Ninaifanya Kenya daraja la kuvuka kucheza kimataifa

Muktasari:

  • Kilichosemwa na kufanikishwa na Howard kinaendana na kile ambacho amekiazimia beki na kati wa zamani wa Majimaji ya Songea, Tumba Lui (26) ambaye amejiunga na Wazito F.C ya Kenya kwa makataba wa miaka miwili.

Kipa wa zamani wa Everton ya England, Timothy Matthew Howard ‘Tim Howard’ (38) ambaye anaichezea Colorado Rapids ya nyumbani kwao, Marekani aliwahi kusema kuwa ilikuwa ni ndoto yake kuwa mchezaji wa daraja la juu.

Kilichosemwa na kufanikishwa na Howard kinaendana na kile ambacho amekiazimia beki na kati wa zamani wa Majimaji ya Songea, Tumba Lui (26) ambaye amejiunga na Wazito F.C ya Kenya kwa makataba wa miaka miwili.

Wazito F.C ya Nairobi ambayo ipo chini ya kocha wao mkuu, Frank Ouna inashiriki Ligi Kuu Kenya msimu huu wa 2018/2019 kutokana na kupanda kwao daraja mwaka jana.

Leo katika mfululizo wa Makala zetu za ufuatiliaji, uvumbuzi wa wachezaji wa Kitanzania wanaocheza nje, tunaye beki huyo mwenye ndoto pia ya kuitumikia Taifa Stars.

“Wakati naanza kucheza mpira wa mtaani, nilipenda sana siku moja kuja kuwa mchezaji wa kimataifa kwa kupata nafasi ya kucheza nje ya nchi, sijawahi kukata tamaa kwa hata kuwaza kuachana na soka.

“Majimaji imekuwa sehemu ya kupiga kwangu hatua kwa kuonekana, unaweza ukajiulizaje ni kwa namna gani? Kwa sababu hatujashiriki mashindano yoyote ya kimataifa.

“Nilipokuwa nacheza Ligi Kuu Bara na Majimaji kumbe kulikuwa na kocha wa Wazito alikuwa anafuatilia mwenendo wangu kwa kipindi kirefu,” anasema beki huyo.

Anaendelea; “Safari hii ambayo wamenisajili, kocha alikuja maana tayari ilikuwa ameshaipandisha Wazito daraja na kuamua kufanya mawasiliano ya haraka ili kuona kama kuna uwezekano wa kunisajili.

“Sikuona kama kunatatizo la kufanya uamuzi kwa upande wangu kwa sababu niliona huo unaweza kuwa mwanzo wa kupiga hatua zaidi, mwanzoni kupata nafasi ya kucheza ligi kuu niliona ni hatua ya kwanza.”

Tumba anadai kuwa alifanya makubalino na Majimaji ili apate ruhusa ya kwenda kufungua ukurasa wake mpya wa utafutaji wa mafanikio upande wa soka la kimataifa.

“Japo haikuwa rahisi lakini nilipata barua ya kuniruhusu kujiunga na Wazito ambao nimeingia nao mkataba wa miaka miwili, na ninatarajia kuitumia Ligi Kuu Kenya kama daraja la kuvukia na kusonga mbele kama ilivyokuwa Majimaji.

Hata hivyo, Tumba hakuficha shauku aliyonayo ya kuichezea timu ya Taifa chini ya Salum Mayanga.

“Hakuna kitu ambacho nitaweza kujivunia kama kuwa shujaa kwa Taifa langu, unaweza kuwa shujaa ndani ya klabu fulani lakini ule uthamani wake ukawa mdogo.

“Taifa linaweza kuwakumbuka mashujaa wake.Nitakapo hitajika siwezi kusita kuja kuipigania Tanzania,nimelelewa na kukulia hapa kwa hiyo siwezi kuwa na chaguo la kuchezea Taifa lingine”anasema.

Anaendelea: “Matarajio yangu Kenya ni ushindani, nasikia kuna Watanzania wenzangu kule ambao wanacheza ligi hivyo sidhani kama nitakuwa mpweke.

Bado nipo Afrika Mashariki kwa hiyo siwezi kupata shida kwenye mazungumzo, vyakula na utamaduni mwingine, karibu nchi zote za Afrika Mashariki tunaingiliana kwenye mambo mbalimbali.”

Nyota wengine wa Kitanzania wanaocheza Ligi Kuu Kenya ni Abdul Hilal (Tusker), Aman Kyatta (Chemelil Sugar),Hamis Abdallah (SoNY Sugar) na David Naftar anayekipiga Nakumatt.

Katika mazungumzo hayo na Spoti Mikiki, Tumba hakuacha kutoa meneno yake kwa viongozi wa Majimaji, wachezaji na mashabiki wa timu hiyo ambao wamekuwa naye pamoja pindi akiichezea timu hiyo.

“Ninawashukuru sana viongozi na wachezaji wenzangu kwa nyakati mbaya na nzuri ambazo tumekuwa pamoja, nilijituma kuichezea Majimaji kwa nguvu na akiri zangu zote. Ninawatakia mwenendo mzuri kwenye ligi,” anasema.

Utekelezaji wa alichokisema Howard katika kuhitaji kuwa mchezaji wa daraja la juu, ulianza mwaka, 1997 kwa kuicheze North Jersey Imperials mara baada ya kulelewa na Central Jersey Cosmos.

Dhamira yake ya kweli miaka kadhaa baadaye ilimfanya kuwa mchezaji wa daraja la juu kwa kuichezea hata Manchester United kuanzia mwaka 2003 hadi 2007 na baadaye kuhamia Everton.

Howard mwenye miaka 38 soka lake limefikia ukingoni lakini Tumba ana nafasi ya kuendelea kupigania ndoto yake ya kuhitaji kuwa mchezaji wa daraja la juu.