Utafiti; Motisha kwa walimu itaondoa mbumbumbu

Muktasari:

  • Ni ukweli usiopingika kwamba hakuna mwanafunzi anayeweza kuvuka darasa pasipo jitihada za mwalimu.

Kujua kusoma, kuhesabu na kuandika, hutegemea mwalimu.

Ni ukweli usiopingika kwamba hakuna mwanafunzi anayeweza kuvuka darasa pasipo jitihada za mwalimu.

Ni mwalimu huyohuyo pia anaweza kusababisha wanafunzi wakahama madarasa na hatimaye kuhitimu elimu ya msingi wakiwa mbumbumbu.

Utafiti wa ‘Uwezo’ chini ya uratibu wa shirika la Twaweza, uliofanyika mwaka jana, unaonyesha kati ya wanafunzi 10 wanaomaliza darasa la saba, watatu hawawezi kufanya hesabu za darasa la pili, wakati nusu ya wanaomaliza elimu hiyo sawa na asilimia 49.1, hawawezi kusoma hadithi kwa Kiingereza.

Mkurugenzi wa shirika hilo, Aidan Eyakuze anasema changamoto za wanafunzi kushindwa kujifunza,ndiyo iliyowasukuma kufanya utafiti mwingine wa namna ya kuboresha ufundishaji.

Japo upo usemi kwamba ualimu ni wito, bado ari ya walimu kufundisha inaweza kuongezeka mara dufu wanapothaminiwa ikiwamo kupewa motisha.

“Tunaitaka Tanzania ya viwanda, lakini ili tuifikie ni lazima kuhakikisha watoto wetu wanajua kusoma, kuhesabu na kuandika. Mwalimu ndio chanzo cha uwezo na uelewa wa watoto wetu hivyo kukiwa na walimu bora watoto watajifunza,” anasema.

Kwa mujibu wa matokeo ya utafiti wa ‘KiuFunza’, kuwalipa walimu motisha kunaongeza ari ya kufundisha na kuleta matokeo chanya ya wanafunzi kujifunza.

Katika utafiti huo, asilimia 91 ya walimu waliohojiwa wanakiri kuwa motisha ni dawa ya kuongeza kiu ya kufundisha na kufaulisha.

Eyakuze anasema utafiti wao unaonyesha kuwa walimu na uwajibikaji ni mambo ambayo yamekosekana shuleni na ndiyo yanayochangia kupunguza kiwango cha kujifunza.

INAENDELEA UK 16

INATOKA UK 15

“Motisha inaweza kuboresha matokeo ya kujifunza, japokuwa kujifunza kunachangiwa na mambo mengi. utafiti huu unaonyesha kuwa kuchanganya motisha na uwajibikaji kutaleta matokeo mazuri,” alisema.

Utafiti ulivyofanyika

Twaweza katika utafiti wao walitoa kati ya Sh8, 100 hadi Sh3.6 milioni kama motisha kwa walimu 788.

Awali fedha hiyo iliahidiwa kwa walimu mwanzo wa mwaka, kwamba mwisho wa mwaka wale watakaowawezeha wanafunzi wao kupata stadi za kujifunza, watapewa motisha.

Eyakuze anasema utafiti huo uliwalenga wanafunzi wa darasa la kwanza, pili na tatu na uliwahusisha wanafunzi 65,643 katika shule za msingi 135 za wilaya 21 nchini, katika kipindi cha miaka miwili.

Hata hivyo uwiano ulikuwa kati ya shule zilizo na walimu walipewa motisha na zile zisizo na walimu waliopewa motisha.

Mkurugenzi huyo wa Twaweza anasema wanafunzi 48,042 waliokuwa kwenye shule zilizopewa motisha waliweza kujifunza zaidi kuliko wenzao waliokuwa kwenye shule zisizo na walimu waliopewa motisha.

Kutokana na utafiti huo, watoto waliofunzishwa na walimu wenye motisha walikuwa na uwezo wa kujifunza zaidi na kuelewa zaidi stadi za kujifunza kuliko wenzao.

Kulingana na utafiti huo, mtoto aliyefundishwa na mwalimu aliyepewa motisha anauwezo wa kujifunza stadi kwa mwaka mmoja wakati mwingine, anatumia mwaka mmoja na nusu.

“Watoto waliofundishwa na mwalimu aliyeahidiwa motisha anaelewa zaidi kuliko anayefundishwa na walimu asiye na motisha,” anasisitiza.

Mkurugenzi huyo wa Twaweza anasema ni ukweli usiopingika kwamba fedha ni kichocheo kikubwa cha mtu yeyote kufanya vizuri kwenye kile anachokifanya.

Hivyo fedha inaweza kutumika kama kichocheo cha motisha kwa walimu, na kuongeza ufaulu.

Walimu wazungumzia utafiti

Walimu waliofikiwa na utafiti huo wanakiri kuwa motisha inaongeza ari ya kazi.

Mwalimu wa shule ya Msingi Mtongani Jijini Dar es Salaam, Hellen Mbogo anasema motisha inaweza kumfanya mwalimu akapata mbinu nyingine mpya za kuhakikisha mwanafunzi anafanya vizuri ikiwamo, kumfuatilia kwa wazazi wake.

“Darasa langu lina wanafunzi 250 ambao huwa nawagawa kwenye makundi, hatuwezi kuwafundisha pamoja kwa sababu ya uwingi,”anasema.

Anasema kwenye shule yake, wameanzisha darasa maalum kwa ajili ya kuwasaidia wanafunzi wanaojifunza polepole ili kuwanoa jambo lililosababisha ifanye vizuri wakati wa utafiti.

Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mbweni jijini Dar es Salaam, Moses Amani anasema mfanyakazi yeyote anapopewa motisha kwenye kazi anayoifanya, anaongeza uwezo wa kuelewa na kufanya.

“Nilipata pia motisha kwenye huu utafiti, kwa kweli inaongeza ari ya kazi kwa sababu ilitufanya walimu kushirikiana na kufanya kazi pamoja,” anaeleza.

Mratibu wa utafiti huo Wilaya ya Kinondoni, Sofia Komba anasema awali walipowapelekea walimu suala la kupewa posho mwisho wa mwaka watakapofanya vizuri kiufundishaji, wengi walipuuza wakiona haiwezekani.

Lakini mwaka wa kwanza wa utafiti, walimu walioingia kwenye utafiti huo walipewa posho jambo lililosababisha wengine kuongezeka kwenye utafiti kwa mwaka wa pili.

Upo umihimu wa Serikali kutunza sera itakayoelezea masuala ya motisha, ikiwa kweli tunataka kuhakikisha hakuna mwanafunzi atakayeachwa nyumba kitaaluma.

Wachambuzi wazungumza

Baadhi ya wadau wa elimu wamekiri kwamba motisha inaweza kuongeza ari ya kufundisha na kufaulisha lakini wamekosoa utafiti huo kuwa sio motisha ya fedha (Bahshish) kwa walimu ndiyo kunaweza kunaweza kuongeza ufaulu kwa wanafunzi.

Mchambuzi wa masuala ya elimu, Profesa Marjorie Mbilinyi anasema fedha sio motisha peke yake inayoweza kutumika kuwapima walimu, katika kuwaongezea ari ya kujifunza.

Anasema pamoja na fedha, Twaweza wangeweza kutizama aina nyingine ya motisha ambayo, walimu wanaweza kupatiwa katika kuongeza ari ya kufundisha shuleni.

Profesa Mbilinyi anaeleza kuwa mazingira mazuri ya kufundishia, sehemu nzuri za kuishi na uboreshaji wa mfumo wa ufundishaji vinaweza kuwa motosha kwa walimu.

Mshauri wa Elimu, Beatrice Omary anasema utafiti huo haukuweza kuonyesha jitihada zilizowahi kufanywa na Serikali au mashirika mengine katika kuboresha mazingira ya walimu.

Anasema kabla ya utafiti wao, walipaswa kuangalia kazi nyingine zilizofanywa ili kujua matokeo gani yalipatikana.

“Ili kujua kama kumpatia mwalimu pesa moja kwa moja kutasaidia basi zingeangaliwa jitihada nyingine zilizowahi kufanywa zimefanyaje,” anahoji.

Mkuu wa Kitengo cha Utafiti cha Baraza la Mitihani nchini, Dk Alfred Mdimo anasema kwa sababu katika uwasilishaji wa utafiti huo walitoa takwimu zinazoonyesha asilimia 30 ya wanafunzi wanaofikia darasa la saba hawana stadi za kujifunzia za darasa la pili, wangekuja na suluhisho la kuondoa tatizo hilo.

“Utafiti wao ungeonyesha pia katika hao walimu walioahidiwa kupewa motisha, wangapi waliwezesha wanafunzi waliokuwa hawajui kusoma na kuandika kujua, na wale walioshindwa,” anaeleza.

Naye Mwakilishi wa Shirika la Kuhudumia watoto la Umoja wa Mataifa (Unicef), Audast Muhina anasema ni kweli kwamba motisha inaweza kuongeza ufaulu japo fedha sio njia peke yake ya kumpa motisha mwalimu.

Anasema huenda matumizi ya fedha yakawa makubwa zaidi ikiwa njia hiyo itatumika kwenye kumpa motisha mwalimu ili kumuongezea ari ya kufunzisha.