Upandaji bangi majumbani uzunguni na madhara yake, kisirisiri...

Muktasari:

  • Matumizi ya dawa za kulevya ni kati ya “silaha” zinazotafutwa na wanaoshindwa kupambanua siri ya maisha yaani, uwiano. Ndiyo maana tukaumbwa na kushoto na kulia. Upande huu dhaifu mwingine wenye nguvu; ila vinategemeana.

Takwimu za shirika la Afya Duniani (WHO) zinaeleza mwaka 1960 asilimia 34 ya wanadamu tuliishi mijini. Idadi imefikia 54, kipindi tulichopo. Ongezeko limeleta kubanana banana na mabadiliko mabaya na mazuri. Wanadamu tunaoshindwa kukabiliana na harakati ama tunaparamia “masuluhisho hewa”.(ushabiki wa kila aina) au unyamavu na amani.

Matumizi ya dawa za kulevya ni kati ya “silaha” zinazotafutwa na wanaoshindwa kupambanua siri ya maisha yaani, uwiano. Ndiyo maana tukaumbwa na kushoto na kulia. Upande huu dhaifu mwingine wenye nguvu; ila vinategemeana.

Ukiacha ugaidi, ujambazi (biashara) wa dawa za kulevya unawaumiza sana vichwa wanausalama duniani. Ugaidi unaotughasi sasa hivi umetokana na siasa nyeti za Mashariki ya Kati ambazo hazikufumbuliwa sawasawa. Tatizo si udini.

Dawa za kulevya ni binti wa akili muflisi zilizoshindwa kupambanua pikipiki na baiskeli.

Sasa hivi Ulaya pamezuka wimbi jipya la bangi. Upandaji bangi majumbani, ni mgumu kutokana na hali ya hewa ya mvua na baridi Uzunguni. Pili, kuwepo kwa kamera doria (usalama) za video (CCTV), kila mtaa. “Kilimo” hiki ki sambamba na “mifugo bandia.”

Kuku, ng’ombe, kondoo , bata mzinga,na samaki wanafugwa ndani kupitia taa za umeme (badala ya jua asilia) ; matokeo nyama na mayai si tuliyozoea zamani. Bahati mbaya ufugaji huu “rahisi” ni mzuri kifedha. Kuku anayechukua miezi 6 na zaidi anahitaji majuma matatu tu. Vitoweo hivi ni vya bei nafuu, havina ladha, vinadhuru miili na watoto leo wanazaliwa na kila sampuli ya “maradhi siri.”

Hilo ndilo shimo ambalo bangi imedumbukia siku hizi. Humiminiwa takataka kadhaa (“toxins”) kuyakuuza majani hayo haraka.

Kawaida bangi ina kucha mbili.

Majani yake na mbegu au maua.

Vipimo vya nishai ya bangi vilivyofanywa mara ya kwanza mwaka 1840 viling’amua nishai yake huingia moja kwa moja ubongoni. . Ndiyo kisa cha watumiaji hupata maradhi ya usahaulifu na ulemavu wa akili (wazimu). Kiini cha bangi (“tetrahydroCANABIDINOL”) , yaani THC, ndicho huzaa nishai na kubatilisha ufahamu. Kwa uangalifu wa waganga, sehemu ndogo ya kiini yaweza kutuliza baadhi ya maradhi yenye maumivu makali, kama inavyofanyika Marekani.

Neno CANABIDINOL ndiyo limezua Cannabis. Hadi miaka ya Themanini kiasi cha THC (Sumu) katika bangi kilikuwa asilimia 1 au 2 tu. Leo kimefika asilimia 16.

Bangi inayolimwa majumbani inageuka sumu ya kisirisiri. Inaitwa “Skunk” (tamka Skank) na kusababisha ugomvi, wazimu, uhalifu, ajali za magari, kujiua, na kuua. Magaidi hung’wafua dawa za hizi za kulevya kabla ya kufanya ushetani wao.

Kwa miezi kadhaa askari Uingereza wamekamata “wakulima” wenye viwanda majumbani. Tatizo?

Wapandaji hupewa onyo na kuachiwa.

Wiki chache zilizopita mama aliyekuwa mwalimu wa elimu viumbe (biolojia), aliandika barua gazetini akilalamika kuwaachia majambazi hawa ni noma.

Mary Brett akasisitiza:

“Bangi inazua saratani, maradhi ya moyo,kiharusi, na kunyanyapaa kinga maradhi. Watoto wanaozaliwa na kina mama wavutaji huwa wadogo kiumbo, akili dhaifu na matatizo ya kitabia...wanaume wavutaji huwa na matatizo ya uhanithi na utasa...”

Akaongeza ukianza na bangi hatimaye unataka kutumia dawa kali zaidi.