SAIKOLOJIA : Fahamu aina za wanaume ambao wanawake wanawataka

Muktasari:

  • Lakini nilipowauliza kama kuna tofauti kati ya hisia za wanaume wa zamani kwa wanawake na za wanaume wa leo zaidi ya nusu walikiri kuwa kuna mabadiliko chanya.
  • Kila ninapoandika kuhusu mahusiano katika ndoa kati ya mume na mke huwa nakumbuka kisa cha Rais mmoja wa nchi ya Kiafrika aliyeandaliwa karamu na Malkia Elizabeth wa Uingereza alipoitembelea nchi hiyo.

Kuna wakati nilijaribu kuwauliza wanawake kadhaa walioolewa kama wamefanikiwa katika ndoa kupata aina ya wanaume waliokuwa wametarajia. Wengi walikuwa wanasita kunipatia jibu la moja kwa moja kama ndiyo au hapana.

Lakini nilipowauliza kama kuna tofauti kati ya hisia za wanaume wa zamani kwa wanawake na za wanaume wa leo zaidi ya nusu walikiri kuwa kuna mabadiliko chanya.

Kila ninapoandika kuhusu mahusiano katika ndoa kati ya mume na mke huwa nakumbuka kisa cha Rais mmoja wa nchi ya Kiafrika aliyeandaliwa karamu na Malkia Elizabeth wa Uingereza alipoitembelea nchi hiyo.

Rais huyo aliyekuwa amefuatana na mkewe alipoingia katika ukumbi ulioandaliwa karamu alishangazwa na idadi kubwa ya vyombo vya kutumia kwa kulia chakula vilivyokuwa vimepangwa mezani kwa ajili ya kila mtu.

Kwa bahati yeye aliwahi kuishi Uingereza kwa miaka kadhaa alipokuwa masomoni, lakini alikuwa na wasiwasi kuwa huenda mkewe hatajua namna sahihi ya kukitumia kila chombo; hasa kwa sababu vilikuwa vya aina nyingi kuliko vile ambavyo huwa wakiandalia wageni katika Ikulu ya nchini kwao.

Alichanganyikiwa zaidi alipogundua kuwa mkewe hakupangwa karibu naye ili walau awe akimsaidia kwa kumwelekeza kwa ishara. Alihangaika katika nafsi yake afanye nini ili kumuepusha mkewe na fedheha.

Hata hivyo, baada ya hotuba za makaribisho kabla hawajaanza kula alimweleza malkia kuwa wao wana desturi ya kimila ambayo huwa hawathubutu kuivunja. Lazima waombe kwa lugha yao ndipo yeye na wenzake waweze kula. Aliporuhusiwa akijifanya kama anaomba dua, lakini alikuwa akimwelekeza mkewe jinsi ya kutumia baadhi ya vyombo vilivyoandaliwa pale mezani ambavyo alihisi alikuwa hajawahi kuvitumia. Kila alipokuwa akikamilisha sentensi ukumbi wote uliungana na wageni katika kuitikia Amina.

Baada ya karamu wageni walipokuwa peke yao walimpongeza rais wao kwa ujasiri aliouonyesha kwa ajili ya heshima ya mkewe. Mmoja katika viongozi wa kike aliyekuwa katika msafara akasema: “Hiki kilichotokea ni dalili kuwa sasa yule aina ya mwanaume ambaye sisi wanawake tulimtarajia kwa muda mrefu ameanza kutokea.” Wanume wakacheka sana kwa mzaha ule. Labda nianze makala yangu hii kwa kuanzia na usemi wa yule kiongozi wa kike aliyekuwa katika msafara huo. Kufuatia harakati za wanawake za miaka mingi kugombea haki sawa, mwanaume wa kisasa amebadilika kwa kiasi kikubwa.

Hivi leo mwanaume amekuwa mwenye hisia ya upendo, mtunzaji, mwelewa na mwenye kumjali mwenzi wake katika ndoa kwa kiasi ambacho hata wanawake hawakuwahi kufikiria.

Wanaume wengi siku hizi wanapowafikiria wenzi wao katika ndoa wanahoji usahihi wa fikira walizokuwa nazo mababu zetu kuhusu hadhi ya mwanamke katika jamii na falsafa iliyotumika katika kumuenzi zaidi mtoto wa kiume na kumuweka nyuma wa kike. Siku moja nilipokuwa nikisikiliza mazungumzo ya wanaume wanaotoka kwenye makabila yaliyokuwa yakiongoza katika mila za kuwaweka wanawake nyuma, niliamini kuwa sasa wanaume wamebadilika. Walisema: “Sisi wanaume wa siku hizi tunakabiliwa na shinikizo la hoja za usawa wa kijinsia ambalo ingawa linapingana na mila zetu hatuna budi kupima kama zina mashiko katika maisha ya sasa ambayo ni tofauti sana na yale ya zamani.”

Walikiri kuwa katika ulimwengu wa sasa ambapo mume na mwanamke wanafanya kazi, ni lazima mwanaume awe tofauti na babu zetu. Ingawa bado mwanaume anastahili kuwa na mamlaka katika kaya, lakini mamlaka hayo hayastahili kuwa na mwelekeo wa kumnyanyasa mwenzi wake katika kuijenga familia yao. Aidha, ni kweli kuwa mwanaume anapaswa kufanya juhudi kubwa ili kupata ufanisi mkubwa katika kazi kwa manufaa ya familia, lakini ni lazima ahakikishe anapata muda wa kuwa na familia yake na kuijali kwa kila hali.

Mwanamke wa leo anawajibika kujijengea siyo tu uwezo wa kuilea familia yake, bali pia kujenga haiba na hadhi yake katika jamii na kupanda ngazi za juu katika kazi yake na pengine hata juu kuliko wanaume.

Mwanamume akumbuke kuwa licha ya kumsaidia mkewe katika shughuli za familia, yeye ndiye mwenye jukumu la kumsaidia kufanikisha ndoto zake za kutukuka katika jamii na katika kazi yake. Wanawake wamekuwa wakitekeleza jukumu hili kwa waume zao kwa miaka mingi. Hata kuna methali ya kiingereza isemayo “The road to success if full of women pushing their husbands in wheelbarrows” Yaani njia ya kuelekea kwenye ufanisi imejaa wanawake wanaowasukuma waume zao katika matoroli.”

Kitendo alichofanya Rais wa Marekani anayemalizia kipindi chake cha utawala, Barack Obama ni ushuhuda tosha wa methali hii ya kiingereza niliyoitaja. Katika hotuba yake ya kuwaaga Wamarekani iliyorushwa kwa televisheni kote ulimwenguni alimshukuru mkewe, Michelle Obama kwa msaada aliompatia katika kuliongoza taifa la Marekani kwa kipindi cha miaka minane. Alipokuwa akitamka hizo shukrani alimtazama mkewe na akatokwa na machozi na kuchukua kitambaa mfukoni kujifuta.

Wanaume wa kisasa, kama alivyo Obama wamejifunza kuwa mwanamke wa leo sio tena yule wa zamani ambaye alifikiriwa kama mama wa nyumbani tu asiye na mchango wowote katika maendeleo ya ulimwengu huu yanayokwenda kwa mwendo wa kasi hata kuliko saa.

Aidha, ninapokaribia mwisho wa makala hii naona sina budi kuwaasa wanawake kuwa kwa kiwango kikubwa wanaume wa kisasa walio wa kweli wamebadilisha hisia zao kuhusu nafasi ya mwanamke katika jamii. Vilevile wapo walio katika hatua mbalimbali za kuekea kwenye mageuzi yanayotarajiwa.