Nahitaji darasa kuielewa orodha ya wasanii ‘bankable’

Muktasari:

  • Nimeisoma orodha ya wasanii kumi Afrika ambao ni ‘bankable’ kwa mujibu wa Forbes. Wamo Davido, Wizkid, Don Jazzy, Sarkodie, Hugh Masekela, Black Coffee, Don Jazzy, Tinashe, Jedanne na Oliver Mtukudzi.

Kwa mujibu wa kamusi niliyosoma neno ‘bankable’ ni kivumishi kinachomaanisha mtu au bidhaa fulani inafaa kwa uwekezaji kutokana na kile anachokifanya.

Kwa mfano ukiwekeza kwa Davido, Wizkid una uhakika kuwa fedha zako zitarudi kwa sababu ukichungulia mialiko wanayopata kwa mwaka mzima unaiona hela yako ikielekea benki na faida juu.

Nimeisoma orodha ya wasanii kumi Afrika ambao ni ‘bankable’ kwa mujibu wa Forbes. Wamo Davido, Wizkid, Don Jazzy, Sarkodie, Hugh Masekela, Black Coffee, Don Jazzy, Tinashe, Jedanne na Oliver Mtukudzi.

Orodha hii ina majina ambayo yanaleta sintofahamu. Huenda kuna vigezo vimatumika kuipata orodha hii lakini wengine wanatafsiri kama hawa ndio wasanii matajiri Afrika.

Nakubali kwamba Akon ni Mwafrika. Nakubali kwamba ni mwanamuziki mzuri. Nakubali kwamba kutokana na uzuri wa kazi zake anauzika na anastahili kuwa bilionea.

Nakubali kwamba anastahili kuwa bilionea kwa sababu yupo katika nchi ya fursa. Akitoa wimbo mmoja tu na robo ya raia wa nchi yake wakaununua kwenye mitandao na kuutazama Vevo au Youtube atapata pesa nyingi kuliko mwanamuziki wa Bongo atakayoipata atakapozunguka nchi nzima kufanya matamasha.

Akon ni Mwafrika aliyebahatika kuzaliwa Marekani na shughuli zake za muziki anafanyia kule. Ni tofauti na Sarkodie aliyezaliwa Ghana au Diamond aliyekulia Tandale. Hawa wakienda Marekani wanakwenda kuwaburudisha Waafrika wenzao.

Siku zote hapa tunasema wanakwenda kufanya shoo sebuleni sijui nini wakati Akon katika nchi hiyo hiyo anaweza kufanya shoo ya peke yake ya watu 60,000.

Ninahitaji maelezo zaidi kujua Don Jazzy anaingiaje katika orodha hii. Huenda maelezo yalipaswa kuwa marefu kidogo kwamba utajiri huu kaupata kwa kuwasimamia kina Tiwa Savage na Ricado Banks au biashara nyingine.

Namuona Don Jazzy kama mfanyabiashara wa muziki  na si mwanamuziki. Hata utajiri anaotajwa kuwa nao hakuupata kwa kushika maiki. Ni mwekezaji katika muziki ambaye naye mara moja moja anafanya muziki.

Naona si sahihi kumshindanisha mtu anayefanya biashara ya muziki na mwanamuziki. Wengine wanajituma jukwaani, wanakata viuno halafu wanashindanishwa na mtu anayeimba kujifurahisha si sahihi. Diamond na Don Jazzy ni watu wawili wanaounganishwa na uwekezaji katika muziki lakini Diamond ni mwanamuziki hodari kuliko Don Jazzy.

Sitaki kumzungumzia Jedanne  na Tinashe walioingia katika orodha hii kwa sababu nachanganyikiwa ziaidi.