NDANI YA BOKSI: Mkubwa Fella njoo tunywe kahawa...

Muktasari:

  • Kuna wanamuziki na wadau wa muziki ambao nalazimika kuwaheshimu kwenye hili game la Bongo Fleva. Walifanya mambo kwenye nafasi zao na kujenga himaya kubwa.

Muziki wa Bongo Fleva umepitia mengi sana. Kuna watu waliishia njiani na kuamua kufanya mengine. Wapo ambao wameamua kukomaa mpaka leo hii. Mungu awarehemu waliotangulia mbele za haki.

Inasikitisha kuna wengine muziki ulipita kushoto wao kulia na kuishi kubwia unga. Mjanja yeyote havuti unga. Lakini kila jambo lina sababu tusichoke kuwaombea warudi kwenye mstari.

Kuna wanamuziki na wadau wa muziki ambao nalazimika kuwaheshimu kwenye hili game la Bongo Fleva. Walifanya mambo kwenye nafasi zao na kujenga himaya kubwa.

FA. Akiwa kwenye ubora wake. Kwenye umaarufu wenye umaarufu wa kuzimiwa na totozi za mjini.

Akashindwa kuendekeza ‘hagi’ na mitego ya totozi. Akaangalia kesho yake. Akaamua kurudi darasani. Shule inamfanya awe FA unayemuona hii leo.

Ukitaka kujua linganisha kati yake na wengine. Elimu ilimfanya atafute njia ya namna ya kupambana na game linavyokwenda. Alijua kula na kipofu.

Fid Q. Hawa kina Darassa, Billinas na wenzao. Bila uwepo wa Fid Q wangekata tamaa. Kukomaa kwenye misingi yake na kuitwa Ngosha. Kulifanya hata Joh Makini aamini kuwa ‘any thing can happen’ (lolote lawezekana) kwenye hip hop. Fid alisimama mwenyewe katikati ya wimbi la muziki wa kuimbaimba kama ndio muziki bora. Akakomaa bila kujali kuwa Mchizi Mox, D Knob na kina Jaymoe wamesanda. Ndipo wakaibuka kina Young Killer na wenzake na kuona kuwa mbona inawezekana? Kumbuka kuwa watu kama kina Solo Thang waliimba mpaka Mduara. Wakaamua kukimbia nchi kwa kukwama ila Fid akakomaa.

JIDE. Moja kati ya wasichana ambao waliwafanya wasichana wajue kuwa kuna maisha nje ya kujiuza. Nje ya kupata digrii na nje ya ajira ya rushwa ya ngono. Uwepo wake na kukomaa kwake kuliwazalisha wengi mpaka kina Shilole. Snura. Linnah na wenzao.

Maisha ya Jide ni daraja moja na kina Shy-Rose Bhanji na wenzake ila yeye akaunti yake inatuna kwa sauti na tungo zake.

Bila yeye wengi wao wangeishia sehemu mbaya kimaisha ila muziki umewaondoa huku na kuwaweka sehemu moja na Ester Bulaya.

AY. Ni wanamuziki wa mwanzo kabisa ambao walianza kuupaisha muziki wa Bongo Fleva nje ya mipaka ya Tanzania.

Aliwateka Uganda na Kenya miaka mingi iliyopita. Wanamuziki wa mwanzo kabisa ambao walianza kuonesha njia ambazo wanapita kina Diamond kwa sasa.

Na zaidi ana akili ya biashara. Hategemei pesa za shoo tu ana miradi mingi kupitia muziki na wanamuziki.

ALI KIBA. Wakati Diamond anaanza ‘swaga’ zake yeye alikuwepo. Ila alikuwepo kama hayupo. Fujo za Diamond zilimuamsha na kufanya kitu kilichomfanya awe mpinzani wa Diamond.

Kitu kilichowashinda Q Chillah na wengineo kama kina Matonya na wenzake. Kiba aliamka akasimama. Leo hii Mwakyembe akimtaja Diamond lazima amhusishe na Ali Kiba. Si jambo dogo kushindana na Diamond mwenye Ruge, Fella, Babu Tale na Sallam. Waandishi na watangazaji kibao waliokuwa upande wa Diamond.

JOH MAKINI. Huyu Mweusi toka Kaskazini siyo mtu wa kumchukulia poa poa. Hata kama mdogo wake ila kuwa ‘role model’ wa msomi kama Nikki wa Pili siyo kitu kidogo. Nikki kusema hataki kazi ni kwa sababu ya uwepo wa kakaake kwenye game la muziki.

Kama Joh angekuwa kwenye hali kama ya wenzake wengi walioshindwa kuugeuza muziki kuwa pesa. Hata Nikki wa Pili asingethubutu kusema hataki kazi.

RUGE. Huyu kiumbe ngumu sana kumuongelea kwenye huu muziki. Aliufanya huu muziki. Rasta za wanamuziki. Kwato za wanamuziki na harufu za vikwapa za wanamuziki wa Bongo Fleva kufika kwenye viunga vya Ikulu ya Magogoni Dar es Salaam.

Ushawishi wake na kuitumia vyema Clouds FM, waliupandisha muziki huu na kutengeneza ajira kubwa sana kwa vijana wengi.

DIAMOND. Bado anaendelea kufanya miujiza yake. Miujiza iliyomshinda Mr Nice na wenzake. Kutoka Tandale ambako na mvua hii hakukaliki mpaka kupiga stori na kufanya kazi na NE-YO? Nahisi kuna mengi zaidi kutoka kwake. Tusubiri.

FELLA. Mkubwa Fella hakudandia treni kwa mbele kama wengi wanavyodhani. Ni mtu kati ya watu wanaohitaji heshima kwenye huu muziki.

Aliowasimamia wakasimama ni ushahidi kamili. Waliokwama kwa kukataa kusimamiwa naye pia ni ushahidi tosha.

Tofauti ya Fella na Sallam. Ni Sallam kumsukuma aliyejisukuma. Na Fella ni kugeuza karanga kuwa dhahabu. Yamoto Band inatosha.

Mae West anasema “Kuishi ni mara moja pekee, lakini ukifanya vema, mara moja yatosha”. Fella muziki unaudai haukudai. NI wakati wa kufurahia maisha. Njoo tunywe kahawa.

Sugu na Profesa Jay kuwaelezea wanahitaji WARAKA KAMA WA MTUME PAULO. Tuwaache kwanza.