Sababu ya Dk Masanja kuanzisha chuo cha kilimo

Muktasari:

Uzoefu unaonyesha ili ujihakikishie wanafunzi wa kutosha unapofungua chuo nchini, huna budi kutoa kozi kama kompyuta, uhasibu, afya, uandishi wa habari, utawala na nyinginezo.

Wakati mtazamo wa wawekezaji wengi katika sekta ya elimu ukiwa ni kufungua shule au taasisi zinazotoa kozi ambazo kwa wengi ni kozi zinazolipa, wapo wenye mtazamo tofauti.

Uzoefu unaonyesha ili ujihakikishie wanafunzi wa kutosha unapofungua chuo nchini, huna budi kutoa kozi kama kompyuta, uhasibu, afya, uandishi wa habari, utawala na nyinginezo. Huko ndipo walipowekeza wawekezaji wengi binafsi.

Hata hivyo, kuna wawekezaji wachache wanaoona fursa kwenye sekta ya kilimo. Miongoni mwao ni Dk Aloyce Masanja aliyeamua kuanzisha chuo cha masuala ya kilimo na ufugaji.

Kwa muda mrefu Serikali ndiyo imekuwa mwekezaji pekee kwenye sekta hiyo, lakini sasa nguvu imeongezeka kwa kuwapo taasisi binafsi kikiwamo chuo hiki.

Dk Masanja ambaye pia ni Mkurugenzi wa Chuo kijulikanacho kwa jina la Canre, anasema haikuwa kazi rahisi kuwavutia wanafunzi kusoma kozi za kilimo lakini sasa mwitikio umekuwa mkubwa.

Chuo hicho kilichopo Bonyokwa, Segerea jijini Dar es Salaam, kilianzishwa mwaka 2006 huku kikiwa na wanafunzi wawili, lakini sasa kina zaidi ya wanafunzi 600.

“Mwitikio ulikuwa mdogo sana kwa wanafunzi kusomea masomo ya kilimo; kuna wakati nilikuwa najiuliza hivi mimi nitaweza kweli mana niliona kama masomo haya ya kilimo hayapendwi hata hivyo sikukaata tama,”anasema.

Anasema baada ya chuo hicho kusajiliwa mwaka 2010 wanafunzi waliongezeka huku mwitikio kwa wasichana kusomea kilimo ukiwa mdogo.

“Lakini sasa hivi naona vijana wanaongezaka na kwa mtazamo huu natarajia kuona wataalamu wengi wa kilimo wanatoka hapa na kwenda kukomboa wananchi katika masuala ya kilimo na ufugaji,”anaongeza.

Kilichomsukuma kuanzisha chuo cha kilimo

Anasema wazo la kuanzisha chuo cha kilimo lilikuja baada ya kuona sekta ya kilimo haina maendeleo ya kuridhisha kwa maana kwamba watu wengi wanaikimbia na hata waliokuwa wakilima na kufuga, hawakufanya kitaalamu.

Anasema kilimo ni uti mgongo lakini hakiwezi kuwa na tija kama hakutakuwa na wataalamu wa kutosha watakoashauri wakulima hasa katika maeneo ya vijijini.

Kabla ya hapo alikuwa na utaratibu wa kwenda kutembelea nchi mbalimbali kuona maeneo gani yanakwamisha Watanzania wenye nia ya kufanya kilimo na ufugaji.

“Mfano nilipokwenda Japani nilikuta watu wanalima tena kwa kutumia enao dogo tu lakini wanavuna mazao mengi, nikasema kwani sisi Tanzania tunashindwaje?

Nikaweka nia kwamba lazima niikomboe nchi yangu katika masuala ya kilimo,”anasema.

Anasema pia kilichomvuta kuanza chuo hicho ni kwamba alizaliwa kwenye familia ya wakulima hivyo kuanzia elimu ya msingi, sekondari hadi chuo alijikita zaidi katika masomo ya kilimo.

“Nimefikiria sana nikaona hapa nchini vyuo vingi vya binafsi ni vya fani nyigine nikaona kwa nini nisianzishe chuo cha kilimo ili kuongeza nguvu kile cha Serikali tuweze kuzalisha wataalamu wa kutosha,” anasema.

Anasema alichokiona ni kwamba jamii inashindwa kutambua kuwa kilimo ni sehemu ya ajira. Wapo wanaolima zao la aina moja tu wakidhani kwamba mazao mangine hayana faida.

“Sasa hivi kilimo ni biashara, nchi za wenzetu wanafanya kilimo hadi cha maua lakini kinalipa lakini kwa Tanzania mtu anaona maua ni kwa ajili ya kupendezesha nyumba yake tu lakini kumbe maua ni mtaji,”anasema.

Alivyoanzisha chuo hicho

Kwa kuwa alikuwa mwajiriwa katika Wizara ya Kilimo kwa miaka 20, hakutaka kupoteza ujuzi wake hivyo wazo la kuanzisha chuo hicho likaanzia hapo.

“Katika eneo hili kulikuwa pori kubwa kwa bahati nzuri nilikuwa nalima mahindi, migomba, nilikuwa pia nafuga kuku na samaki nikaona ni vyema nianzishe chuo cha kilimo na ufugaji,”anasema Dk Masanja.

Hata alipokuwa masomoni nje ya nchi akichukua Shahada ya Uzamivu, aalijikita kwenye masuala ya kilimo na ufugaji, lengo likiwa kuja kuisaidia jamii nchini baada ya kuona haijahamasika katika sekta hiyo.

“Basi baada ya hapo nilianza na wanafunzi wawili na walimu wawili nilienda nao hivyo hivyo japo mwanzo ulikuwa mgumu lakini sikukata tamaa na safari yangu ya kuwakomboa wakulima,”anasema.

Kwa nini watu wanakimbia kilimo?

Dk Massanja anasema: “Nilichokiona hapa ni mtazamo wa wengi kufikiria kwamba kiilimo ni cha wazee na hata ukiangalia asilimia kubwa watu wanaishi kijijini kwa hiyo huku mjini mtu anaona kilimo hakina tija.’’

Kutokana na zana zinazotumika kutokuwa za kisasa ndiyo maana wengi wanasema kilimo hakilipi.

“Mkulima anatakiwa kujua kilimo kina maana gani kwake, wengi wanalima kimazoea na wengi wanashindwa kwa sababu hawajapata elimu ya kutosha kilimo kina maana kubwa sana ndani ya jamii,”anasema.

Anasema uwepo wa vyuo vya kilimo nchini utakiongezea tija kilimo kwani ni wachache wenye mwamko na kutambua umuhimu wa kilimo, hivyo ni vyema Serikali ikaongeza juhudi ikiwemo kuongeza sehemu za mafunzo.

“Lakini pia hata sera ya Serikali ya kilimo ya mwaka 2013 mimi nilivyoiona imetoa mwelekeo mzuri na imegusa karibu maeneo yote muhimu, kwa hiyo sasa hivi watu wameanza kupata ufahamu kuwa kilimo sio kwa ajili ya chakula tu bali kilimo ni biashara,”anaongeza.

Changamoto

Dk Masanja anasema tangu ameanzisha chuo hicho amepitia changamoto mbalimbali ambazo kama sio ujasiri wake zingeweza kumkatisha tamaa na kurudisha nyuma malengo yake ya kukomboa wakulima.

Moja ya changamoto hizo ni kutoaminiwa na taasisi za kifedha wakati wa kuomba mkopo, kwani anasema kutokana na chuo hicho kuwa na wanafunzi wachache walihisi asingeweza kulipa.

Changamoto nyingine ni kutoungwa mkono na Serikali.

Anasema mbali na chuo hicho ni kuiinua sekta ya kilimo kwa kuzalisha wataalamu wa kilimo, lakini bado Serikali haiungi mkono juhudi zao.

“Mimi sikufichi nimetoa zaidi ya wanafunzi 2000 tangu naanzisha hiki chuo, lakini hakuna hata kiongozi mmoja aliyekuja kuona wala kuangalia ninachokifanya. Ningefarijika pengine hata masuala ya kodi wangenipunguzia,” anaeleza

Anasema suala la kodi lina mtesa kwani wakati mwingine hadi vifaa anavyopatiwa kama msaada analazimika kuvilipia kodi.

Mbali na changamoto hizo anasema kwa kuwa amedhamiria kuwa mkombozi wa kilimo na ufugaji. Anasema mbali na kutoa elimu kwa ngazi ya astashahada na stashahada, ana lengo la kuanzisha chuo kikuu.

“Mimi sitoishia hapa, nitaenda mbali zaidi kwa kuanzisha shahada ya kilimo na mifugo na tayari eneo nimeshalitenga kwa ajili hiyo,”anasema.

Mafanikio yake

Masanja anajivunia kuona wanafunzi waliotoka chuoni kwake wakiajiriwa katika halmasahauri mbalimbali wakitoa huduma ya masuala ya kilimo kwa Watanzania.

“Hayo ndiyo mafanikio yangu mimi, siwezi kujivunia nyumba wala mali nilizonazo kwa kuwa lengo langu ni kutoa elimu ya kilimo kwa vijana kwa hiyo najivunia kupiga hatua kubwa,” anasema.