.

Ili kuona kama zinaweza kufanya kazi, alilazimika kufanya majaribio kwa wagonjwa ambao walimpatia matokeo yanayotia moyo kuwa walipata nafuu

“Watu wenye sukari walikiri kuwa ilishuka na kuwa kawaida, presha ikashuka na wazee waliokua wana maumivu ya misuli na miguu walipoitumia, walisema wamepata nafuu huku watoto wakiweza kukaa hadi miezi sita bila kuugua,” anasema.

Inaendelea uk 28

Inatoka uk 27

Anasema baada ya sifa na maajabu waliyopata wagonjwa, wateja waliweza kuongezeka ndani ya muda mfupi jambo lililomfanya kuongeza uzalishaji.

“Kutoka kilo mbili nilianza kusaga kilo 20 za mbegu za mchicha ili niweze kukidhi mahitaji ya wateja,” anaongeza.

Anasema anajivunia kuwa mtu anayeboresha afya ya jamii kwa kuwapunguzia magonjwa, huku akitumia biashara hiyo kuongeza kipato yeye mwenyewe na wakulima kwa jumla. Anasema hivi sasa kwa mwezi anaweza kutengeneza kiasi cha Sh 700,000 hadi 1,000,000.

Tiba ya magonjwa mengi

Kwa mujibu wa taarifa ya kitaalamu iliyomo kwenye blogu ya mazingiranp,

mchicha nafaka una vitamin E sawa na mafuta ya mzeituni, huku mmea huo ukiwa na uwezo wa kutibu magonjwa kama kisukari, magonjwa ya moyo, maumivu ya magoti, maumivu ya vidonda vya koo (mdomoni), baridi yabisi, minyoo aina ya tegu, kansa ya tumbo, maziwa, koo, mapafu, kupunguza uzee, magonjwa ya ngozi

Mengine ni kuzuia meno kupata kutu, shinikizo la damu, kuzuia mwili kufa ganzi, udhaifu wa misuli, lehemu,

Atoa mafunzo

Mwaka 2005 alipatiwa mafunzo kutoka Shirika la Viwanda Vidogovidogo (SIDO) ya namna ya kuwafundisha wakulima faida za fursa zinazopatikana katika mchicha nafaka baada ya kuonekana ana uzoefu.

“Niliweza kutoa mafunzo katika maeneo ya Mbeya, Mufindi na Morogoro. Baada ya kuwafundisha wakulima waliomba niwe nanunua mbegu hizo ili wao wapate soko,” anasema na kuongeza:

“Kwa sasa wakulima wananufaika kwa sababu tangu mwaka 2010, kilo moja ya mbegu za mchicha imepanda hadi kufikia Sh5,000 kutoka 2,500 mwaka 1997 na hiyo ni baada ya wafanyabiashara wa Kenya kuanza kuzitafuta,” anasema.

Anasema kuongezeka kwa mikoa inayolima mbegu hizo kumepunguza changamoto ya upatikanaji wa malighafi kwa wafanyabiashara tofauti na hapo awali walipokuwa wakitegemea wilaya ya Same pekee kama mzalishaji mkuu.

Changamoto

Consolata anasema moja kati ya changamoto kubwa zinazomkwamish ni kukosa vibali kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Chakula na Dawa (TFDA() na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ambazo ni taasisi zinazohusika na utoaji wa vibali vya ubora wa bidhaa.

“Niliwahi kupata wateja kutoka nje, mmoja China na mwingine Uholanzi wakiwa na uhitaji wa bidhaa hizi, lakini walishindwa kuchukua kwa sababu sikuwa na nembo ya TBS,” anaeleza.

Anasema masharti yaliyowekwa na TFDA kwa wajasiriamali ni magumu na hawawezi kuyamudu kutokana na mitaji yao kuwa midogo.

“Wao wanataka eneo utakalotumia kutengeneza bidhaa lisitumike kwa shughuli nyingine, lakini hiyo ni ngumu na hata wakisema tukatengenezee SIDO bado ni vigumu,” anasema Consolata.

Ulimaji wa mbegu za mchicha

Anasema mbegu hizo hutumia miezi miwili hadi kukomaa tangu kupandwa, hulimwa kiangazi na baada ya kuvunwa hupepetwa na kusafishwa.

Ili mtu aweze kulima mchicha nafaka, lazima atayarishe shamba mwezi mmoja kabla ya kupanda na kuweka mbolea za asili zilizooza vizuri ili kuongeza rutuba ya udongo.

Mbolea hiyo hufanya udongo ushikamane vizuri na kuhifadhi unyevu kwa muda mrefu. Kiasi cha ndoo moja ya lita 20 ya mbolea kinatosha katika eneo la mita moja ya mraba na baada ya kumwaga, udongo ni lazima uchanganywe na mbolea hiyo.

Wiki mbili kabla ya kupanda, lainisha tena eneo shamba lako kwa kupigapiga mabonge makubwa na sawazisha.

Kuna aina mbili za upandaji mchicha huu. Aina ya kwanza ni kupanda moja kwa moja na nyingine ni kupandikiza miche.

Upandaji wa mbegu

Kumwaga mbegu: Mbegu hupandwa katika shamba la kudumu kwa kumwagwa baada ya kuchanganywa na mchanga ilio kiwango sawa na mbegu ili kuweka urahisi na kuepusha mbegu nyingi kukaa katika eneo moja.

Baada ya wiki mbili hadi tatu, mimea hupunguzwa na kuachwa mmoja mmoja kwa nafasi ya sentimita 15 hadi 23 na inaweza kupandwa katika sesa au matuta.

Lengo la kuacha sentimita hizo kati ya mmea mmoja na mwingine, ni kuipa nafasi ya kuchanua na kuzaliana kwa sababu miche hiyo huwa na matawi makubwa.

Kiasi cha kilo moja hadi mbili za mbegu kinatosha kuotesha katika eneo la hekta moja.

Kuotesha miche: Kupitia njia hii, miche huoteshwa katika kitalu kingine kabla ya kuhamishiwa katika shamba la kudumu.

Baada ya wiki mbili au tatu, miche hiyo hupandwa mmoja baada ya mwingine kwa kufuata mstari kwa upana ule wa awali katika shamba ambalo tayari limekwishaandaliwa mwezi mmoja kabla.