Waafrika hawawezi kumsahau Sepp Blatter

Muktasari:

  • Haikuwahi kutokea lakini Afrika ikaandaa. Afrika Kusini ilipewa kazi ya kujipanga na jukumu hilo lilifanyika tangu mwaka 2006.

Pamoja na kupatwa na kashfa zilizomng’oa madarakani, kamwe Waafrika hawawezi kumsahau Rais wa zamani wa Fifa, Sepp Blatter ambaye alipambana kwa hali na mali tangu 2006, Afrika kuwa mwenyeji wa Fainali za Kombe la Dunia.

Haikuwahi kutokea lakini Afrika ikaandaa. Afrika Kusini ilipewa kazi ya kujipanga na jukumu hilo lilifanyika tangu mwaka 2006.

Ukweli kulikuwa na fitna za mataifa yaliyoendelea, yaliona Afrika haiwezi kuwa mwenyeji lakini Blatter alisimama kidete na kusisitiza Afrika Kusini itaweza na Bara la Afrika litakuwa mwenyeji wa Fainali za Kombe la Dunia 2010.

Katika moja ya kauli zake alizozitoa kwenye mkutano uliofanyika kwa ajili ya kupata wenyeji wa Kombe la Dunia alisema kabla hajaondoka, anataka aone Afrika ikiandaa fainali hizo. Mataifa yaliyokuwa yakiwania Fainali za 2010 ni England, Afrika Kusini yenyewe, Ujerumani, Morocco na Brazil

Wafuatao ni marais ambao ama walikaimu au waliongoza Fifa kama marais wake. Infantino ni kiongozi wa 12 katika mlolongo wa watawala ndani ya Shirikisho la Kimataifa la Soka, Fifa.

1.Rais wa kwanza wa Fifa alikuwa Robert Guérin ambaye ni Mfaransa ambaye alizaliwa Juni 28, 1876 na alifariki Machi 19, 1952 (akiwa na miaka 75). Aliiongoza Fifa kwa miaka miwili, aliingia madarakani Mei 23, 1904 hadi Juni 4, 1906.

2.Daniel Burley Woolfall, raia wa Uingereza. Alizaliwa Juni 15, 1852 na alifariki Oktoba 24, 1918 (akiwa na miaka 66) Aliiongoza Fifa kuanzia Juni 4, 1906 hadi Oktoba 24, 1918.

3.Cornelis August Wilhelm Hirschman, raia wa Uholanzi. Alizaliwa Februari 16, 1877 na alifariki Juni 26, 1951 (akiwa na miaka 74). Aliingia madarakani Oktoba 24, 1918 (akikaimu) hadi mwaka 1920.

4.Jules Rimet Raia wa Ufaransa, alizaliwa Oktoba 14, 1873 na alifariki Oktoba 16, 1956 (akiwa na miaka 83). Aliongoza Fifa kuanza 1920 hadi Machi 1, 1921.

5.Rodolphe Seeldrayers, raia wa Ubelgiji, alizalia Desemba 16, 1876 na alifariki Oktoba 7, 1955 (akiwa na miaka 78). Aliingia madarakani Juni 21, 1954 hadi Oktoba 7, 1955.

6.Raia wa Uingereza, Arthur Drewry alizaliwa Machi 3, 1891 na alifariki Machi 25, 1961 (akiwa na miaka 70). Alikaimu nafasi Fifa kuanzia Oktoba 7, 1955 hadi Juni 9, 1956.

7.Ernst Thommen, raia wa Uswisi alizaliwa Januari 23, 1899 na alifariki Mei 14, 1967 (akiwa na miaka 68). Aliingia Fifa akikaimu Machi 25, 1961 hadi Septemba 28, 1961.

8.Raia wa Uingereza, Stanley Rous alizaliwa Aprili 25, 1895 na alifariki Julai 1986 (akiwa na miaka 91). Aliingia ofisini Septemba 28, 1961 hadi Mei 8, 1974.

9.João Havelange, Mbrazil aliyezaliwa Mei 8, 1916 na alifariki Agosti 16, 2016 (akiwa na miaka 100). Aliongoza Fifa kuanza Mei 8, 1974 hadi Juni 8, 1998.

10.Sepp Blatter, Raia wa Uswisi alizaliwa Machi 10, 1936 (ana miaka 81). Bado anaishi na aliiongoza Fifa kuanzia Juni 8, 1998 hadi Oktoba 2015 (alisimamishwa).

11.Issa Hayatou, raia wa Cameroon, alizaliwa Agosti, 9 1946 (ana miaka 71). Alikaimu urais Fifa, Oktoba 8, 2015 hadi Februari 26, 2016.

12.Gianni Infantino, raia wa Uswisi-Italia. Alizaliwa Machi 23, 1970 (ana miaka 47). Aliingia madarakani Februari 26, 2016 hadi sasa.