Uhusiano wa ufaulu wa darasani na mahitaji ya soko la ajira

Muktasari:

  • Nilifanikiwa pia kukutana na watu hasa wanafunzi waliokuwa mwaka wa pili na watatu walionishauri nisome kwa bidii ili nipate alama nzuri darasani. Watu hawa waliniambia ufaulu mzuri unafaida nyingi sana.

Nilipokuwa nikianza masomo yangu ya Shahada ya kwanza Chuo Kikuu cha Mzumbe niliwatafuta watu kadhaa wanishauri. Lengo langu lilikuwa ni kujua nitumie mikakati ipi ili nifanye vizuri kwenye masomo yangu. Wapo walionishauri kuwa chuoni ufaulu sio kitu cha muhimu sana hasa katika kupata ajira, huku wakinipa mifano ya watu waliokuwa na matokeo ya kawaida lakini wameshapata kazi huku wale waliofanya vizuri wakiendelea kutafuta kazi mtaani. Wengine walinithibitishia hakuna uhusiano kati ya ufaulu mzuri na ufanisi kazini.

Nilifanikiwa pia kukutana na watu hasa wanafunzi waliokuwa mwaka wa pili na watatu walionishauri nisome kwa bidii ili nipate alama nzuri darasani. Watu hawa waliniambia ufaulu mzuri unafaida nyingi sana.

Baada ya muda niligundua walionishauri kuwa ufaulu mzuri hauna maana sana kwa ngazi ya chuo kikuu walikuwa hawafanyi vizuri sana darasani na wale walionishauri niweke bidii kwenye masomo, walikuwa na ufaulu mzuri.

Baada ya muda niligundua wanafunzi wengi hukosa watu wa kuwashauri hasa kwenye masomo yao au pengine hushauriwa vibaya na hivyo kukosa motisha ya kufanya vizuri kwenye masomo yao.

Hivi sasa, vijana waliomaliza kidato cha sita na viwango vingine vya elimu wameshaanza masomo ya chuo kikuu katika ngazi mbalimbali huku wengine wakiendelea kujiunga na taasisi hizo.

Huu ni muda muafaka wa kuwashauri vijana hawa juu ya umuhimu wa kuwa na ufaulu mzuri.

Ufaulu na Upatikanaji wa ajira

Kuna vigezo kadhaa ambavyo waajiri huangalia pindi wanapotaka kumuajiri mtu yeyote, ufaulu ukiwa ni moja ya vigezo hivyo.

Ukweli ni kwamba, uzito wa vigezo unatofautiana kati ya kazi moja na nyingine.

INAENDELEA UK 24

INAENDELEA UK 24

Kwa kazi ambazo zinavutia watafutaji ajira wengi, ufaulu unaweza kutumika kama kigezo cha kuchuja watafuta ajira. Na zipo kazi ambazo huanisha kiwango cha ufaulu ambacho muombaji anatakiwa awenacho.

Yapo mashirika mengi sana ambayo huweka viwango vya ufaulu kama moja ya vigezo ambavyo waombaji wanatakiwa wawenavyo ili kupata ajira. Hii inaonesha kuwa watu wenye viwango vizuri vya ufaulu wana nafasi kubwa ya kupata ajira hizo kuliko wale ambao hawana viwango hivyo. Hii hupunguza ushindani katika kutafuta ajira ukizingatia kuwa soko la ajira limekuwa na ushindani zaidi ya kipindi chochote kwenye historia.

Ikumbukwe kuwa katika kusaili waombaji ajira mashirika mengi hutoa mitihani kabla ya usaili wa mahojiano. Hii pia inatoa fursa kwa watu wanaotia juhudi kwenye masomo yao na kujua mambo mengi juu ya taaluma zao na hata yale ya nje ya taaluma zao. Taasisi nyingi pia zinazotoa ufadhili katika ngazi mbali mbali za elimu huangalia ufaulu kama kigezo cha kutoa ufadhili.

Ufaulu na Uwezo wa Kujiajiri

Hivi karibuni kumezuka wimbi la watu wengi wanaobeza ufaulu kwa kusema kuwa mara nyingi hawa wanaofaulu vizuri mwisho wa siku huajiriwa na wale waliofanya vibaya darasani au wenye ufaulu wa wastani na wakati mwingine wale ambao hawakumaliza masomo yao kabisa. Wengine wamefika kiwango cha kuwakatisha tamaa wale wenye nia ya kufanya vizuri darasani kwamba eti hata wakifanya vibaya watajiajiri. Ushawishi wao umefika kiwango cha kutoa mifano ya watu walio katiza masomo yao kama Bill Gates (mwanzilishi wa Microsoft), Mark Zuckerberg (mwanzilishi wa facebook), Steve Jobs (Mwanzilishi wa kampuni ya Apple) na wengine bila kuwaelezea uwezo walikuwa nao watu hao katika ujuzi wa vitu walivokuwa wakivifanya ambavyo kwa kiwango kikubwa waliupata shuleni.

Katika mifano wanayotoa uwa hawataji waanzilishi wa makampuni na watu waliofanikiwa kupitia elimu zao na kutambua mchango wa elimu za watu wengi katika kufikia malengo yao. Wengi wanaojiajiri ni wale wenye elimu za kawaida au ufaulu wa wastani kwa sababu nyingi ikiwemo ukweli kwamba mara nyingi wenye ufaulu mzuri sana uwa ni wachache hivyo kwa namna yoyote tutarajie wengi watakao jiajiri ni wale wenye ufaulu mdogo au ule wa wastani.

Pamoja na hayo tukubaliane kuwa bado tunahitajiana katika suala zima ajira na kujiajiri. Mtu anayeanzisha hospitali atahitaji daktari msomi na pengine mbobezi hivyo kujiajiri kwa wenye uwezo mdogo au wastani kusitumike kubeza wale wenye uwezo mzuri darasani au walio ajiriwa. Tuwakumbushe vijana umuhimu wa kujiajiri na kuwatia moyo wengine wafanye vizuri kwenye masomo yao.

Ufaulu na ufanisi kazini

Mjadala wa uhusiano kati ya ufaulu na ufanisi kazini umekuwa ikiendelea kwa miaka mingi kiasi cha kuvutia watafiti mbalimbali. Zipo tafiti zilizoonesha kuwa hakuna uhusiano kati ya ufaulu mzuri na ufanisi kazini. Wapo waajiri wanaolalamika kuwa wale wenye ufaulu mzuri sana uwa hawafanyi vizuri katika maeneo ya kazi. Zipo tafiti pia zilizothibitisha ubora wa wale wenye ufaulu mzuri darasani.

Changamoto za utoaji wa madaraja katika taasisi za elimu ni moja ya maeneo ya kulaumiwa kwani mara nyingi hupima uwezo wa wanafunzi katika nadharia zaidi kuliko vitendo. Pamoja na hayo ikumbukwe kuwa kufanya vibaya darasani hakukupi sifa ya kuwa mfanisi kazini. Wapo wenye ufaulu mzuri na ni wafanisi pia kwani juhudi kwa kila jambo ni muhimu hasa katika kujifunza.

Ufaulu darasani sio kitu pekee chenye umuhimu lakini ni moja ya mambo mengi. Wanafunzi wanashauriwa kuhakikisha wanajiongezea ujuzi kwenye mambo mengi ikiwemo suala la ujuzi wa mawasiliano, ubunifu, ujasirimali na mambo mengine. Ufaulu darasani pekee hautoshi kwani tumeshuhudia wataalam wenye elimu zinazoheshimika wakitia hasara mashirika na hata nchi kwa kufanya maamuzi yasio na tija wala maslahi kwa taasisi zao.

Ifahamike kuwa kuajiriwa pekee hakutoshi katika kuwa na uhuru wa kifedha. Kuna haja ya kuhakikisha waajiriwa wanajiongezea vyanzo vingine vya mapato kama biashara na kilimo kwani mahitaji yameongezeka sana kiasi kwamba ujira kutoka kwenye kazi za kuajiriwa kushindwa kukidhi mahitaji muhimu ya kila siku.

Mwisho, lengo la elimu sio kutajirisha wanufaika wa elimu bali kuwapa uwezo wa kutatua changamoto mbali mbali katika jamii. Tusiangaike kutafuta uhusiano kati ya utajiri na elimu bali elimu na ufumbuzi wa changamoto tunazozikabili ajira ikiwa ni moja tu ya changamoto nyingi.

Kelvin Mwita ni Mhadhiri Chuo Kikuu Mzumbe, 0659 081838, [email protected], www.kelvinmwita.com