Nay wa Mitego: Siwezi kurudiana na Siwema, Skiner wala Shamsa

Nay wa Mitego

Muktasari:

Nay alisema iwapo itatokea nafasi kwa yeye kurudiana na mmoja kati yao, atampa nafasi mwanamke aliyezaa naye mtoto wake wa kwanza.

Dar es Salaam. Rapa wa muziki wa kizazi kipya nchini, Nay wa Mitego amesema hana ndoto za kurudiana na mwanamke yeyote kati ya aliwaowahi kuwa nao katika uhusiano wa mapenzi.

Nay alisema iwapo itatokea nafasi kwa yeye kurudiana na mmoja kati yao, atampa nafasi mwanamke aliyezaa naye mtoto wake wa kwanza.

Alisema kwa sasa hana mapenzi na yeyote kati yao, kwa sababu amekuwa akilea watoto wake kwa muda mrefu, hivyo hadhani kuna kitu kinachoweza kumvutia tena kwa wapenzi wake hao.

“Hamna hata mmoja ambaye ninaweza kurudiana naye, labda yule ambaye nilizaa naye mtoto wa kwanza japokuwa yeye alishaolewa, huwa napenda kumwita Mama Vishma maana mtoto wangu wa kwanza anaitwa jina hilo,” anasema Nay wa Mitego.

Nay anasema hana sababu ya kuwasogeza mama wa watoto wake karibu tena, kwani kukaa karibu na watoto hao kummemfanya ajifunze mengi katika malezi.

Anasema japokuwa wengi bado wanashangaa kwa jinsi anavvyomudu maisha bila mama zao, kwake anafaidi mengi ikiwamo kupata baraka katika kazi zake anazoamini zinatokana na watoto.

“Wazazi wa kiume wengi hawapo karibu na watoto hawajengi mazoea mazuri na hata mtoto anakosa upendo kwao, nimejifunza ukiwa nao karibu kuna baraka hata Mungu akiangalia upendo ulionao kwa watoto wako anakupa riziki zaidi,” anasema Nay.

Mkali huyo wa wimbo “Saka Hela” ambaye wimbo wake “Pale Kati” ulifungiwa na Basata baada ya kuonekana hauna maadili, amesema kwa sasa anajipanga ili atakaporudi kwa mara nyingine awe amebadilika zaidi.

Anasema licha ya kudaiwa amekuwa akiimba nyimbo zisizo na maadili, amejipanga atakaporudi kwa mara nyingine.

“Siwezi kufanya muziki wa kuvunja maadili kwa makusudi hakuna mtu ambaye anacheza na kazi yake, huwezi kubadilisha aina ya muziki, lakini nitawashirikisha zaidi wao ili yasitokee haya yaliyotokea,” anasisitiza.