Samahani naombeni ‘mnisaidie kushea’ makala hii

Muktasari:

  • Darassa na muziki wake wamesumbua kwa miezi minne kama sikosei, kila aliyejaribu kutoa wimbo alibuma  au kama alipata airtime basi ilikuwa kidogo tu.

Mitandao ya simu nadhani ndizo kampuni pekee nchini zinazoendelea kupata faida kubwa katika mauzo ya data. Kwa Mtanzania mwenye smartphone wakati huu sidhani kama anaweza kukaa siku moja bila kununua data. Kuliko kupitwa na ubuyu mitandaoni ni bora kukosa kula.

Mambo yamekuwa mengi kiasi kwamba kuna vitu vizuri vinatokea katika tasnia ya burudani halafu havipati tena kiki au nafasi ya kung’aa katika media zetu na mitandao ya kijamii.

Darassa na muziki wake wamesumbua kwa miezi minne kama sikosei, kila aliyejaribu kutoa wimbo alibuma  au kama alipata airtime basi ilikuwa kidogo tu.

Nakumbuka kuusikia wimbo wa Darassa ukipigwa hata mara tano kwa siku katika kituo kimoja cha redio au televisheni na huko klabu usiseme.

Lakini hapo katikati upepo wa mjadala ukabadilika, kiki zikachukuliwa na wenye kiki zao. Kwa miezi miwili sasa ni watu wachache wanaofuatilia burudani ndiyo wanaweza kuwa na taarifa sahihi za kinachotokea katika tasnia hiyo.

Kuna mapinduzi yamefanyika katika filamu lakini ni kama vile sicho tulichokuwa tukikipigania. Filamu ya Homecoming imezinduliwa kwa kishindo lakini mwangwi wake umeshindwa kuakisi kutokana na kinachoendelea nchini.

Nimeamua kuandika kuwakumbusha na kuweka kumbukumbu kuwa katikati ya yanayotokea nchini, kwenye burudani kuna vitu vinaendelea.

Jay Mo ametoa wimbo wake Nisaidie Kushare, Profesa Jay ametoa wimbo wake alioubatiza jina Kibabe, Shishi Trump naye ameachia ngoma yake Hatutoi Kiki na Baraka The Prince ameingiza mtaani wimbo wake Niende.

WCB nao wameathirika katika hili kwani Harmonize naye ametoa wimbo Niambie na bila kusahau Rockonolo wa Lomino ambao Diamond ameshirikishwa nao upo hewani.

Ollah wa Christian Bella akishirikiana na Kalighaph Jones wa Kenya  nao upo kwenye chati mbalimbali nchini hivyo ni vyema kuliweka katika kumbukumbu zetu.

Najua zimetoka nyimbo nyingi na video za kutosha hivyo sitaweza kuziweka katika kumbukumbu hii lakini ikumbukwe kuwa kuna mambo yanafanyika katika tasnia nyingine nchini na mimi kama mdau inabidi nisaidie kuwakumbusha.

Katika kuweka sawa kumbukumbu nyingine ni kwamba Baraza la Sanaa (Basata) limetangaza kutoa tuzo kwa wanafunzi waliofanya vizuri katika masomo ya sanaa ili kuwahamasisha waendeleze vipaji.

Huenda kuna mengine yamenipita kwa sababu na mimi sipo nyuma katika kufuatilia yanayojiri nchini.