Wakitokea kina Rado watano tu Bongo Movie itasimama

Muktasari:

  • Miaka miwili iliyopita soko la filamu za Bongo nchini lilikufa kabisa. Ray na wenzake waliokuwa wakitoa filamu kila mwezi wakatoweka kwenye shelfu za maduka ya filamu. Wakorea, Wazungu na Wahindi wakarudi kwenye chati.

Ni kawaida yetu binadamu linapotokea tatizo kutafuta kichaka cha kujificha. Ni wachache ambao hurudi nyuma kuangalia wapi walijikwaa na kuanza upya.

Miaka miwili iliyopita soko la filamu za Bongo nchini lilikufa kabisa. Ray na wenzake waliokuwa wakitoa filamu kila mwezi wakatoweka kwenye shelfu za maduka ya filamu. Wakorea, Wazungu na Wahindi wakarudi kwenye chati.

Cha kustaajabisha kila mmoja alikuwa na sababu zake za kuporomoka kwa soko la filamu. Wengi waliwalaumu ‘Wahindi’ na wengine wachache wakatangaza kabisa kuwa hawatatoa tena filamu mpaka mdosi atakapokubaliana na matakwa yao.

Wengine walisema kilichowaangusha ni kujiingiza katika siasa hasa katika uchaguzi mkuu wa mwaka juzi. Wasanii waligawanyika na wengine walihama toka kada moja kwenye nyingine kila dakika.

Wachache akiwamo nguli wa filamu za Kiswazi, Riyama Ally alikiri kuwa anguko la filamu ni ubora na si kitu kingine. Alisema mashabiki wamechoshwa kuibiwa kwa kuwahadaa kwa makava mazuri lakini ndani kilichowekwa ni utumbo mtupu.

Kwa kiasi kikubwa hicho ndicho kilichoangusha soko la filamu. Ubora! Mdosi alichangia kuangusha soko kwa sababu Bongo Movie wenyewe walimwacha awapangie nini cha kufanya. Mdosi alitoa fedha na maagizo ya majina ya watu anaowataka ndani ya filamu. Mwongozaji atajua atakachofanya lakini ahakikishe majina tajwa yamo ndani.

Wiki iliyopita mwigizaji Rado alizindua filamu yake Bei Kali. Ni filamu nzuri kwa kila kitu. Lakini kinachofanya niamini kuwa wakitokea kina Rado watano Bongo Movie itarudi kwenye mstari ni uthubutu wake.

Pamoja na changamoto na kubezwa amejifunga mkanda na kutoa filamu. Ni ujasiri wa kipekee. Wengine wamesusa na baadhi wamejificha nyuma ya kichaka cha kutengeneza tamthilia kwa maana wamekubali filamu ndiyo basi tena.

Kitendo cha kutoa filamu wakati Wadosi hawataki kuzinunua wakiamini haizuziki ni cha kishujaa na kinapaswa kuingiza kwenye kumbukumbu za tasnia hiyo.

Naamini soko la filamu bado lipo kubwa kwa sababu kiu ya Watanzania kuona kazi zinazowahusu haiwezi kukatwa na tamthilia na filamu za Wakorea na Wahindi. Kiu ya Mtanzania ni kuona filamu inayoakisi maisha ya mtu wa Tandale, Sinza au Mwanjelwa.

Rado aungwe mkono kwa kuwakomalia Wadosi kutotengeneza filamu wanazotaka wao bali walaji.