Teknolojia ya Aflasafe inavyoondoa sumu kuvu kwenye mazao

Mtafiti mshiriki wa sumu kuvu, Jacob Njela, akielezea jinsi teknolojia ya Aflasafe inavyofanya kazi kwenye mazao. Picha na Asna Kaniki

Muktasari:

  • Mazao kama karanga, mahindi na yale ya jamii ya mizizi na kunde, mara nyingi wanalalamika mazao yao kushambuliwa na fangasi ambao huzalisha kemikali za sumu, maarufu sumu kuvu.
  • Hii ni sumu na watumiaji wasipochukua tahadhari, afya zao ziko shakani na pengine wanaweza kupoteza maisha.

Wakulima wengi hasa wa mazao ya nafaka, wanatambua namna wadudu wanavyosumbua mazao yao.

Mazao kama karanga, mahindi na yale ya jamii ya mizizi na kunde, mara nyingi wanalalamika mazao yao kushambuliwa na fangasi ambao huzalisha kemikali za sumu, maarufu sumu kuvu.

Hii ni sumu na watumiaji wasipochukua tahadhari, afya zao ziko shakani na pengine wanaweza kupoteza maisha.

Habari njema

Baada ya tatizo hili kuonekana kuwa kubwa kwa wakulima nchini timu ya wanasayansi kutoka Taasisi ya kimataifa ya Kilimo cha Kitropiki (Ukanda wa joto) (IITA, imeegundua teknolojia itwayo Aflasafe kama tiba ya changamoto hiyo.

Kupitia teknolojia hiyo, sasa mkulima anaweza kulima mazao yake huku akiwa na uhakika wa kuvuna yakiwa salama.

Wataalamu hawa wanatengeneza Aflasafe kwa kutumia mchanganyiko wa mtama mweupe , rangi ya bluu, gundi pamoja na fangasi asilia wajulikanao kama “A.flavus” ambao hawazalishi sumu na ni salama kwa mkulima.

Jacob Njela ni mtafiti mshiriki wa kudhibiti sumu kuvu kwenye mimea amesema teknolojia hiyo ina uwezo wa kupunguza sumu kuvu katika mazao kwa asilimia 80 hadi 99.

“Mwaka jana tuliijaribu katika wilaya za Babati, Masasi, Kilombero, Nanyumbu, Mpwapwa, Kilosa, na Kongwa na ikaleta matokeo mazuri na sasa tupo katika jaribio la pili,”anasema.

Anasema kwa kushirikiana na Shirika la Chakula Duniani (FAO) wameongeza wilaya nyingine nne ambazi ni Chemba, Kondoa, Kiteto na Chamwino katika jaribia la pili la msimu wa pili.

Anasema kwa kuwa fangasi wanaotengeneza sumu kuvu huingia shambani kipindi mazao yanapotoa maua,hivyo ili kudhibiti wadudu hao wasiingie Aflasafe inapelekwa shambani wiki mbili kabla ya mazao kutoa maua.

Lengo la wataalamu hao kupeleka Aflasafe shambani mapema ni kutoa nafasi kwa fangasi hao wasiozalisha sumu, ya kuzaliana wakiwa shambani hapo ili wakue na kukomaa tayari kwa ajili ya kuthibiti sumu kuvu.

“Kwa kipindi hiki tuna uhakika kabisa kwamba sumu kuvu haitakuwa na uwezo kabisa wa kuingia shamba kwani hawezi kushindana na Aflasafe kwa chakula, kwa hewa na hatimaye watakimbia kwa kuwa hawatapata nafasi ya kuwepo shambani,” anaeleza

Njela anasema kwa mkulima mwenye ekari moja atapaswa kutumia kilo 10 tu za Aflasafe.

Sababu ya kugunduliwa teknolojia hii

Madhara makubwa yatokanayo na sumu kuvu ndio hasa sababu ya wataalamu hawa kubuni teknolojia hiyo ambayo itakuwa suluhisho la madhara hayo kwa wakulima lakini pia hata kwa wale ambao wanatumia mazao hayo kama chakula.

Anasema sumu kuvu haiathiri afya pekee bali hata soko kwa mkulima, mazao yaliyoshambuliwa na sumu kuvu hayafanyi vizuri sokoni hasa masoko ya nje kama vile Ulaya.

Mbali na soko la nje, Njela anasema hata hapa nchini ni vigumu kwa mkulima kupata kipato kwa kuuza mazao ambayo tayari yamekwisha shambuliwa na sumu kuvu.

“Teknolojia hii ya Aflasafe kama itatumika vizuri na kwa usahihi itamsaidia mkulima katika kudhibiti sumu kuvu ambao ndio adui wa maendeleo ya mkulima nchini kiafaya na kimasoko” anasema

Anasema lengo la teknolojia hii sio kibishara ila lengo ni kuona wananchi wanakuwa salama dhidi ya sumu hatari ambao wanaweza kusababisha magonjwa mbalimbali ya hatari ikiwemo kansa.

Anasema pia Aflasafe ikitumika vizuri itaweza kupunguza fangasi wanaozalisha sumu na itaongeza wale wasiozalisha sumu na wasio na madhara kwa mkulima na jamii kwa jumla.

Tamko la Serikali kuhusu Aflasafe

Beatrice Pallangyo ni Ofisa mfawidhi wa udhibiti wa visumbufu uvamizi wa mimea kutoka Wizara ya Kilimo, anayesema kama nchi itafanikiwa kupunguza sumu kuvu, itaboresha afya pamoja na kipato kwa wakulima.

Anasema teknolojia hiyo ya aflasafe itasaidia kupunguza hatari za sumu kuvu kufuatia kufanya vizuri katika jaribio la kwanza katika wilaya saba hapa nchini.

“Aflasafe imesajiliwa na inatumika pia katika nchi za Marekani, Nigeria na Kenya hivyo kwa kuwa sumu kuvu ni tatizo hapa nchini na sisi tupo katika hatua ya kusajili bidhaa hiyo ili iweze kutumika mashambani kama njia ya kudhibiti,”anasema na kuongeza:

“Katika kufanikisha hili, Serikali itafanya utafiti kupita katika maeneo yote yanayosumbuliwa na tatizo hili, ili kuwarahisishia kutambua mapema kabla ya kuanza kusambaza bidhaa hiyo,”.

Hii ni habari njema kwa wakulima Kwani kwa miaka kadhaa suala hili la sumu kuvu limekuwa likidhoofisha mazao yao pamoja na mifugo kwani nayo hufa kwa sumu kuvu.

Kama ilivyo ada, matumizi ya teknolojia bila elimu hayawezi kuleta mafanikio mazuri.

Pallangyo anasema kwa kuwa bidhaa hii imethibitika kudhibiti sumu kuvu, Serikali itaenda sambamba na kutoa elimu kwa wakulimu juu ya umuhimu wa Aflasafe.