Sailo teknolojia bora ya kuhifadhi nafaka

Huu ndio mwonekano wa maghala ya kisasa yaitwayo sailo yanayoweza kutumika kuhifadhia mazao ya nafaka na yale ya jamii ya mikunde. Picha na mtandao

Muktasari:

Wakati wote wamenawiri kuliko hata wakulima hutumia nguvu kubwa kulima kwa ajili yao wanawiri.

Hawalimi, hawana uwezo wa kulima wala kuvuna lakini wana afya njema.

Wakati wote wamenawiri kuliko hata wakulima hutumia nguvu kubwa kulima kwa ajili yao wanawiri.

Hawa ni wadudu waharibifu wa mazao ambao ni adui mkubwa wa wakulima. Hujineemesha kwa kushambulia mazao tangu shambani mpaka nafaka zinapohifadhiwa ghalani.

Wadudu hao ni pamoja na dumuzi na kiwavi chake wanaoathiri mazao kama mahindi.

Ni wazi kwamba wadudu hao na wengine wamekuwa wakisababisha mateso kwa wakulima wengi, licha ya juhudi za kuwadhibiti ambazo zimekuwa zinafanywa.

Pamoja na kuwepo viuatilifu ambavyo hutumika katika kuwadhibiti wadudu wasishambulie mazao shambani, bado wengine hufanikiwa kushambulia baada ya kuvunwa.

Sailo kama mkombozi kwa wakulima

Wadudu wharibifu wakiwa kero kwa wakulima kwa kuwapa hasara, wataalamu hawapo nyuma kuwasaidia wakulima. Wamekuwa wakijitahidi kubuni mbinu mbalimbali za kuwadhibiti wadudu hao.

Miongoni mwa mbinu hizo ni pamoja na vifaa vya kiteknolojia vya kuhifadhi mazao baada ya kuvunwa ikiwamo ghala la kisasa liitwalo Sailo.

Kwa mujibu wa kitabu cha Teknolojia za Utayarishaji, Usindikaji na Hifadhi ya Mazao ya Nafaka baada ya Kuvuna kilichoandikwa na wataalam wa Wizara ya Kilimo mwaka 2013, kuna umuhimu mkubwa wa kuhifadhi nafaka kwenye ghala bora kama sailo.

Wataalamu wanasema sailo ni maghala yanayojengwa kwa dhana ya kutokuwepo na mzunguko wa kawaida wa hewa ndani yake.

Hatua hiyo husaidia wadudu waharibifu na vimelea vya magonjwa kutoweza kustawi na kuharibu nafaka kwa sababu wanakosa hewa.

Wataalamu hao wanabainisha kuwa Sailo hujengwa kwa kutumia bati la chuma ngumu kisha kusiribwa kwa matofali ya kuchoma au ya saruji.

Hata hivyo, wanabainisha kuwa Sailo za bati hazifai kujengwa katika maeneo ambayo mabadiliko ya vipindi vya joto na vya baridi ni makubwa kwa sababu wakati wa joto bati linapata joto kwa haraka.

Aidha, wakati wa baridi bati hupoa kwa haraka na kupa

ta unyevu kwa ndani, jambo ambalo husababisha nafaka au mazao jamii mikunde iliyohifadhiwa kuoza.

“Lengo la uandaaji wa kitabu hiki ni kuelimisha jamii kuhusu teknolojia sahihi za uvunaji, utayarishaji, ufungashaji, usindikaji na hifadhi ya mazao ya nafaka baada ya kuvuna,” inaelezwa.

Wanabainisha kuwa uwezo mdogo na maghala duni yanayotumiwa na wakulima vijijini kwa kuhifadhi, huruhusu upotevu wa nafaka hadi asilimia 10

“Huu ni mwongozo kwa wakulima na wadau wengine, ili kuziweka bayana teknolojia sahihi na mbinu bora za kutunza baadhi ya mazao ya nafaka baada ya kuvuna ili kupunguza

upotevu,” kinasema kitabu hicho.

Wanaeleza kuwa wakulima wengi nchini huhifadhi nafaka kwa kutumia njia za asili kama vile vilindo, mitungi au vibuyu ambazo ni duni na husababisha upotevu wa nafaka kwa kiasi kikubwa.

“Pia hifadhi ya namna hii mara nyingi haikidhi mahitaji ya kaya, ili kuepuka upotevu wa mazao wakati wa kuhifadhi, hivyo ni muhimu kutumia maghala bora yanayokidhi mahitaji ya mkulima.

Faida za Sailo

Hupunguza gharama kwa mkulima kununua magunia kila mwaka. Hutumia nafasi ndogo ya eneo la kuhifadhi. Huzuia wadudu waharibifu na wanyama kama vile pannya kuharibu nafaka.

Ni nzuri kwa ajili ya kuhifadhi mazao ya nafaka ambayo ni pamoja na mahindi, kunde, maharage na choroko. Lina sehemu ya juu ya kuwekea na sehemu ya chini ya kutolea nafaka.

Faida nyingine ni kudhibiti matumizi kwa kuweka kufuli, bei nafuu ili kumwezesha mkulima kumiliki na kuwa na usalama wa chakula. Linapatikana kwa ujazo mbalimbali kuanzia Kg250 hadi Kg 2000 kulingana na mahitaji.

Vyakula vya nafaka vinaaminika kuwa vinaweza kuhifadhiwa kwa muda mrefu ikilinganishwa na mazao mengine ya chakula.

Inabainishwa kuwa iwapo wakulima wakiitikia wito na kutumia teknolojia hiyo ya kisasa ambayo imefanyiwa utafiti, vyakula vyao vitakuwa salama .

Mwitikio wa wakulima kuhusu teknolojia hii

Mwenyekiti wa Kijiji cha Ulaya, wilayani Kilosa Julius Lumambo anaeleza kuwa wakulima wengi wamekuwa wakipoteza sehemu kubwa ya vyakula baada ya kuvuna kutokana na kukosa elimu.

“Kuna wakati tuliwekwa kwenye mradi wa kuzuia upotevu wa nafaka,lakini hakukuwa na mwitikio mzuri kwa wakulima, pengine wengi hupenda kuuza muda mfupi baada ya kuuza,” anasema.

Anasema kuwa hali hiyo imekuwa ikiwatesa wakulima wengi kwa njaa hasa inapozuka mabadiliko ya hali ya hewa, mvua ikiwa nyingi au ikichelewa kunyesha kwa wakati.

Mkulima Malekela Kayombo wa kijiji cha Malangali mkoani Iringa anaeleza kuwa anahifadhi mazao yake kwenye viroba.

“ Kuna watu wamepita kuja kutuelimisha kuhusu uhifadhi wa mazao kwenye Sailo, nimevutiwa nayo kwa sababu sitohitaji kunyunyuzia dawa kwenye mahindi au mazao mengine ya nafaka, jambo ambalo ni la kiafya zaidi,”anasema.

Kayombo anabainisha kuwa ameshindwa kuwa na kifaa hicho kwa sasa kwa sababu kinauzwa kwa gharama ya Sh190,000 ambapo ukubwa wake ni sasa na gunia 40, hivyo amejipanga kununua msimu mwingine wa mavuno.

Mkulima mwingine Laurian Mbale wa Kijiji cha Msolwa wilayani Kilosa, anasema kuwa kwa sasa amekuwa anahifadhi mazao yake kwa kutegemea kunyunyuzia dawa, lakini ana lengo la kununua kifaa hicho.

“ Natamani kununua kwa ajili ya kuhifadhi mahindi maana pamoja na kwamba nalima na mpunga, lakini wadudu wanashambulia zaidi mahindi ingawa huwa najitahidi kuhakikisha yamekauka vizuri lakini bado wanasumbua,” anasema Mbale.