P4R; mpango uliobadilisha maisha ya wanafunzi Ukerewe

Makamu Mkuu wa Shule ya Sekondari Pius Msekwa iliyopo Ukerewe, Ally Yusuf akionyesha majengo ya vyoo vya kisasa, yaliyojengwa shuleni hapo.Na Mpigapicha Wetu

Muktasari:

Ni kwa sababu hii jitihada mbalimbali zimekuwa zikifanyika ili kuifanya Tanzania kuwa nchi ya watu walioelimika. Katika jitihada hizo, upo mpango uitwao;: Lipa kulingana na Matokeo au kwa Kiingereza , Program for Results (P4R).

Elimu ni ufunguo wa maisha; Elimu ni bahari haina mwisho. Misemo hii inadhihirisha kuwa, ili binadamu aweze kuendesha maisha yake katika misingi inayokubalika, lazima awe ameelimika.

Ni kwa sababu hii jitihada mbalimbali zimekuwa zikifanyika ili kuifanya Tanzania kuwa nchi ya watu walioelimika. Katika jitihada hizo, upo mpango uitwao;: Lipa kulingana na Matokeo au kwa Kiingereza , Program for Results (P4R).

Huu ni mfumo mpya wa kufadhili sekta ya elimu ambao unatumiwa na Benki ya Dunia (WB), Idara ya Maendeleo ya Kimataifa (DFID) na Wakala wa Maendeleo ya Kimataifa Sweden (SIDA).

Kupitia mfumo huu, fedha hutolewa kwa kukidhi vigezo vilivyokubalika baada ya kufanyiwa uhakiki na kuthibitika utekelezaji wake umefikiwa.

Huu pia ni mfumo wa ufuatiliaji ambao unahakikisha kuwa vipaumbele vya sekta ya elimu vinatekelezwa kwa kuzingatia mipango na bajeti iliyoidhinishwa na Bunge kwa mwaka husika.

Fedha zilizopatikana kupitia programu hii hutumika katika kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia. Kupitia programu hii Wizara imendelea kushirikiana na Tamisemi katika kuratibu uboreshaji wa miundombinu ya shule za msingi na sekondari.

Umekuwa ukitoa ruzuku kwa ajili ya ujenzi wa madarasa, vyoo, mabweni, mabwalo, ofisi za walimu, uzio wa shule, visima, maktaba na maabara katika shule mbalimbali za umma zenye mahitaji makubwa pamoja na ukarabati wa miundombinu mingine chakavu katika shule hizo.

Hadi sasa ujenzi na ukarabati wa jumla ya madarasa 1,405, matundu ya vyoo 3,394, ofisi za walimu sita, mabweni 261, mabwalo tisa, nyumba za walimu 11, majengo ya utawala katika shule 13, maabara 3, uwekaji wa uzio katika shule 4, maktaba 2 na uwekaji wa umeme katika shule 2 upo katika hatua mbalimbali na hadi sasa halmashauri 129 zimenufaika kupitia mpango huu.

Ukerewe ilivyonufaika

Miongoni mwa halmshauri zilizonufaika ni pamoja na halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe iliyopo mkoani Mwanza ambapo Mkurugenzi wa Wilaya hiyo Frank Bahati anasema wilaya yake awali ilikuwa na shule za kidato cha kwanza mpaka cha nne kwa muda mrefu, lakini baada ya kupata fedha za P4R, halmashauri hiyo imeweza kujenga vyumba vya madarasa, mabweni kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha tano.

“Tulianza na miundombinu michache lakini Serikali ilisikia kilio chetu na tunaishukuru kwa kutambua umuhimu wa kuanzisha kidato cha tano wilayani humu, kwani tulikuwa na shule za kidato cha kwanza na nne tu, lakini sasa tuna kidato cha tano na sita. Aidha, wanafunzi wanakaa hapahapa shuleni kwa kuwa tayari tuna mabweni” anasema.

Bahati anasema wilaya yake imepatiwa kiasi cha fedha Sh518 milioni kutoka P4R ambazo zimeshatumika katika ujenzi na ukarabati wa miundombinu mbalimbali ya shule za sekondari za Pius Msekwa na Bukongo zilizoanzisha mchepuo wa kidato cha Tano.

“Katika shule hizi mbili tumejenga mabweni mawili mawili, vyumba vya madarasa vinne, matundu ya vyoo 10 na ukarabati wa maabara katika shule. Katika shule ya Pius Msekwa wameongeza maabara ya Fizikia kwa ajili ya kidato cha tano na sita,’’ anasema na kuongeza:

‘’Ujenzi huo wa mabweni utawezesha wanafunzi wa kidato cha tano na sita kukaa na kusoma katika mazingira ya shuleni na kupunguza mwendo mrefu wanaotembea wanafunzi na kuacha kujiingiza katika makundi mbaya.’’

Wasaidia tatizo la mimba

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe Estomih Chang’ah, anasema programu ya P4R ni mkombozi kwa wananchi wa Ukerewe, kwani pamoja na kuwezesha kuwa na madarasa ya kidato cha tano na sita, lakini pia umeweza kusaidia katika mikakati ya kupunguza na kuondoa tatizo la mimba shuleni.

“Programu hii kwangu naona ilikuja kwa wakati mwafaka kwani imeweza kuifanya wilaya hii kwa mara ya kwanza kuwa na masomo ya kidato cha tano, lakini pia kuondoa tatizo la mimba kwani wanafunzi wote waliokuwa wanapanga mitaani watapata nafasi ya kukaa mabwenini,” anasema.

Oliva Kato ni Ofisa habari mwandamizi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.