Mtunze mbuzi akutunze

Muktasari:

  • Unapofuga wanyama kama mbuzi, una uhakika wa kutengeneza mfumo imara wa kukuingiza kipato. Unaweza kufuga mbuzi kwa ajili ya maziwa au nyama.

Ufugaji wa wanyama kama mbuzi, kondoo, ng’ombe na wengineo, unalipa hasa ikiwa mfugaji atafuata kanuni na miongozo ya ufugaji kwa njia za kisasa.

Unapofuga wanyama kama mbuzi, una uhakika wa kutengeneza mfumo imara wa kukuingiza kipato. Unaweza kufuga mbuzi kwa ajili ya maziwa au nyama.

Lakini ili kujihakikishia una mfumo mzuri wa kuingiza kipato kupitia ufugaji wa mbuzi, matunzo ya wanyama hawa ni muhimu ili nao wawe na tija kwako kiuchumi. Makala haya yanaangazia baadhi ya vitu muhimu katika ufugaji wa mbuzi.

Ili kuwa na mbuzi wenye afya nzuri ni muhimu kuzingatia mambo yafuatayo:

Moja, chagua mbuzi ambao wanakabaliana na hali ya hewa na magonjwa kwenye ukanda wako. Hawa watahitaji matunzo kidogo ya kiafya.

Mbili, mbuzi ni lazima walishwe vizuri kulingana na mahitaji yao. Malisho bora na ya kutosha ni muhimu kwa

afya ya wanyama wote. Lishe hiyo ni lazima iwe ya kiasili kwa asilimia kubwa inavyowezekana.

Tatu, mbuzi wote wanahitaji kupata maji safi.

Nne, mfugaji lazima awe makini katika kupunguza kiasi cha minyoo, kwa kuweka banda la mbuzi katika hali

ya usafi. Hakikisha kuwa kihondi, matandiko na banda kwa ujumla ni safi na kavu wakati wote.

Tano, banda la mbuzi lazima liwe na sehemu ya malazi, mwanga, sehemu nzuri za kupitisha hewa na eneo la kutosha la kuzunguka. Ni lazima msongamano uepukwe.

Sita, mbuzi wanahitaji eneo la kutosha kuzunguka kwa uhuru. Mazoezi mfano kwenda machungani ni muhimu.

Saba, utunzaji wa mbarika: Ni rahisi sana mbarika kudhuriwa na wadudu na magonjwa. Dang’a (maziwa ya

awali) yanasaidia kulinda wanyama wadogo baada ya kuzaliwa katika wiki za mwanzo. Mbarika wanahitaji malazi, mazingira safi, maziwa ya kutosha, malisho mazuri ili kujijengea ulinzi wanapokua.

Nane, kukata kwato mara kwa mara na kutunza miguu ni muhimu kwa wanyama wote wanaocheua. Angalia kwato zote kabla na baada ya mvua na ukate kama ni lazima.

Tisa, kudhibiti wadudu. Udhibiti mzuri wa wadudu ni pamoja na ratiba nzuri ya kuchunga. Epuka eneo lenye tindiga na wape dawa ya minyoo mara kwa mara na kudhibiti kupe.

Kuchunga kijamaa kunaweza kuepukwa, vinginevyo kama jamii inafanya shughuli zao kwa karibu sana, ili kukabiliana na mazingira hatarishi.

Kumi, Chanja mbuzi wako kulingana na mapendekezo yanayotolewa katika ukanda wako ili kuepuka hasara

isiyo ya lazima. Chanjo hukinga wanyama vizuri kutokana na magonjwa ambayo kwa kawaida hayawezi kutibiwa.

Chunguza mbuzi wako

Kwa kiasi kikubwa, mbuzi husumbuliwa na wadudu na magonjwa sawa na kondoo na ng’ombe. Mbuzi huathiriwa zaidi na wadudu waliomo ardhini wakati wa kula. Pia, wanapata na kuathiriwa kirahisi na homa ya mapafu na kukohoa, hivyo kamwe wasiachwe kwenye mvua au nyumba isiyokuwa na nafasi ya kutosha, hewa na sehemu za wazi kupitisha hewa.

Dalili za kuumwa

Moja, mbuzi anakuwa amezubaa na asiyechangamka kama ilivyo kawaida, huwa na tahadhari, masikio na mkia

huanguka badala ya kuwa juu.

Mbili, hujitenga na wanyama wengine, na hajishughulishi na shughuli za wengine kama vile kula na kunywa, hupungua kwa kasi.

Tatu, Kinyesi kinakuwa si laini au unaweza kuona akiharisha.

Nne, mbuzi hukohoa, kutetemeka, au kupumua kwa haraka kuliko ilivyo kawaida.

Tano, mbuzi anakuwa na matongotongo au makamasi.

Sita, mbuzi hulala au kusimama katika mtindo ambao si wa kawaida.

Saba, manyoya kutokuwa katika mpangilio mzuri wa kawaida.

Nane, unaweza kugundua uvimbe au ugumu fulani mwilini mwake

Dalili za maumivu

Yafuatayo yatakuongoza kujua kama mbuzi wako ana maumivu; kulia, kuhangaika, kutafuna meno,

kutoa sauti kidogo au hafifu, hujigusagusa na kupiga mateke.

Tiba kwa mbuzi mgonjwa

Mnyama anayeumwa, lazima atibiwe mara moja. Kwa kawaida mbuzi huwa na msongo wanapoumwa na wanahitaji kusaidiwa haraka. Muone mtaalamu wa mifugo endapo una wasiwasi na anachoumwa mbuzi.

Mwache mbuzi mgonjwa apumzike kivulini, palipotulia na pasafi, na uhakikishe anapata maji na majani mabichi. Anaweza kupona haraka kama hatasumbuliwa.

Asilimia kubwa ya magonjwa na vifo vya mbuzi vinaweza kuzuilika.

Kwa maswali unaweza kuwasiliana na mtaalamu kwa simu: 0754 511 805

Makala haya ni kwa hisani ya mtandao wa mkulimambunifu. www.mkulimambunifu.org