Uaminifu unazidi kuwa bidhaa iliyopitwa na wakati

Labda umeshawahi kukutana na visa kama hivi. Ndugu au jamaa ana kupigia simu akikuomba umkopeshe kiasi fulani cha fedha na kuahidi kukurudishia siku tatu baadaye. Kwa mfano, anakupigia simu Alhamisi na kuahidi kuwa Jumamosi atakurudishia.

Huenda nawe huna kitu siku hiyo na kwa kuwa unataka kumsaidia kweli, unamwambia asikilizie kidogo ili na wewe utafute. Inapita siku, kesho yake anakupigia kuuliza kama umefanikiwa unamwambia bado unatafuta.

Ijumaa nayo inapita hakijaeleweka, inaingia Jumamosi ambayo alikuahidi kukulipa kama ungemkopesha kwa kuwa mipango yake ingetiki siku hiyo, lakini la kustaajabisha anakupigia simu kuulizia ule mtonyo uliomwahidi kumkopesha.

Sasa mtu alikuahidi kuwa angerudishia fedha hizo Jumamosi halafu siku hiyo anakupigia kukuulizia kama umepata. Maana yake alipanga kukudanganya na inawezekana hana kabisa mpango wa kukulipa. Mimi na wewe ni mashahidi kwa kiasi gani madeni yamevunja urafiki na kuwafarakanisha ndugu.

Kuchukuliana wapenzi sasa hivi ni fasheni, yale mambo ya kumwamini rafiki yako kuwa mlinzi wa penzi lako yamepitwa na wakati.

Zamani kulikuwa na msemo kuwa mtoto ni wa jamii nzima lakini siyo sasa. Mtoto anachungwa kuliko kitu chochote kwa sababu ukizubaa utakuja kulia kwa kitakachomtokea. Siyo mtu baki, hata ndugu haaminiki kuachiwa mtoto siku hizi.

Sasa hivi unapiga tu kura kwa kuwa hakuna jinsi. Unaanzaje sasa kumuamini mwanasiasa! Kwa kuwa hakuna namna inabidi ukubali tu kumpa mtu ulaji huku ukijua kabisa unapigwa changa la macho.

Ukisikia ving’ora vya gari la wagonjwa  barabarani unalipisha tu lakini moyoni unajisemea inawezekana hakuna hata mgonjwa.

Ndio. Tumeshazisikia sana hadithi za watu kutumia magari hayo kufanikisha shughuli zao za kila siku kwa hadaa kuwa wanawawahisha wagonjwa mahututi.

Umuamini nani? Polisi, daktari,  hakimu au kiongozi wa dini? Kila mmoja ana jibu lake lakini imefikia mahali hata majibu ya daktari inabidi ukajiridhishe kwa kupima katika hospitali nyinyine, kwa nini? Kwa sababu biashara imeondoa utu.

Yaani daktari hajali madhara ya dawa atakazokuandikia kwa afya yako kwa kuwa anachotaka kufanya ni kuona anaingiza fedha.

Wangapi wapo magerezani kwa makosa ya kusingiziwa. Wangapi wanaishi kwa hofu kwa sababu wakisema ukweli wataumia? Wengi tu.
Sms 0744 053 111